Buibui (Arithropodi)

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Buibui
Jike la buibui uzi-dhahabu katika utando
Jike la buibui uzi-dhahabu katika utando
Uainishaji wa kisayansi
Himaya: Animalia
Faila: Arthropoda
Nusufaila: Chelicerata
Ngeli: Arachnida
Oda: Araneae
Ngazi za chini

Nusuoda 2:

Buibui au bui (buibui wakubwa) ni arithropodi wa oda Araneae katika ngeli Arachnida. Kama arakinida wote wana miguu minane na pia wanaweza kusokota nyuzi za aina ya hariri (hariri ya buibui). Kinyume na arithropodi wengine kiwiliwili chao kina sehemu mbili tu: kefalotoraksi (cephalothorax: kichwa na kidari) na fumbatio zilizoungwa kwa pediseli (pedicel) nyembamba kwa umbo wa mrija. Kefalotoraksi inabeba miguu na kando ya mdomo kuna jozi ya viungo vikubwa vinavyoitwa kelisera (chelicerae) na jozi nyingine ya viungo vidogo vinavyoitwa pedipalpi. Kelisera zina viungo viwili na kile cha mbele kina aina ya chonge kali inayotumika kwa kuingiza sumu katika windo. Isipotumika chonge hii imekunjwa kwenye upande wa ndani wa kelisera. Pedipalpi ni kama sehemu za mdomo na hutumika kwa kushika na kuminya windo. Madume hutumia pedipalpi kwa kuweka shahawa katika ufunguzi wa uzazi wa jike.

Buibui wanaojulikana sana hutengeneza utando ili kukamata arithropodi wengine, wadudu hasa, lakini hata wanyama wadogo (bui). Buibui wengine huwinda wakikimbia au kuruka. Bui wakubwa sana huitwa bui-nyani (spishi za dunia ya kale) na tarantula (spishi za dunia mpya) na wanaweza kukamata mijusi, nyoka wadogo, vipanya na ndege.

Picha[hariri | hariri chanzo]