Mwarobaini

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Mwarobaini (Neem)
(Azadirachta indica)
Mwarobaini
Mwarobaini
Uainishaji wa kisayansi
Himaya: Plantae (Mimea)
(bila tabaka): Angiospermae (Mimea inayotoa maua)
(bila tabaka): Eudicots (Mimea ambayo mche yake una majani mawili)
(bila tabaka): Rosids (Mimea kama mwaridi)
Oda: Sapindales (Mimea kama mmoyomoyo)
Familia: Meliaceae (Mimea iliyo na mnasaba na mwarobaini nusu)
Jenasi: Azadirachta
Spishi: A. indica
A.Juss.

Mwarobaini (Azadirachta indica) ni mti unaofahamika kwa uwezo wake wa kutibu magonjwa ya aina mbalimbali. Inaaminika kuwa mti huu umetoka huko India na Burma. Mwarobaini hushamiri zaidi katika nchi za tropiki na una uwezo mkubwa wa kuhimili ukame.

Jina “mwarobaini” linatokana na imani kuwa mti huu una uwezo wa kutibu magonjwa yapatayo arobaini. Majani na mbegu ya mwarobaini imekuwa ikitumiwa kama tiba kwa miaka maelfu huko nchini India na hivi sasa inatumiwa katika sehemu mbalimbali duniani likiwemo bara la Afrika.

Wanasayansi wa nchi za Magharibi hutumia pia mti huu kwenye tiba na utafiti. Mwanzoni mwa mwaka 2005, serikali ya India ilipeleka kesi mahakamani kupinga hatua ya mamlaka ya leseni ya Ulaya (European Patent Office) kutoa leseni kwa Wizara ya Kilimo ya Marekani na kampuni ya kimataifa ya WR Grace kumiliki haki ya kutengeneza na kuuza dawa ya ukungu inayotokana na mwarobaini.

Kati ya magonjwa ambayo mti huu umetumika kutibu au kupoza ni matatizo ya kusaga chakula tumboni, kisukari, kansa, magonjwa ya ngozi, malaria, ukungu (fungus), n.k. Matawi yake hutumiwa kama mswaki na magome yake hutumiwa kama dawa ya kusafisha meno.

Mafuta ya mbegu ya mwarobaini hutumika kutengenezea vipodozi na sabuni. Kiziduo cha mbegu au mafuta yake hutumiwa kama dawa ya kuulia wadudu wanaoharibu mimea shambani.

Picha[hariri | hariri chanzo]

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]