Johannes Gutenberg

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Johannes Gutenberg
Biblia iliyochapwa na Gutenberg mwaka 1455 hivi.
Wachapishaji wa karne ya 16

Johannes Gensfleisch zur Laden zum Gutenberg, anayejulikana kifupi kama Johannes Gutenberg, (mnamo 1398 - 3 Februari 1468) alikuwa fundi dhahabu na mvumbuzi kutoka Ujerumani anayekumbukwa hasa kama mbuni wa uchapaji vitabu kwa herufi za kusogezeka.

Alitengeneza mashine ya kwanza ya kuchapa vitabu, alibuni aloi ya kufaa kwa herufi alizotumia katika mashine hii pamoja na wino.

Alitengeneza pia kifaa kilichomwezesha kusubu herufi za metali haraka.

Vitabu kabla ya Gutenberg[hariri | hariri chanzo]

Kabla ya Gutenberg vitabu vingi viliandikwa kwa mkono. Kunakili kitabu kimoja kama Biblia kwa mkono kulichukua angalau mwaka mmoja.

Teknolojia ya kuchapisha vitabu ilipatikana tayari lakini haikuridhisha. Kwa kawaida ukurasa wote ulichorwa halafu kukatwa katika ubao. Ubao ulipakwa wino na karatasi zilisukumwa kwenye ubao huu. Shida zilikuwa: kwanza kazi kubwa ya kutengeneza bao, halafu bao hizi hazikudumu sana.

Teknolojia mpya[hariri | hariri chanzo]

Mbinu ya Gutenberg ilikuwa hasa kutumia herufi metalia za kusogezeka.

Metali inadumu kuliko ubao ikamwezesha Gutenberg kuandaa ukurasa na kuuchapisha mara maelfu. Aliweka maandishi kwa kuandaa herufi metalia nyingi alizounganisha kuwa maneno, mistari hadi ukurasa wote.

Ukurasa ulibanwa pamoja ukawa tayari kwa uchapishaji. Kama makosa yalionekana au mabadiliko yalihitajika aliweza kufungua ukurasa, kuongeza au kutoa herufi na kubana ukurasa upya.

Alitengeneza herufi kwa kumwaga aloi ya plumbi (metali ya risasi), stani na antimoni katika kalibu ilipopoa. Kwa njia hii aliweza kusubu herufi nyingi zilizokuwa sawa kabisa, tofauti na herufi zilizokatwa kwa mkono katika ubao.

Baada ya kupanga herufi na kuzibana aliweza kuchapisha ukurasa mara nyingi jinsi ilivyohitajika. Aliweza pia kufungua mbano wa ukurasa na kutumia herufi kwa kazi nyingine au kutunza ukurasa kwa marudio yaliyotarajiwa.

Pamoja na hayo alibuni mgandamizo uliokuwa mashine bora ya kuchapa vitabu.

Biblia ya Gutenberg[hariri | hariri chanzo]

Kazi ya kwanza ya Gutenberg ilikuwa Biblia (1455 hivi). Imesifiwa kama kazi bora kifundi na kisanii.

Matokeo ya kazi ya Gutenberg[hariri | hariri chanzo]

Uvumbuzi huo wote ulianzisha mapinduzi ya teknolojia na utamaduni. Vitabu vilianza kupatikana haraka kuliko awali. Bei ya vitabu ilishuka. Baada ya kuongezeka kwa vitabu, watu wengi zaidi walianza kusoma. Shule zilienea kushinda zamani.

Teknolojia ya Gutenberg iliwezesha uenezi wa harakati ya matengenezo ya kiprotestanti iliyoanzishwa na Martin Luther mwaka 1517. Maandiko ya Luther yalisambaa haraka kote Ulaya. Maandiko ya wafuasi na wapinzani wake yalifuata. Watu wengi walishiriki na kufuatilia habari hizi.

Gutenberg amehesabiwa kati ya watu 100 wa historia ya dunia wenye athira kubwa. Gazeti la Newsweek alimteua kama "Mtu wa milenia 1000-2000".

Tanbihi[hariri | hariri chanzo]

Vyanzo[hariri | hariri chanzo]

Marejeo[hariri | hariri chanzo]

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]

Wikimedia Commons ina media kuhusu: