Reichstag

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru

Reichstag(tamka: raikh-s-tag) ni neno la lugha ya Kijerumani linalotaja bunge la kihistoria la Ujerumani lakini pia jengo la bunge huko Berlin.

Martin Luther alivyojitetea mwaka 1519 mbele ya Reichstag na Kaisari Karolo V

Reichstag kama bunge la watemi hadi 1806[hariri | hariri chanzo]

Kiasili "Reichstag" ilikuwa mkutano wa watemi wote wa Dola Takatifu la Kiroma yaani Ujerumani [1] ulioitishwa na mfalme au kaisari. Mikutano ya aina ilijulikana tangu zamani za Kaisari Karolo Mkuu mnamo mwaka 800.

Baadaye Reichtag hadi mwaka 1806 ilikuwa mkutano wa wawakilishi wa watawala wadogo walioshauriana pamoja na kaisari au mwakilishi wake. Hapo ilikutana katika vikundi vitatu:

  1. kundi dogo la watemi wakuu wenye haki ya kupiga kura katika uchaguzi wa kaisari mpya; kwa jumla walikuwa kati ya 7 na 9.
  2. halmahauri ya watemi wa milki wenye wajumbe 100; watemi wakubwa zaidi walikuwa na kura zao lakini wale wadogo walishirikiana nafasi ya mjumbe 1.
  3. halmashauri ya miji ya milki yaani miji iliyojitegemea na haikuwa chini ya mtemi wowote.

Mwisho wa Dola Takatifu 1806 ulikuwa pia mwisho wa awamu hili la kwanza la Reichstag. Hali halisi halikuwa bunge kwa maana ya kisasa bali mkutano wa watemi au wawakilishi wao.

Hotuba ya Hitler mbele ya Reichstag 1933

Bunge la Dola la Ujerumani 1871 - 1945[hariri | hariri chanzo]

Bunge la kwanza lenye jina hili lilikuwa bunge la Shirikisho la Ujerumani ya Kaskazini tangu 1866 na 1970. Baada ya kuundwa kwa umoja wa Ujerumani kutokana na ushindi katika vita ya vita ya Ujerumani na Ufaransa ya 1870/71 bunge la Dola la Ujerumani lilipewa pia jina la "Reichstag". Likaendelea kwa jina hili kama bunge la milki ya Kaisari hadi 1918, kama bunge la Jamhuri ya Weimar hadi 1933 na mwishoni kama bunge la Dola la Tatu hadi 1945 mwaka ambako Dola la Ujerumani lilikwisha baada ya vita kuu ya pili ya dunia.

Jengo la Reichstag mjini Berlin tangu 1990

Jengo la mjini Berlin linaloitwa "Reichstag"[hariri | hariri chanzo]

Reichstag ni pia jina la jengo la bunge la Bundestag katika mji wa Berlin. Baada ya umoja wa Ujerumani katika karne ya 19 na kuundwa kwa Dola la Ujerumani hapakuwa na jengo la kufaa. Jengo jipya kwa ajili ya bunge hili lilimalizika mwaka 1894 likajulikana kama "jengo la Reichstag". Mwaka 1933 lilichomwa halikutumiwa tena wakati wa Hitler. Baada ya vita lilikaa karibu na mpaka uliotenganisha sehemu mbili za Berlin upande wa magharibi. Kwa hiyo halikuwa sehemu ya Berlin mji mkuu wa Ujerumani ya Mashariki na bunge la Ujerumani ya Magharibi lilikaa Bonn. Serikali ya magharibi likatengeneza nyumba likatumiwa kama makumbusho na pia kwa ajili ya mikutano ya kamati za bunge ya Bonn.

Tangu umoja wa Ujerumani wa pili tangu mwaka 1990 bunge la umoja likaamua kuhamia Berlin na kutumia jengo la Reichstag tena kama jumba yake. Hata kama bunge hili haliitwi tena "Reichstag" bali "Bundestag" makao yake hujulikana kwa jina la kale.

  1. hili lilikuwa jina rasmi la Ujerumani kati ya 800 na 1806