Dignitatis Humanae

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru

"Dignitatis Humanae" ni jina la Kilatini la hati iliyotolewa na Papa Paulo VI na washiriki wengine wa Mtaguso wa pili wa Vatikano (kwa kura 2308 dhidi ya 70) tarehe 7 Desemba 1965 kuhusu uhuru wa dini. Tafsiri ya jina hilo ni "Hadhi ya Binadamu".

Tamko hilo la mwisho la mtaguso mkuu huo lilisababisha mijadala mikali wakati wa mtaguso na baada yake hata likachangia kwa kiasi kikubwa farakano la askofu Marcel Lefebvre.

Sababu ni kwamba linasisitiza haki ya binadamu ya kufuata ukweli wa kidini kadiri alivyoujua, wakati mafundisho ya zamani ya Kanisa Katoliki yalikuwa yakisisitiza kuwa imani ya Kikristo ni ya lazima kwa wokovu.

Lakini masisitizo hayo hayapingani, kwa maana ni wajibu wa kila mtu kuutafuta ukweli na kuufuata, ila Wakristo hawawezi kumlazimisha asiyejaliwa bado imani au mwanga wa kutosha, bali wanapaswa kuendelea kumtangaza Yesu kwa wokovu wa watu.

Kinyume cha baadhi ya matendo ya Wakristo wa zamani, Kanisa linaamini kwamba Ukristo unapaswa kuenea kwa nguvu ya ukweli wake, sio kwa upanga, kwa kuwa Mungu mwenyewe anamheshimu binadamu na hiari yake.

Mfano bora ni ule wa Yesu Kristo na wa mitume wake.

Basi, kila mtu na kila serikali waheshimu uhuru wa kufuata dini yoyote. Haki hiyo inahusu mtu binafsi na makundi pia.

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]