Mlangobahari wa Taiwan

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
(Elekezwa kutoka Taiwan Strait)
Ramani ya Mlangobahari wa Taiwan
Taiwan Strait

Mlangobahari wa Taiwan (kwa Kiingereza: Taiwan Strait au Formosa Strait) ni sehemu ya bahari iliyopo kati ya China bara na kisiwa cha Taiwan. Huu ni mlangobahari unaounganisha Bahari ya Mashariki ya China na Bahari ya Kusini ya China. Upana wake ni kilomita 180, sehemu nyembamba kabisa km 131.

Ni njia ya bahari inayotumiwa na meli nyingi sana zinazobeba kontena baina ya bandari za China bara.

Tangu ushindi wa ukomunisti katika China bara kwenye mwaka 1949 mlangobahari huo uliona mapambano kadhaa ya kijeshi. Jeshi la Kuomintang chini ya rais Chiang Kai-shek liliweza kujiokoa mbele ya Wakomunisti chini ya Mao Zedong wakivuka bahari wakafaulu kujitetea pale Taiwan na pia kwenye visiwa vidogo karibu na pwani ya bara. Jeshi la ukombozi la watu wa China lilipiga mizinga visiwa vya karibu kama Qemoy kwa miaka mingi. Kwa jumla manowari za Marekani zilizuia mashambulio ya jeshi la bara kufika Taiwan. Mwaka 1965 kulikuwa na mapigano kadhaa baina ya manowari za pande zote mbili katika eneo la mlangobahari.

Baada ya Jamhuri ya Watu wa China kupokewa mwaka 1972 katika Umoja wa Mataifa mashambulio katika mlangobahari yamekwisha. Baada ya kifo cha Mao na siasa mpya chini ya Deng Xiaoping biashara imeweza kuanza baina ya pande hizo mbili za China, mwanzoni kwa umbo la magendo na baadaye pia kwa njia halali.

Leo hii watalii na wafanyabiashara kutoka pande zote mbili za mlangobahari wanavuka na kutembelea upande mwingine bila shida.

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]

Wikimedia Commons ina media kuhusu: