Al-Andalus

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru

Al-Andalus (Ar.: الأندلس) ilikuwa jina la Kiarabu kwa sehemu za Rasi ya Iberia (Hispania na Ureno wa leo) zilizotawaliwa kwa karne kadhaa na Waislamu kati ya miaka 711 and 1492.[1]

Kisiasa ilikuwa chini ya falme na watawala mbalimbali kwanza chini ya Wamuawiya, halafu Ukhalifa wa Cordoba (929-1031) na baadaye chini ya milki mbalimbali hasa Wamurabitun (Almoravi)(1073-1147) na Wamuwahidun (Almohad) (1125-1269) kutoka Moroko.

Kwa historia yake yote Al-Andalus ilikuwa kando ya milki za Wakristo katika kaskazini zilizokuwa mwanzoni chini ya nguvu ya Waislamu. Lakini polepole walijipatia uhuru wao wakaanza urudisha utawala wa kiislamu nyuma na kutwaa maeneo makubwa kutoka kwao. Tangu kuanguka kwa Cordoba mwaka 1236 emirati wa Granada ilikuwa dola la mwisho la Kiislamu la Hispania hadi ilikamatwa mwaka 1492 na malkia Isabella na ii ilikuwa mwisho wa watawala waislamu katika rasi ya Iberia.

Eneo la Al-Andalus chini ya makhalifa wa Cordoba mnamo mwaka 1000

Wakazi wa Al-Andalus[hariri | hariri chanzo]

Wakazi wa Al-Andalus walikuwa wa vikundi vitatu: Wakristo, Waislamu na Wayahudi.

Waislamu walitawala nchi. Mwanzoni walikuwa wachache waliofika kama wanajeshi waliokuwa mchanganyiko wa Waarabu na Waberber waliofuata Uislamu wa Kisunni. Katika miaka ya kwanza ni hasa makabaila Wakristo waliogeukia Uislamu kwa sababu waliweza kutunza mali na utawala wa kieneo kwa kuwa Waislamu. Baadaye watu wapya walifika kutoka pande mbalimbali za dunia ya Kiislamu. Wengine walikuwa watumwa Waslavoni walioitwa Saqaliba kutoka Ulaya ya Mashariki walionunuliwa na Waislamu na kutumiwa kama wanajeshi hasa. Baada ya kusilimu waliweza kupanda ngazi jeshini na serikalini.

Wakristo walikuwa kiasili mchanganyiko wa Waiberia asilia, Waroma na makabila mbalimbali wa Kigermanik waliofuata Ukristo wa kikatoliki.

Wayahudi walikuwa jumuiya iliyostawi kwa jumla chini ya utawala wa Kiislamu na hali yao ilkuwa juu ya wenzao katika maeneo chini ya utawala wa Kikristo.

Wakristo na Wayahudi walikuwa katika hali ya dhimmi chini ya Uislamu. Walipewa nafasi ya kufuata dini zao lakini hawakuwa na heshima na cheo sawa na Waislamu. Katika karne za kwanza walipata ustahimilivu mkubwa lakini tangu watawala kutoka Moroko kuchukua mamlaka ya Al-Andalus uhuru kwa wasio Waislamu ilipungua hadi kutokea kwa madhulumu dhidi ya Wyahudi na Wakristo.

Katika karne ya 8 na 9 polepole sehemu kubwa ya Wakristo walipokea Uislamu uliokuwa dini tawala. Mnamo mwaka 1100 takriban 80% za wakazi walikuwa Waislamu. Baadaye idadi yao ilipungua pamoja na uenezaji wa falme za Wakristo kutoka kaskazini.[19][20]

Mesquita ya Cordoba iliyokuwa msikiti kuu ya ukhalifa.

Utamaduni[hariri | hariri chanzo]

Chini ya watawala wa nasaba ya Muawiyya ushirikiano wa dini na tamaduni ulikuwa bora. Uhuru wa kiutamaduni ulikuwa mkubwa na hasa mji wa Cordoba ulikuwa maarufu kama kitovu cha taaluma na elimu. Wataalamu Wayahudi, Wakristo na Waislamu walishirikiana vizuri.

Kwa muda mrefu Al-Andalus ilikuwa tajiri kwa sababu ya hali ya juu ya kilimo na uchumi. Nguvu nyingine ilikuwa biashara ya dhahabu kutoka Afrika ya Mashariki iliyobebwa na wafanyabiashara Waislamu hadi Hispania na hapa kupelekwa kwenda Ulaya ya Kikristo. Cordoba kama mji mkuu wa makhalifa ilikuwa na wakazi wapatao 500,000 na hiyi mji mkubwa wa Ulaya kushinda Konstantinopoli.

Kurasa husika[hariri | hariri chanzo]

Marejeo[hariri | hariri chanzo]

  1. "Andalus, al-" Oxford Dictionary of Islam. John L. Esposito, Ed. Oxford University Press. 2003. Oxford Reference Online. Oxford University Press. Accessed 12 Juni 2006.

Bibliografia[hariri | hariri chanzo]

An Islamic History of Europe Archived 3 Novemba 2011 at the Wayback Machine.. video documentary, BBC 4, Agosti 2005.

  • Stavans, Ilan. 2003. The Scroll and the Cross: 1,000 Years of Jewish-Hispanic Literature. London: Routledge. ISBN 0-415-92930-X
  • Wasserstein, David J. 1995. Jewish élites in Al-Andalus. In Daniel Frank (Ed.). The Jews of Medieval Islam: Community, Society and Identity. Brill. ISBN 90-04-10404-6

Filamu[hariri | hariri chanzo]

Tovuti za Nje[hariri | hariri chanzo]