Amerika ya Kilatini

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Nchi za Amerika ya Kilatini zinazotumia lugha za Kihispania, Kireno na Kifaransa. Belize imo kwa sababu ya wasemaji wengi wa Kihispania.

Amerika ya Kilatini ni jina linalotumika kutaja sehemu kubwa ya Amerika.

Asili ya jina[hariri | hariri chanzo]

Amerika ya Kilatini humaanisha kwa kawaida nchi za Amerika ambako lugha za Kihispania na Kireno pamoja na Kifaransa hutumiwa kama lugha rasmi au lugha ya watu wengi. Lugha hizo zote zimetokana na Kilatini na hujumlishwa pamoja na nyingine kama "Lugha za Kirumi".

Nchi za Amerika ya Kilatini[hariri | hariri chanzo]

Kuna tofauti kuhusu ya namna ya kutaja nchi za Amerika ya Kilatini. Mara nyingi Amerika ya Kusini, Amerika ya Kati na Meksiko hutajwa hivyo kwa jumla. Lakini kuna nchi ndogo kama Guyana, Surinam na nchi za visiwani vya Karibi zinazotumia zaidi Kiingereza au Kiholanzi zisizo lugha za Kirumi. Nchi hizo wakati mwingine hujumlishwa pamoja ndani ya Amerika ya Kilatini lakini mara nyingi zinatazamwa kuwa za pekee kutokana na tofauti za utamaduni.

Kiutamaduni hata sehemu ya Marekani ya Kusini yenye wasemaji wengi wa Kihispania ni karibu sana na Amerika ya Kilatini. Majimbo hayo ya Marekani kama Texas na Kalifornia yalikuwa sehemu za Meksiko hadi karne ya 19.

Historia na utamaduni[hariri | hariri chanzo]

Kipaumbele cha lugha za Kirumi kimetokana na historia. Baada ya Kristoforo Kolumbus nchi hizo zilikuwa makoloni ama ya Hispania ama ya Ureno hadi karne ya 19. Wakazi wengi ni watoto wa wahamiaji kutoka Ulaya Kusini au machotara waliotokana na wahamiaji hao na wakazi asilia.

Katika nchi kadhaa, hasa Meksiko na nchi za Andes, ambako Waindio wengi kidogo walibaki, wanaendelea kutumia lugha zao pamoja na Kihispania.

Dini kubwa katika Amerika ya Kilatini ni Ukristo wa Kanisa Katoliki lililokuwa kanisa rasmi ya Hispania na Ureno.