Wangari Maathai

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Wangari Maathai akipokea tuzo kutoka Tume ya Kitaifa ya Haki za Binadamu ya Kenya

Wangari Muta Maathai (1 Aprili 1940 – 25 Septemba 2011) alikuwa mwanaharakati wa masuala ya mazingira na haki za wanawake kutoka nchini Kenya. Mwaka wa 2004 alikuwa mshindi wa Tuzo ya Nobel ya Amani.[1] Yeye ni mwanamke Mwafrika wa kwanza kupokea tuzo hilo. Pia, aliwahi kuwa mbunge wa Kenya na waziri msaidizi katika serikali ya Mwai Kibaki kati ya Januari 2003 hadi Novemba 2005.

Katika maandalizi ya uchaguzi wa 2007 Maathai alisimama upande wa rais Kibaki lakini hakuteuliwa na chama cha PNU akagombea kwa chama cha Mazingira Green Party lakini hakurudi bungeni.

Elimu na Tuzo[hariri | hariri chanzo]

Maathai alihudhuria shule ya msingi ya Ihithe, halafu shule ya upili ya Loreto Convent, Limuru. Baada ya kuhitimu sekondari, alienda ng’ambo kusoma bayologia nchini Ujerumani na Marekani. Mwaka wa 1967, alipata shahada ya kwanza ya bayologia kutoka Chuo Kikuu cha Benedictine, Marekani. Aliendelea na masomo yake katika Chuo Kikuu cha Pittsburg ambako alipata shahada ya pili. Halafu alirudi Nairobi na kupata shahada ya udaktari kutoka Chuo Kikuu cha Nairobi katika somo la udaktari wa wanyama. Kuanzia mwaka wa 1977, Maathai alikuwa profesa msaidizi wa anatomia ya wanyama huko Nairobi akiwa mwanamke wa kwanza kupata uprofesa katika chuo kikuu cha Nairobi. Baadhi ya tuzo zake ni Tuzo ya Mwanamke ya Dunia (1983), Tuzo ya Goldman kwa Mazingira (1991), Elder of the Burning spear (2003) kutoka serikali ya Kenya, Tuzo ya Nobel ya Amani (2004), na Legion D’Honneur (2006) kutoka serikali ya Ufaransa.

Shirika la GBM[hariri | hariri chanzo]

Mwaka wa 1977, Maathai alianzisha shirika la Green Belt Movement ambalo linajihusisha hasa na mazingira, haki za raia na demokrasia.

Ndoa na familia[hariri | hariri chanzo]

Mwaka wa 1969, Wangari Muta (jina lake la kuzaliwa) alifunga ndoa na Mwangi Maathai, mwanasiasa wa Kenya. Wana watoto watatu, Waweru, Wanjira na Muta, lakini walitengana baadaye.

Marejeo chini ya ukurasa[hariri | hariri chanzo]

  1. Gettleman, Jeffrey. "Wangari Maathai, Nobel Peace Prize Laureate, Dies at 71," New York Times (US). 26 Septemba 2011; Abudulai, S.M. "Tribute to Wangari," Archived 7 Oktoba 2011 at the Wayback Machine. The Mail (Ghana). 4 Oktoba 2011.
Makala hii kuhusu mwanasiasa fulani bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Wangari Maathai kama wasifu wake, habari za maisha au kazi yake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.