NSDAP

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Nembo la NSDAP kwneye bendera rasmi ya Dola la Ujerumani (1933/1934 – 1945)

NSDAP ni kifupi cha Nationalsozialistische Deutsche Arbeiterpartei (Chama cha Kizalendo - Kisoshalisti cha Wafanyakazi Wajerumani) kilichotawala Ujerumani kuanzia 30 Januari 1933 hadi 8 Mei 1945 wakati wa udikteta wa kiongozi wake Adolf Hitler. Chama chenyewe kilitumia pia kifupi cha "NS" kwa harakati yake na vitengo vyake.

Chama hiki kinachojulikana pia kama Chama cha Nazi (tamka: natsi) kilianzishwa mjini München (Munich) 1919 kwa jina la Deutsche Arbeiterpartei (Chama cha Wafanyakazi Wajerumani) (DAP). Jina likabadilishwa 1920 kuwa NSDAP. Sababu za kuanzishwa kwa chama zilikuwa mipango ya matajiri wenye mwelekeo wa kizalendo waliotaka kujenga harakati dhidi ya vyama vya kijamaa vyenye wafuasi wengi kati ya wafanyakazi. Walitegemea ya kwamba chama kinachoitwa cha wafanyakazi na cha kizalendo kitapunguza athira ya Wajamaa na Wakomunisti kati ya wafanyakazi.

Hadi mwaka 1923 chama kilikua katika jimbo la Bavaria lakini hakikuwa na athira kubwa nje ha hapa.

Hitler kama kiongozi wa NSDAP

Adolf Hitler alijiunga na DAP mwaka 1919 kwa amri ya wakubwa wake jeshini. Wakati ule Hitler alikuwa bado mwanajeshi na wakubwa wake walitafuta habari juu ya vyama vingi vipya vilivyoundwa Munich baada ya mwisho wa Vita Kuu ya Kwanza ya Dunia. Alionekana mara moja kama msemaji bora mwenye uwezo wa kuwahotubia wasikilizaji wake. Hotuba zake ziliwavuta watu wengi na chama kikamtegemea. 1921 Hitler alikuwa mwenyekiti wa chama.

Tangazo la Hitlerjugend (Vijana kwa Hitler) lamwonyesha kijana katika sare na Hitler nyuma yake;
Maneno yasema: Vijana wamhudumia Kiongozi; wote kuanzia umri wa miaka kumi wajiunge katika Hitlerjugend!

1923 NSDAP ilishiriki katika jaribio la mapinduzi ya München lililoshindikana. Chama kikapigwa marufuku na mwenyekiti Hitler akafungwa jela.

Shabaha na itikadi

Itikadi ya NSDAP ilikuwa mchanganyiko wa shabaha mbalimbali. Kwa jumla zilikusanywa chini ya kichwa cha "uzalendo". Hii ililenga dhidi ya maadui watatu:

  • Mkataba wa Versailles ulioweka masharti makali dhidi ya Ujerumani baada ya Vita Kuu ya Kwanza ya Dunia. NSDAP pamoja na vikundi vingine vya kizalendo ilipinga masharti haya pamoja na malipo ya fidia kwa gharama za vita, kundolewa kwa koloni za Ujerumani, kubanwa kwa jeshi kutozidi askari 100,000 na kutengwa kwa maeneo yaliyowahi kuwa sehemu ya nchi hadi 1919.
  • Harakati ya kisohalisti au kijamaa ya kimataifa iliyotazamiwa kama tishio kwa taifa na utamaduni wa Ujerumani
  • Ubebari wa kimataifa iliyotazamiwa ilitaka kukandamiza taifa la Ujerumani.

Itikati ya ubaguzi wa kimbari

Haya yote yaliunganishwa na itikadi ya kimbari iliyofundisha kuwa watu hutofautiana kutokana na "damu" na kila mbari au rangi ya watu ina uwezo na thamani tofauti. Katika itikadi hii watu weupe wenye damu safi ya Kigermanik walikuwa juu kabisa kama watu wa Skandninavia, Wajerumani na sehemu ya Waingereza. Lakini Waslavoni wa Ulaya ya Mashariki walitazamiwa kuwa wa ngazi ya chini; Warusi waliitwa "Untermensch" (mwanadamu duni). Watu wenye rangi kama Waafrika mara nyingi walitazamiwa kuwa duni zaidi.

Lakini wabaya kabisa machoni pa itikadi hii walikuwa Wayahudi waliotazamiwa kama mbari au rangi ya pekee. Walitazamiwa kuwa walilenga kutawala dunia kwa mikono yao mawili ya Ukomunisti wa kimataifa na ubebari wa kimataifa. Katika itikadi hii yote miwili ilitawaliwa na Wayahudi.

Kwa njia ya itikadi hii NSDAP ilifaulu kutunza uhusiano na mabepari Wajerumani wazalendo waliotoa misaada mingi kwa chama ikidai ya kwamba maovu ya ubepari yalitokana na Wayahudi tu. Kwa upande mwingine walivuta wafanyakazi waliozoea mapingamizi dhidi ya ubepari kutoka vyama vya kijamaa na wakomunisti.

Kuanza upya 1925

Baada ya kutoka gerezani Hitler aliunda NSDAP upya 1925. Akidharau demokrasia alianzisha muundo wa kijeshi ambako yeye mwenyewe kama kiongozi mkuu wa chama aliteua viongozi wa kimkoa wenye madaraka ya kuteua viongozi wengine wa ngazi za chini.

Hitler akisalimu maandamano ya chama; mbele ya gari lake wanamgambo wa SA, nyuma yake wa SS

Vikundi vya Chama

Kando la chama vikundi vya pekee viliundwa kama vile

  • vikosi vya ulinzi vya Sturmabteilung (SA) na Schutzstaffel (SS);
  • vikundi vya vijana kama Hitlerjugend (Wavulana kwa Hitler), BDM (wasichana), Umoja wa wanawake wa kizalendo-kisoshalisti, Maungano wa wanafunzi katika NSDAP, Shirika la madereva wa NSDAP na vingi vingine kwa karibu kila kikundi katika jamii. Baada ya mwaka 1933 Wajerumani wengi walipaswa kujiunga na vikundi hivi vya walimu, wakulima, madaktari, wanasheria wenye mwelekeo wa kijamii-kisoshalisti.

Kufanyikiwa tangu 1930

Hadi 1930 chama kilikuwa kikapanua katika maeneo mbalimbali ya Ujerumani lakini hakikufaulu kisiasa kikapata kura chache tu katika chaguzi zote. Uchaguzi wa kitaifa 1928 iliona asilimia 2.6 kwa NSDAP pekee.

Matatizo ya kiuchumi ya kimataifa ya 1929 yalisababisha wafanyakazi wengi kupoteza kazi wakikatika tamaa juu ya siasa ya demokrasia. Serikali ya kidemokrasia ya Ujerumani ilishindwa kuzuia matatizo haya na vyama vya bunge vilifarakana vikasababisha kuvunjwa kwa bunga mara kadhaa.

Katika chaguzi hizi NSDAP ilianza kusogea mbele kwa sababu watu wasio na tumaini ya serikali tena waliipigia kura. Idadi ya wanachama ilikua haraka ikafikia 850,000 kabla ya kushika serikali.

Katika uchaguzi wa 31 Juli 1932 NSDAP ilipata asilimia 37,3 % za kura ikawa chama kikubwa bungeni lakini haikuingizwa katika serikali. Rais Paul von Hindenburg alimdharau Hitler akakataa kumpa madaraka. Uchaguzi wa pili wa 1932 katika Novemba ukaleta kupunguiwa kwa chama kilichoshika 33,1% pekee.

Kuingia serikalini 1933

Lakini serikali mpya ilivunjika tena mwezi wa Januari 1933 na Chansella von Papen alipaswa kutafuta washiriki wapya. Hapa alimwomba rais akubali kuingiza NSDAP serikalini kwa imani ya kwamba wanasiasa wa chama chake watafaulu kumsimamia Hitler na wafuasi wake. Hii ilikuwa kosa kwa sababu Hitler alikuwa tayari kushika madaraka yote na nafasi zote za serikali kwa lengo la kutoziacha tena.

Tarehe 30 Januari 1933 Hitler aliapishwa na rais kuwa chansella mpya katika serikali ya ushirikiano.

Muundo wa NSDAP mnamo 1938

Uchaguzi wa mwisho katika Ujerumani hadi 1946 ulifanyiwa tar. 5 Machi 1933. Hitler alitumia nafasi ya moto kwenye bunge kupitisha sheria za dharura kwa usalama wa taifa. Kwa msaada wa sheria hii alipiga marufuku chama cha kikomunisti na kuanzisha mateso dhidi ya chama kikubwa cha kijamaa SPD. Uchaguzi ulifanyika kwa hofu upande wa wapinzaniwa Hitler wengi walikamatwa tayari. NSDAP ilipata 44 % za kura ikapaswa kuingia katika serikali ya ushirikiano tena.

Sheria ya kuipa serikali madaraka ya bunge

Kwa tishio mbalimbali Hitler alipata kibali cha vyama vya katikati kwa sheria ya kuipa serikali madaraka ya kibunge kwa muda. Sasa aliweza kutangaza sheria bila bunge kwa kibali cha rais tu. Alihitaji theluthi mbili za kura za bunge kwa sheria hii alizipata kwa sababu wabunge wakomunisti walikataliwa kuhudhhuria na sehemu ya wabunge wa SPD walikamatwa tayari.

Chama cha pekee

Sheria hii ya kumpa madaraka ilikuwa msingi wa kugeuza Ujerumani kuwa udikteta katika muda wa miezi michache. Rais von Hindenburg alikuwa mzee asiyeelewa tena mabadiliko yaliyotokea. Hitler aliendelea kutangaza sheria za kupiga marufuku vyama vya upinzani. VYama vingine vilijiondoa wenyewe. Sheria ya Desemba 1933 ilitangaza NSDAP kuwa chama cha kisiasa cha pekee katika Ujerumani.

Uchaguzi wa Novemba 1933 ilifanyiwa na wagombea wa NSDAP pekee. Baada ya kifo cha rais Hindenburg Hitler alichgauliwa na bunge kuwa "rais na kiongozi wa taifa".

Sasa chama kilikuwa muhimu sana. Watu wengi walipaswa kuwa wanachama wakitafuta ajira au nafasi mpya za kazi. Viongozi wa chama kwenye ngazi za mikoa, wilaya, miji na vijiji walikuwa na athira kubwa katika maazimio yote ya serikali.

Uanachama

Idadi ya wanachama wa NSDAP iliendelea hivyo:

Mwaka Wanachama
1919 55
1921 3.000
1923 55.287
1928 96.918
1930 129.563
1933 849.000
1935 2.493.890
1937 2.793.890
1938 4.985.400
1939 5.339.567
1942 7.100.000
1943 7.600.000
Januari 1945 8.000.000
15. Mei 1945 0

Mwisho

NSDAP ilipigwa marufuku na mataifa washindi tar. 10 Mei 1945 baada ya mwisho wa Vita Kuu ya Pili ya Dunia. Nembo la chama ni marufuku katika Ujerumani hadi leo.

Viungo vya Nje

WikiMedia Commons
WikiMedia Commons
Wikimedia Commons ina media kuhusu: