Kaligrafia

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Injili ya Lindisfarne, chanzo cha Injili ya Mathayo, "Liber generationis Iesu Christi filii David filii Abraham" (Kilatini kwa "Kitabu cha ukoo wa Yesu Kristo, mwana wa Daudi, mwana wa Ibrahimu." )
Basmala katika kaligrafia ya Kiarabu

Kaligrafia ni sanaa ya kuandika vizuri na kurembisha maandishi. Neno latokana na lugha ya Kigiriki (καλλιγραφία (kalligrafía) inayounganisha κάλλος (kállos, uzuri, urembo) na γράφειν (gráfein, kuandika)) kupitia Kiingereza calligraphy.

Asili ya kaligrafia iko katika kazi ya kunakili maandiko matakatifu kama vile Korani au Biblia au kutoa hati rasmi. Kabla ya kuanzishwa kwa uchapishaji vitabu vyote viliandikwa kwa mkono kwa kutumia kalamu au burashi.

Katika utamaduni ya Wakristo wa Ulaya waandishi walilenga kutumia herufi nzuri kwa matini kwa jumla waliponakili sehemu za Biblia zilizotumiwa kwa masomo katika makanisa au monasteri. Herufi za kwanza za milango au sehemu maalumu mara nyigi zilipambwa kwa namna ya pekee.[1] Njia nyingine ilikuwa kuongeza picha kando la maneno.

Katika utamaduni wa Uislamu kaligrafia ilipata nafasi ya pekee kwa mapambo ya muswada au majengo kama msikiti na madrasa. [2] Kufuatana na mafundisho ya walimu Waislamu wengi hairuhusiwi kuchora picha ya viumbe na hata kama kuna mifano mingi ya uchoraji picha katika utamaduni wa Kiislamu kwa jumla hautumiwi katika muswada ya kidini na kwenye majengo ya kidini. Badala yake wasanii wa Kiislamu walitumia ayat za Qurani, maneno ya basmala (=bismillah), takbir, majina ya Allah, Muhamad, makhalifa rashidun au maimamu ya Shi'a yanayoandikwa kwa uzuri na kuwa pambo la ukuta au muswada.

Utamaduni wa Asia ya Mashariki hasa China, Korea na Japani inaheshimu sana kaligrafia tangu zamani hadi leo. Maneno au sentensi ya wanafalsafa au ya kidini yanachorwa na kuwekwa kama mapambo katika mabustani nyumbani, kwenye mahekalu au majengo ya umma. Watoto hufundishwa sanaa hii nyumbani na pia shuleni. [3]


References[hariri | hariri chanzo]

  1. http://www.bibliotheca-laureshamensis-digital.de/de/bildergalerie/initialen/zierinitialen.html Mifano ya "initials" (Jer.)
  2. Blair, Sheila S.; Bloom, Jonathan M. (1995). The art and architecture of islam : 1250–1800 (Reprinted with corrections. ed.). New Haven: Yale University Press. ISBN 0-300-06465-9.
  3. Kuhusu kaligrafia ya China

Tazama pia[hariri | hariri chanzo]