Solomoni

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
(Elekezwa kutoka Suleimani)
Solomoni na malkia wa Saba (mchoro wa Konrad Witz, alias Conradus Sapientis, 1434-1435).

Mfalme Solomoni kadiri ya Biblia alikuwa mfalme wa tatu na wa mwisho wa Israeli nzima, akitawala kuanzia 970 KK hadi 930 KK hivi.

Maisha yake[hariri | hariri chanzo]

Solomoni katika ikulu yake (kadiri ya Ingobertus, 880 hivi).

Alikuwa mwana wa Daudi na Bath-Sheba (Betsheba), aliyewahi kuwa mke wa Uria Mhiti.

Daudi alimchagua kuwa mrithi wake kwa sababu alikuwa uthibitisho hai wa msamaha aliopewa na Mungu kwa kuzini na hatimaye kumuua Uria.

Ufalme wake ulitazamwa na Wayahudi kuwa na ustawi usio na mfano, kutokana na hekima yake na amani iliyopatikana wakati wote wa utawala wake.

Ufalme wake uliweza kustawi kuliko ule wa baba yake kutokana na msingi imara aliouweka Daudi. Lakini mwenyewe aliudhoofisha na kusababisha mara baada ya kifo chake utokee utengano kati ya makabila ya Kaskazini na yale ya Kusini.

Kati ya kazi muhimu alizozifanya, mojawapo ni kujenga hekalu la Yerusalemu na kuliweka wakfu kwa sherehe kubwa ya siku saba, ambapo Mungu alionyesha kibali chake kwa kulijaza kwa sura ya wingu (1Fal 8). Polepole hekalu hilo likaja kuwa la pekee hata patakatifu pengine pote pakakatazwa chini ya mfalme Yosia.

Ingawa Solomoni anasifiwa kwa hekima yake, alishindwa kukwepa majivuno na tamaa, akataka kuwapendeza wake zake waliokuwa 700 (mbali na masuria 300), wengi wao Wapagani, hata akawajengea mahali pa kuabudia miungu yao akamchukiza Mungu hata akamtabiria mtoto wake atanyang’anywa sehemu kubwa ya ufalme (1Fal 11:1-13) ikawa hivyo.

Hata hivyo mwishoni aliweza kulaumiwa kwa kuzidisha fahari, hasa upande wa wanawake waliomvuta kwenda kinyume cha imani ya Mungu pekee.

Sala zake[hariri | hariri chanzo]

"Nipe mimi mtumwa wako moyo wa adili niwahukumu watu wako, na kupambanua mema na mabaya; maana ni nani awezaye kuwahukumu hawa watu wako walio wengi"? (1Fal 3:9)

"Ee Bwana, Mungu wa Israeli, hakuna Mungu kama wewe, mbinguni juu wala duniani chini! Ushikaye maagano na rehema kwa watumishi wako, waendao mbele zako kwa mioyo yao yote". (1Fal 8:23)

Baada ya kifo chake[hariri | hariri chanzo]

Kwa sababu hiyo, ufalme ulivunjika pande mbili mara baada ya kifo chake.

Hata hivyo, Wayahudi waliendelea kumuona kama kielelezo cha hekima, wakaandika vitabu kwa kutumia jina lake au kwa kujifananisha naye.

Yesu alijitangaza kuwa mkuu na mwenye hekima kuliko Solomoni.

Marejeo[hariri | hariri chanzo]

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]

Wikimedia Commons ina media kuhusu: