Marikabu

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru

Kwa chombo cha maji angalia hapa merikebu

Marikabu
(Alfa Pegasi, Markab)
Kundinyota Farasi (Pegasus)
Mwangaza unaonekana 2.48
Kundi la spektra A0 IV [1]
Paralaksi (mas) 24.46 ± 0.19
Umbali (miakanuru) 133
Mwangaza halisi -0.6
Jotoridi usoni wa nyota (K) 9765
Majina mbadala Marchab, 54 Pegasi, HR 8781, BD +14°4926, HD 218045, SAO 108378, FK5 871, HIP 113963


Marikabu (lat. & ing. Markab pia α Alfa Pegasi, kifupi Alfa Peg, α Peg) ni kati ya nyota angavu katika kundinyota la Farasi (Pegasus).

Jina

Marikabu ilijulikana kwa mabaharia Waswahili tangu miaka mingi wakifuata njia yao baharini wakati wa usiku kwa msaada wa nyota. [2]. Walipokea jina hili kutoka kwa Waarabu wanaotumia neno مركب markab kwa maana ya « chombo cha safari », hasa chombo cha usafiri wa maji (linganisha merikebu katika Kiswahili cha kisasa[3]), lakini pia usafiri mwingine kama vile farasi, au tandiko la farasi [4]. Hata hivyo jina hili "markab" linataja nyota kadhaa; siku hizi Waarabu hutumia jina منكب الفرس mankib al-fars inayomaanisha "bega la farasi" . Hii inalingana pia na maelezo ya Ptolemaio katika Almagesti ambako anaeleza nyota hii iko "mgongoni kwenye bega la bawa" [5]; kwenye mwandiko wa Kiarabu irabu fupi mara nyingi haziandikwi. Inawezekana pia ya kwamba herufi za n na r zilikosolewa hivyo "mnkb" (bega) ilisomwa kwa kosa kuwa "mrkb" (chombo cha usafiri) na kuandikwa vile kwa herufi za Kilatini.

Kwa matumizi ya kimataifa Umoja wa Kimataifa wa Astronomia ulikubali jina la Kiarabu na kuorodhesha nyota hii kwa tahajia ya "Markab" [6].

Alfa Pegasi ni jina la Bayer; Alfa ni herufi ya kwanza katika alfabeti ya Kigiriki lakini Marikabu ni nyota angavu ya tatu katika kundi lake na hii ni mfano ya kwamba Bayer hakufuata mwangaza kamili wakati wa kuorodhesha nyota.

Tabia

  • Marikabu iko katika umbali wa miakanuru takriban 133 kutoka Jua letu. Mwangaza unaoonekana ni mag 2.48. Spektra yake inaonyesha kundi la A0 IV. Hii ni dalili ya kwamba ni nyota nusu jitu ya kundi la A iliyomaliza tayari hidrojeni kwenye kitovu chake na sasa imeshaondoka kwenye safu kuu ya nyota. Inabiringika haraka sana kwa kasi ya kilomita 125 kwa sekunde. Jotoridi kwenye uso wake ni karibu na nyuzi 10,000 oK na nyota imeshapanuka hadi kufikia nusukipenyo mara tano ya Jua.

Tanbihi

  1. vipimo kufuatana na Fitzpatrick; Massa (2005)
  2. ling. Knappert 1993
  3. Kufuatana na Kamusi ya Kiswahili-Kiingereza ya Madan (1903), "merikebu" ni matamshi ya Kiunguja ya "marikabu" ambayo ni jina kwa chombo cha maji
  4. Davis (1944) uk. 24 anaeleza: Markab, from Arabic « riding, or anything oin which one is carried », e.g. a horse, chariot, camel, litter, or ship »
  5. ὁ ἐπί τοῦ μεταφρένου καὶ τοῦ ὤμου τῆς πτέρυγος ho epi tou metafrenou kai tou oomou tes pterygos, Heiberg (1903), uk. 78
  6. Naming Stars, tovuti ya Umoja wa Kimataifa wa Astronomia (Ukia), iliangaliwa Novemba 2017

Viungo vya Nje

Marejeo

  • Allen, Richard Hinckley: Star-Names and their Meanings; kwa G. E. Stechert New York, Leipzig, London, Paris 1899, ukurasa 437 (online kwenye archive.org)
  • Fitzpatrick, E. L.; Massa, D. (March 2005), "Determining the Physical Properties of the B Stars. II. Calibration of Synthetic Photometry", The Astronomical Journal, 129 (3): 1642–1662 hapa
  • Knappert, Jan: The Swahili Names of Stars, Planets and Constellations; The Indian Ocean Review September 1993 Volume 6 No. 3 September 1993, kurasa 6-7, ISSN 1031-2331
  • J.L. Heiberg: Claudii Ptolemaei opera quae extant omnia Vol. I, Syntaxis Mathematica, Pars II libros VII-XIII continens; Leipzig, Teubner 1903 (Maandiko yote yaliyopo ya Klaudio Ptolemaio)