Nanyindwa

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru

Nanyindwa ni kijiji ambacho kipo kilomita kama kumi na nane hivi kutoka Masasi mjini ukielekea kusini, kaskazini mwa mkoa wa Mtwara, Tanzania.

Katika kijiji hiki kuna mitaa miwili, Kilimani na Zaire na kimepakana na vijiji vya Lilala, Nangose, na Nraushi.

Wenyeji wake ni Wamakua japokuwa siku hizi kuna Wamakonde wachache. Wenyeji wa kijiji hiki walikuwa na mamwenye (machifu), Namunlia, Mwenye Nakavina na Mwenye Namkuvia (Albano Maita huyu yupo hadi leo).

Wanakijiji ni wakulima wa mahindi, mtama, ufuta na mihogo. Zao la biashara ni ufuta na korosho.

Baadhi ya wanakijiji hula panya au samaki mchanga 'Toro'.

Umaarufu wa kijiji hiki unatokana na kuwa na kanisa la kwanza la Anglikana ambalo lilijengwa mwaka 1912. Kasisi wa kwanza mzalendo alikuwa akiitwa Padri Enrico Akuchigombo ambaye alifariki mwaka 1969 katika wilaya ya Tunduru mkoa wa Ruvuma.

Mwaka 2012 mabaki yake yalirejeshwa Nanyindwa na kuzikwa upya kando kidogo na kanisa hilo kongwe ambalo hata hivyo mwaka huo lilikarabatiwa na Chifu Mkuvia Maita ambaye ni mzaliwa na mkazi wa kijiji hicho; awali alikuwa akifanya kazi Ofisi ya Rais lakini alipostaafu akawa mchimbaji wa madini.

Kanisa hilo lilifanyiwa ibada ya kutabaruku na Askofu Mkuu wa Anglikana Tanzania, Dk Valentone Mokiwa 14 Septemba 2012 ambapo maaskofu wanne walihudhuria. Tarehe hiyo kanisa hilo lilikuwa likitimiza miaka 100 na sherehe kubwa hiyo ilichangiwa na watu mbalimbali akiwemo Cate Kamba ambaye ni kmwenyekiti wa CCM wa mkoa wa Dar es Salaam na wazazi wake chimbuko lake ni kijiji hicho.,

Kijiji hiki kina shule ya msingi na zahanati. Shule hiyo iliwahi kutoa watu maarufu kama vile aliyewahi kuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya kilimo, C.Y. Mpupua, daktari wa kwanza mweusi wilaya ya Nachingwea, Mzee faraja Mpupua au mzee Makiko.

Kijiji hiki ni maarufu kwa kutoa walimu wengi sana ambao walifundisha sehemu mbalimbali za wilaya ya Masasi na kwingineko, kama Carlo Mpupua, Richard Kandaya, Richard Kamenya, Jacob Chitukoro aliyewahi kuwa msaidizi wa Katibu Mkuu wa CCM, Rashid Kawawa, Julius Savava, Luca Munlia, Walace Chitukuro, Brigita Francis Hokororo, Owen Lami na Charles Lami ambao walikuwa mapacha wakaacha kufundisha na kushangaza wengi, Mwalimu Pepetua, Mwl Kambulaje, Stephano Jumbe, Francis Nchihiya, Stefano Limbende na wengine wengi.

Kijiji kimewahi kutoa waandishi wa habari mahiri wawili, Elvan Stambuli na Gabriel Kandaya na mtangazaji maarufu wa Radio Tanzania, George Mpupua pia alikuwa mwanamuziki akiimbia bendi za Mwenge Jazz (Paselepa), Uda Jazz, Matimila n.k.

Lakini pia kijiji hiki kilitoa mapadre wengi kama vile Padri Msamati, Padri Carlo Marcus na kadhalika na mashemasi kama vile shemasi George Rashid, lakini pia mchungaji Noel Alban Stambuli wa Kanisa la Methodisti lenye asili ya Korea Kusini.

Kijiji kina mabomba ya maji ambayo yaliwahi kutoa maji lakini sasa hakuna mashine ya kusukuma maji na siku hizi kina umeme.

Historia ya Wamakua wa Nanyindwa[hariri | hariri chanzo]

Wamakua wa Nanyindwa ndio waanzilishi wa Kijiji cha Nanyindwa wilayani Masasi, kijiji kipo mkoa wa Mtwara. Wamakua hawa kihistoria walitokea Msumbiji sehemu za Mueda zaidi ya miaka 180 iliyopita.

Walipoingia nchini kwa kuwakimbia Wareno, waligawanyika, wapo walioamua kuishi Mumbaka chini ya Mwenye Nakavina na wengine wakaja Nanyindwa chinya Mwenye Namkuvia na baadaye Mwenye Namunlhia.

Namwiilha Wootelha ndiye aliyehamia Nanyindwa naye akawazaa Nachukulha na Navillhellha.

Navillhela akamzaa Achipire, Yohana, Amica na Aluse aliyeolewa na Mwalimu Richard Kamenya ambaye aliwazaa Heriety Alukanda Apugwile (hakuzaa), Mariam Kamenya Maita (Naakoko), Docas (Biti Maneno au Mama Nchiha), Maiko Kamenya, Merry Kamenya Stambuli, na mama Lilian Richard Mbunda wa Ndanda, kizazi cha sasa.

Mariam Naakoko Kamenya Maita alimzaa Mwalimu Daudi Maita, Albano Maita (mzee Mkuvia ambaye ni chifu au mwenye wa sasa), Agnesi Maita, Agatha Maita, Anna Maita, Biti Maita (Mama Nyau), hiki ni kizazi cha sasa, baba yao alikuwa ni Mwalimu Maita.

Merry Kamenya Stambuli amewazaa Edgar, Violet, Merry, Elvan (mwandishi wa historia hii) , Bernadeta, Susana, Noel, Moses, Elia na Judith Stambuli na baba yao ni mzee Christopher Stambuli aliyekuwa afisa Ofisi ya Rais Ikulu Dar, hiki ni kizazi ambacho kipo sasa.

Mama Lilian Mbunda wa Ndanda aliwazaa Mariam, Lucy, Jerald, na watoto wawili ambao majina yao sijayakumbuka. Maisha yao ni Ndanda.

Nachukullha akamazaa Nahatani (mkubwa) na Namwiilha. Nahatani akamzaa Biti Pesi, Biti Pawillha, Mama Chilimba (mama yake Cprian Chilimba au Mpokwa). Namwilha, Patrick Hamisi baba yake Cate Kamba, Nachokorokwa ambaye alimzaa Nahatan (mdogo), Mwalimu Carlos Mpupua (Baba yake Joji Mpupua na marehemu Yuda Mpupua aliyewaki kuwa katibu mkuu wa wizara ya kilimo), Simon Mpupua (Makiko, aliyekuwa daktari Nachingwea), Mariam Rashid Mpupua (mama Ndiinda), Sara, Batholomeo, Beatrice na Angela (biti Fundi aliyefariki mwaka huu 2020 akiwa na miaka 103). Joji Mpupua yupo hadi leo kijijini Nanyindwa.

Mzee Simon Faraja 'Makiko' aliwazaa Faraja, Kweigy na ndugu zao, kizazi cha sasa.

Namwillha alimzaa Akuchigombo, Albart Munlia, Wiliam Munlia, Joji Munlia na ndugu zao, Albat akamzaa mama Scola aliyeolewa na Mwalimu Richard Kandaya ambaye alimzaa Gabriel Kandaya na nduguze skola. James, Mwal Kandaya, nk.

Mbele ya Nanyindwa kuna kijiji cha Lilala, kaskazini mashariki kuna kijiji cha Mraushi, kaskazini kuna kijiji cha Maendeleo na mashariki kuna kijiji cha Nangose, kipo jirani na Masasi. Kusini kimepakana na kijiji cha Nambaya au Chikoweti.

Makala hii kuhusu maeneo ya Mkoa wa Mtwara bado ni mbegu.
Je unajua kitu kuhusu Nanyindwa kama historia yake, biashara, taasisi zilizopo, watu au utamaduni?
Labda unaona habari katika wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.
Tafadhali usiingize majina ya maafisa au viongozi wa sasa maana wanabadilika mno.