Pedro Álvares Cabral

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Pedro Cabral.
Njia ya Cabral akielekea Uhindi kupitia Brazil.

Pedro Álvares Cabral (1467 au 1468 hivi - 1520 hivi) alikuwa mwanajeshi, baharia na mpelelezi kutoka nchini Ureno. Anakumbukwa kama Mzungu wa kwanza aliyefika Brazil (mnamo 22 Aprili 1500).

Mfalme Manuel I wa Ureno alimtuma Cabral kwenye safari kuelekea Uhindi. Cabral alisafiri mnamo 9 Machi 1500 na jahazi 13, akifuata njia ya mpelelezi Mreno aliyetangulia, Vasco da Gama. Akipita pwani ya Afrika katika Bahari Atlantiki, alitumia njia iliyompeleka upande wa magharibi. Mnamo tarehe 22 Aprili 1500 akakuta pwani ya nchi kavu aliyoamini mwanzoni ilikuwa kisiwa lakini aliona baadaye labda ni bara, akaitangaza kuwa mali ya Ureno kufuatana na Mkataba wa Tordesillas.

Cabral alikaa nchini Brazil kwa siku 10 kisha akaendelea na safari kwenda Uhindi. Wakati wa kuzunguka Afrika kwenye Rasi ya Tumaini Njema alipoteza jahazi kadhaa. Alipofika Uhindi pale Calicut alipigana na wafanyabiashara Waislamu, hatimaye alifaulu kununua viungo vya chakula huko Cochin mwanzoni mwa Januari 1501.

Cabral alirudi Ureno mnamo 23 Juni 1501, akiwa na meli 5 tu kati ya 13 za awali, zilizobeba mzigo mkubwa wa viungo na manukato.

Cabral alistaafu kwenye shamba lake huko Santarém, Ureno. Alifariki mnamo 1520 na alizikwa katika nyumba ya watawa huko Santarém, Ureno.

Marejeo[hariri | hariri chanzo]

Kujisomea[hariri | hariri chanzo]

  • Abramo, Alcione (1969). Grandes Personagens da Nossa História (kwa Kireno) 1. São Paulo: Abril Cultural. 
  • Alves Filho, João (1997). Nordeste: estratégias para o sucesso : propostas para o desenvolvimento do Nordeste brasileiro, baseadas em experiências nacionais e internacionais de sucesso (kwa Kireno). Rio de Janeiro: Mauad Consultoria e Planejamento Editorial. ISBN 978-85-85756-48-2. 
  • Barata, Mário (1991). O descobrimento de Cabral e a formação inicial do Brasil (kwa Kireno). Coimbra: Biblioteca Geral da Universidade de Coimbra.