Kulungu pembe-nne

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Kulungu pembe-nne
Kulungu pembe-nne wa kiume (Tetracerus quadricornis)
Kulungu pembe-nne wa kiume
(Tetracerus quadricornis)
Uainishaji wa kisayansi
Himaya: Animalia (Wanyama)
Faila: Chordata (Wanyama wenye ugwe wa neva mgongoni)
Ngeli: Mamalia (Wanyama wenye viwele wanaonyonyesha wadogo wao)
Oda: Artiodactyla (Wanyama wenye vidole viwili au vinne mguuni)
Nusuoda: Ruminantia (Wanyama wanaocheua)
Familia: Bovidae (Wanyama walio na mnasaba na ng'ombe)
J. E. Gray, 1821
Nusufamilia: Bovinae (Wanyama wanaofanana na ng'ombe)
Jenasi: Tetracerus (Wanyama kama kulungu pembe-nne)
Leach, 1825
Spishi: T. quadricornis
(de Blainville, 1816)
Ngazi za chini

Nususpishi 3:

  • T. q. quadricornis (de Blainville, 1816)
  • T. q. iodes Hodgson, 1847
  • T. q. subquadricornis (Elliot, 1839)
Msambao wa kulungu pembe-nne
Msambao wa kulungu pembe-nne

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru

Kulungu pembe-nne ni mnyama mdogo wa spishi Tetracerus quadricornis katika familia Bovidae, anayefanana na kulungu na kuishi msituni wazi kwa Uhindi na Nepal. Huyo ndiye mnyama pekee katika jenasi Tetracerus. Akiwa na kimo cha sm 55–64 tu mabegani, huyo ni mnyama mdogo kabisa katika familia Bovidae huko Asia (suni wa Afrika ni wadogo zaidi). Madume wa spishi hiyo ndio wa pekee miongoni mwa mamalia wote kwa kuwa wana pembe nne za kudumu.

Maelezo[hariri | hariri chanzo]

Kulungu pembe-nne wa kike

Kulungu pembe-nne ni miongoni mwa wanyama wadogo zaidi wa familia bovidae wa Asia, akiwa na kimo cha sm 55–64 tu mabegani, na uzito wa kilo 17–22. Ana umbo dogo wenye miguu myembamba na mkia mfupi. Manyoya yake ni kahawia au kahawianyekundu, yakibadili kuwa meupe katika sehemu za ndani za miguu. Mchirizi mweusi wa nywele upo nje ya kila mguu, na ana maeneo meusi puani na sehemu za nyuma za masikio. Majike wana matiti manne, yaliyopo nyuma katika fumbatio.[1]

Kipengele cha mnyama huyo kisicho cha kawaida ni kuwepo kwa pembe nne; kipengele cha pekee miongoni mwa wanyama hai. Madume tu wana pembe, kwa kawaida wakiwa na pembe mbili kati ya masikio na mbili zaidi mbele yao pajini. Pembe za kwanza hutokea alipo na umri wa miezi michache tu, na za pili hutokea baada ya miezi 10 au 14. Pembe hizo haziambuliwi kamwe, ingawa labda zitadhuriwa wakati wa kupigana. Madume wazima wengine hawana pembe; hasa kwa nususpishi T. q. subquadricornis jozi ya pembe za mbele hazipo, au zipo kama nundu ndogo bila nywele. Jozi ya pembe za nyuma hufika urefu wa sm 7–10, huku jozi ya mbele ni kwa kawaida ndogo zaidi, sm 2–5 tu.[1]

Msambao na makazi[hariri | hariri chanzo]

Kulungu pembe-nne wengi sana wa pori wapo Uhindi, na makundi ya wanyama wachache yapo Nepal. Msambazo wao huenea kusini ya tambarare ya Gangetic mpaka jimbo la Tamil Nadu, na mashariki mpaka Odisha. Wapo pia katika Hifadhi ya Taifa ya Msitu wa Gir, ya Uhindi ya magharibi.[2][1]

Kulungu pembe-nne huishi katika makazi mbalimbali mahali kokote ndani ya usambazaji wao, lakini hupendelea misitu wazi,[3][4] mikavu, na ya kupukutika majani milimani. Kulungu pembe-nne hubaki katika maeneo yenye uoto mwingi wa manyasi marefu au vichaka vizito, na karibu na maji. Wao hukaa mbali na maeneo ya binadamu.[1] Wanyama wawawindao kulungu pembe-nne ni pamoja na chui milia,[5] chui, na dhole (mbwa pori wa Uhindi).[6]

Mwenendo[hariri | hariri chanzo]

Kulungu pembe-nne kwa kawaida ni wanyama wa upweke, ingawa mara chache wako katika makundi ya hadi wanne. Wao hupendelea kukaakaa, badala ya kuhamahama, na mara nyingi wakinga eneo lao kuwatimua wanyama wengine. Madume huweza kuwa wagomvi kwa madume wengine wakati wa misimu ya kupandisha. Wanyama wazima hufanya mlio wa kugutusha ulio na sauti kama "froank", na sauti tulivu zaidi nyingine kuwasiliana na watoto au wazima wengine. Wao huwasiliana pia kutumia harufu, wakiacha chungu za kinyesi katika eneo lao na kutia alama uoto kwa kutumia tezi za harufu zilizopo mbele ya macho yao.[1] Kulungu pembe-nne hula majani laini, matunda na maua.

Uzazi[hariri | hariri chanzo]

Kichawa cha kulungu pembe-nne

Msimu wa kupandisha hudumu toka Mai mpaka Julai, na madume na majike kwa kawaida hubaki mbali kwa salio la mwaka. Mwenendo wao wa ubembe ni kuwa dume na jike kupiga magoti na kusukumana huku shingo zao kufungamana, yakifuatwa na dume kutamba. Kipindi cha kubeba mimba ni takribani miezi minane, halafu ndama mmoja au wawili huzaliwa. Wakati wa kuzaliwa, ndama wana urefu wa sm 42–46, na uzito wa kilo 0.74–1.1. Ndama hubaki pamoja na mama wao kwa mwaka moja, na huweza kuzaa wakiwa na umri wa miaka miwili.[1]

Hifadhi[hariri | hariri chanzo]

Kwa sababu anaishi katika sehemu ya dunia yenye idadi kubwa ya watu, kulungu pembe-nne anawekwa hatarini na upungufu wa makazi yake unaosababishwa na haja ya ardhi ya ukulima. Pia, fuvu lake la kichwa lisilo la kawaida limetamaniwa na wawindaji. Idadi ya wanyama hao hai porini ni takribani 10,000, ingawa wengi wengine wanalindwa katika maeneo ya hifadhi.

Hali ya sasa[hariri | hariri chanzo]

Kulungu pembe-nne wameainishwa na IUCN kama spishi inayoweza kudhuriwa, kwa sababu maangamizi ya makazi.[2]

Marejeo[hariri | hariri chanzo]

  1. 1.0 1.1 1.2 1.3 1.4 1.5 Leslie, D.M. & Sharma K. (2009). "Tetracerus quadricornis (Artiodactyla: Bovidae)". Mammalian Species 843: 1–11. doi:10.1644/843.1. 
  2. 2.0 2.1 IUCN Red List (2014).
  3. Krishna, C.Y, Krishnaswamy, J & Kumar, N.S. (2008). "Habitat factors affecting site occupancy and relative abundance of four horned antelope". Journal of Zoology 276 (1): 63–70. doi:10.1111/j.1469-7998.2008.00470.x. 
  4. Krishna, C.Y, Clyne, P, Krishnaswamy, J & Kumar, N.S. (2009). "Distributional and ecological review of the four horned antelope Tetracerus quadricornis". Mammalia 73 (1): 1–6. doi:10.1515/MAMM.2009.003. 
  5. Biswas, S. & Sankar, K. (2002). "Prey abundance and food habit of tigers (Panthera tigris tigris) in Pench National Park, Madhya Pradesh, India". Journal of Zoology 256 (3): 411–420. doi:10.1017/S0952836902000456. 
  6. Karanth, K.U. & Sunquist, M.E. (1992). "Population structure, density and biomass of large herbivores in the tropical forests of Nagarhole, India". Journal of Tropical Ecology 8 (1): 21–35. doi:10.1017/S0266467400006040. 
Wikimedia Commons ina media kuhusu:

Ili kupata maelezo kuhusu masanduku ya uanapwa ya spishi angalia: Wikipedia:WikiProject Mammals/Article templates/doc.