Shaw Hassan

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Shaw Hassan
Show Hassan kazini
Show Hassan kazini
Maelezo ya awali
Jina la kuzaliwa Shaw Hassan Shaw
Amezaliwa 25 Septemba 1959 (1959-09-25) (umri 64)
Dar es Salaam, Tanzania
Aina ya muziki Muziki wa dansi
Kazi yake Mwanamuziki
Ala Kinanda, Gitaa
Miaka ya kazi Tangu miaka ya 1970-hadi sasa
Ame/Wameshirikiana na PAMA Band, Vijana Jazz Band, Orchestra Safari Sound, Kilimanjaro Connection Band


Shaw Hassan Shaw Rwamboh (alizaliwa 25 Septemba 1959) ni mpigaji kinanda na gitaa maarufu kutoka nchini Tanzania. Huenda akawa anajulikana zaidi kwa wapenzi wa Vijana Jazz wanakumbuka vile vipande vya kinanda vilivyokuwa vikianzisha zile nyimbo mbili alizokuwa akiimba Kida Waziri, Penzi Haligawanyiki na Shingo Feni, ile ni kazi ya Shaw Hassan Shaw Rwamboh.

Historia na kazi ya muziki[hariri | hariri chanzo]

Kutoka kulia: Hassan Shaw wa kwanza aliyenyoosha mkono. Anko John Kitime wa kwanza aliyesimama kushoto. Hapa wakiwa Stadium Morogoro.

Mwanamuziki huyu alizaliwa jijini Dar Es Salaam. Alianza kujifunza kupiga gitaa na wenzie kando ya Ziwa Tanganyika huko Kigoma, wakitumia magitaa ya tajiri mmoja aliyekuwa na meli ya uvuvi. Alipokuja Dar es Salaam akakutana na mwanamuziki Zahir Ally Zorro, Zahir ndiye aliyeboresha upigaji wake wa gitaa kiasi cha kukubaliwa na Patrick Balisidya kupiga gitaa la rythm katika bendi yake ya pili PAMA Band, chini ya Afro70.

Ni chini ya malezi ya Patrick alipojifunza kupiga Keybords (Kinanda). Baada ya hapo aliacha muziki na kujiunga na Dar Technical College. Lakini 1980 alijiunga na Vijana Jazz kama mpiga Keyboards, alishirikiana na wanamuziki wengi lakini wengi kwa mapenzi ya Mungu, wametangulia mbele ya haki. Baadhi ya waliobaki kati ya aliyokuwa nao wakati huo ni John Kitime, Kida Waziri, Saad Ally Mnara, Hamisi Mirambo, Huluka Uvuruge, Hassan Dalali, Hamza Kalala na Rashid Pembe.

Mwaka 1990 alijiunga na Orchestra Safari Sound, chini ya Maalim Muhidin Gurumo (MJOMBA), na Marehemu Abel Baltazar, hapa alikutana na wanamuziki kama Benno Villa Anthony na Mhina Panduka (Toto Tundu). Aliacha bendi baada ya miezi sita tu, mwenyewe anasema, ‘….kutokana na muhusika kutozingatia mkataba wangu…’. Alihamia Zanzibar na kujiunga na bendi iliyokuwa ikipiga Mawimbini Hotel, hakukaa sana kwani Washirika Tanzania Stars walimwita. Hapa akakutana na mwalimu wake wa gitaa Zahir Ally, Ally Choki, Musemba wa Minyugu, Tofi Mvambe, Abdul Salvador na wengine, ilitokea kutoelewana baina ya wanamuziki na yeye kama kiongozi wa bendi ilibidi aachie ngazi kuepusha bendi kuzidi kujichanganya.

Baada ya hapoKanku Kelly ambaye ni mume wa dada wa mke wake alimuita ajiunge na Kilimanjaro Connection Band. Anasema Kanku alimvumilia sana kwa kuwa alikuwa hajawahi kufanya kazi ya kukopi nyimbo za wanamuziki wengine wakubwa duniani, hatimaye akaweza kujiendeleza na kuweza kumudu kupiga vitu vikubwa, bendi hii ya Kanku ilikua inazunguka kwa kupiga muziki hotel mbalimbali katika nchi za Malaysia, Singapore, Indonesia, Thailand na Japan jambo ambalo lilifanya aone kila kitu ni kigeni kila alipokwenda.

Katika bendi hiyo alishirikiana na akina Kanku Kelly, Mafumu Bilal, Maneno Uvuruge, Burhan Adinan, Shomari Fabrice, Bob Sija, Fally Mbutu, Raysure Boy, Delphin Mununga na Kinguti System. Baadaye Shaw, Kinguti na Burhan Muba waliamua kuanzisha kundi dogo wakitumia Sequencer Keyboards na kumuaga Kanku Kelly. Group hili lilijiita Jambo Survivors Band, bendi ambayo itakumbukwa kwa ule wimbo Maprosoo ulioimbwa na Mlasi Feruzi ambao uliokuwa katika album ya MAPROSOO.

Tazama pia[hariri | hariri chanzo]

Viungo vya Nje[hariri | hariri chanzo]

Makala hii kuhusu mwanamuziki/wanamuziki fulani wa Tanzania bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Shaw Hassan kama wasifu wake, habari za maisha au kazi yake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.