Yugoslavia

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Yugoslavia hadi 1991 katika Ulaya

Yugoslavia (Jugoslavija na Југославија kwa Kikyrili "Nchi ya Waslavoni ya Kusini") ilikuwa nchi katika Ulaya kusini mashariki kati ya 1918 na 2003.

Ufalme wa Waserbia, Wakroatia na Waslovenia[hariri | hariri chanzo]

Ilianzishwa kwa jina la "Ufalme wa Waserbia, Wakroatia na Waslovenia" mwaka 1918 baada ya kuporomoka kwa Austria-Hungaria. Ufalme huu uliunganisha nchi za awali za Serbia na Montenegro pamoja na sehemu za Dola la Austria zilizokaliwa na Waslavoni. Tangu 1929 ufalme ulibadilisha jina kuitwa "Ufalme wa Yugoslavia". Tangu mwanzo tatizo mojawapo la nchi ilikuwa uhusiano kati ya mataifa mawili makubwa ndani yale yaani Waserbia na Wakroatia. Ingawa yote mawili ni karibu sana kuna tofauti za historia, dini na utamaduni ziilizosababisha hofu ya kutawaliwa kwa upande mmoja na mwingine.

Vita Kuu ya Pili ya Dunia[hariri | hariri chanzo]

Wakati wa Vita Kuu ya Pili ya Dunia Yugoslavia ilivamiwa na jeshi la Ujerumani. Wapinzani mbalimbali walichukua silaha kupinga wavamizi. Kati ya vikundi hivi wanamgambo Wakomunisti chini ya Josip Broz Tito wakafaulu kuliko jeshi la msituni wa mfalme. Baada ya mwisho wa vita 1945 kundi la Tito lilichukua utawala.

Bendera ya Yugoslavia tangu 1946

Shirikisho la Jamhuri ya Watu wa Yugoslavia[hariri | hariri chanzo]

Faili:SFRYugoslaviaNumbered.png
Majimbo au jamhuri za Yugoslavia kabla ya 1991

Katiba mpya ya 1946 iliunda Yugoslavia upya kama shirikisho la kisoshalisti. Majimbo 6 zilizoitwa pia "jamhuri" ziliundwa pamoja na mikoa miwili ya kujitawala ndani ya Serbia:

  • 1. Jamhuri ya kisoshalisti ya Bosnia na Herzegovina (mji mkuu Sarajevo)
  • 2. Jamhuri ya kisoshalisti ya Kroatia (mji mkuu Zagreb)
  • 3. Jamhuri ya kisoshalisti ya Masedonia (mji mkuu Skopje)
  • 4. Jamhuri ya kisoshalisti ya Montenegro (mji mkuu Titograd (sasa Podgorica))
  • 5. Jamhuri ya kisoshalisti ya Serbia (mji mkuu Beograd) na ndani yake:
      • 5a. Mkoa wa kisoshalisti ya Kosovo (mji mkuu Priština)
      • 5b. Mkoa wa kisoshalisti ya Vojvodina (mji mkuu Novi Sad)
  • 6. Jamhuri ya kisoshalisti ya Slovenia (mji mkuu Ljubljana)

Tito aliamua kutotii tena amri na maagizo kutoka chama cha kikomunisti cha Umoja wa Kisovyeti. Yugoslavia ilifuata siasa ya kutoshikamana na pande zote mbili za vita baridi yaani Marekani na Urusi.

Baada ya kifo cha Tito umoja wa Yugoslavia ulidhoofika. Mashindano kati ya mataifa ndani ya nchi yaliongezeka.

Mwisho wa Yuguslavia[hariri | hariri chanzo]

1991 Kroatia, Slovenia na Masedonia zilichukua hatua ya kutoka nje ya shirikisho na kujitangaza kuwa nchi huru za pekee. 1992 jimbo la Bosnia na Herzegovina likafuata na kutoka nje.

Tangu 1992 "Yugoslavia" ilikuwa jina la umoja wa Serbia na Montenegro pekee. 2003 jina la Yugoslavia lilifutwa.

Mwaka 2006 hata umoja uliobaki kati ya Serbia na Montenegro ulifutwa na kila nchi imeendelea pekee yake.

Makala hii kuhusu mambo ya kihistoria bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Yugoslavia kama enzi zake au matokeo yake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.