Tume ya Kuratibu Udhibiti wa Dawa za Kulevya

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA

Tume ya Kuratibu Uthibiti wa Dawa za Kulevya Tanzania (Kiingereza: Drugs Control Commission of Tanzania au kwa kifupi DCC ni chombo cha umma ambacho kinashirikiana na serikali ya Tanzania. Kilianzishwa kwa sheria ya bunge Bunge la Jamhuri ya Muungano ya Tanzania ya mwaka wa 2013 ili kupambana na utumiaji wa dawa za kulevya pamoja na usafirishaji. Tume hii ipo chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu. Ofisi zake kuu zipo Jijini Dar es Salaam.

Muundo wa tume[hariri | hariri chanzo]

Kifungu cha 4(5) cha sheria hiyo kimewataja wajumbe wa Tume chini ya Uenyekiti wa Waziri Mkuu kama ifuatavyo:-
  • Waziri anayeshughulikia Mambo ya Sheria
  • Waziri anayeshughulikia Mambo ya Ndani ya Nchi
  • Waziri anayeshughulikia Afya
  • Waziri anayeshughulikia Maendeleo ya Jamii
  • Waziri anayeshughulikia Mambo ya Nchi za Nje
  • Waziri anayeshughulikia Fedha
  • Waziri anayeshughulikia Maendeleo ya Vijana
  • Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Kiongozi Zanzibar
  • Waziri anayeshughulikia Utalii (Zanzibar)
  • Waziri anayeshughulikia Mipango (Zanzibar)

Mawaziri wengine wanaweza kukaribishwa kutegemeana na ajenda za kikao. Vilevile tume inaweza kumkaribisha mtu yeyote mwingine aliyemstari wa mbele katika mapambano dhidi ya dawa za kulevya.

Vikao vya tume[hariri | hariri chanzo]

Kwa mujibu wa sheria, tume inatakiwa kukutana si chini ya mara mbili kwa mwaka. Katibu wa vikao hivyo ni Kamishna wa tume ambaye pia ni mtendaji mkuu wa shughuli za kila siku za tume.

Ofisi ya Kamishina[hariri | hariri chanzo]

Uendeshaji wa shughuli za kila siku za tume hufanywa na Kamishna akisaidiwa na timu ya wataalamu wa fani mbali mbali. Ofisi ya tume imeundwa na Sehemu (section) tatu na vitengo (units) vinne kama ifuatavyo:-
  • Kitengo cha Utawala na Utumishi,
  • Kitengo cha Ukaguzi wa Ndani,
  • Kitengo cha Fedha na Uhasibu,
  • Kitengo cha Manunuzi na Ugavi,
  • Sehemu ya Sera, Mipango na Sheria,
  • Sehemu ya Udhibiti, Uchunguzi na Utafiti na
  • Sehemu ya Elimu, Habari na Takwimu

Kazi za tume[hariri | hariri chanzo]

Kifungu cha 5 cha sheria hiyo kinataja majukumu ya Tume kuwa ni kuainisha, kuhamasisha na kuratibu utekelezaji wa sera ya Serikali ya udhibiti wa matumizi na biashara haramu ya dawa za kulevya kwa kufanya mambo yafuatayo:-

  • Kuandaa na kusimamia utekelezaji wa mpango wa taifa wa udhibiti wa dawa za kulevya.
  • Kusimamia utekelezaji wa mikataba na itifaki za kimataifa katika udhibiti wa dawa za kulevya.
  • Kupitia Sheria na Kanuni za udhibiti wa dawa za kulevya na kupendekeza marekebisho ili ziendane na wakati.
  • Kukuza jitihada za kuzuia matumizi ya dawa za kulevya ikiwa ni pamoja na kutoa elimu kwa umma kuhusu madhara ya dawa za kulevya.
  • Kuanzisha mfumo wa ukusanyaji, uchambuzi na utoaji wa taarifa za tatizo la utumiaji na biashara haramu ya dawa za kulevya.
  • Kuanzisha mipango ya tiba na urekebishaji wa watu walioathirika na dawa za kulevya.
  • Kufanya tafiti kuhusu tatizo la dawa za kulevya.
  • Kutoa mafunzo kwa wanaojihusisha na udhibiti wa matumizi na biashara haramu ya dawa za kulevya.
  • Kuimarisha na kuendeleza uhusiano wa kimataifa katika udhibiti wa dawa za kulevya.
  • Kuratibu na kusaidia shughuli zinazofanywa na asasi na vikundi mbali mbali vya kijamii vinavyoshiriki katika kupiga vita dawa za kulevya.
Aidha, Tume inatakiwa kutoa taarifa ya hali ya dawa za kulevya nchini na kuiwasilisha bungeni kila mwaka. Taarifa zimekuwa zikitolewa na kuwasilishwa bungeni tangu mwaka 2003.

Kupunguza upatikanaji wa dawa za kulevya[hariri | hariri chanzo]

  • Kuteketeza mashamba ya bangi.
  • Kuimarisha ulinzi na udhibiti katika mipaka ya nchi, viwanja vya ndege na kwenye maji.
  • Kuimarisha operesheni za ukamataji wa dawa za kulevya mitaani.
  • Kuongeza uwezo wa watendaji na vyombo vinavyojihusisha na udhibiti wa dawa za kulevya.
  • Kuimarisha udhibiti wa kemikali bashirifu (Precursor Chemicals) yaani kemikali zinazotumika katika kutengeneza dawa za kulevya.
  • Kuimarisha udhibiti wa dawa za tiba zenye madhara ya kulevya.

Kupunguza matumizi ya dawa za kulevya[hariri | hariri chanzo]

  • Kuongeza utoaji elimu juu ya athari za dawa za kulevya kupitia vyombo vya habari, mikutano, semina, matamasha, sanaa na michezo.
  • Kuendeleza na kuimarisha mpango wa utoaji tiba na urekebishaji tabia kwa waathirika wa dawa za kulevya.
  • Kuanzisha program zitakazosaidia familia na jamii kujiepusha na matumizi ya dawa za kulevya.

Kupunguza maambukizi ya VVU yatokanayo na matumizi ya dawa za kulevya[hariri | hariri chanzo]

  • Kufikisha huduma (outreach services) kwa watumiaji wa dawa za kulevya ambazo ni elimu juu ya tabia hatari na namna ya kupambana nazo pamoja na kutoa rufaa kama upimaji wa Virusi vya UKIMWI, tiba kwa watumiaji n.k.
  • Kutoa tiba kwa watumiaji wa dawa za kulevya
  • Kujenga vituo vya elimu na ushauri (drop in centres)

Kuongeza upatikanaji wa rasilimali za kupambana na dawa za Kulevya[hariri | hariri chanzo]

  • Kuhamasisha wahisani, idara/taasisi za serikali, mashirika binafsi, Asasi zisizo za kiserikali na wananchi kwa ujumla kuchangia rasilimali.
  • Kuimarisha udhibiti wa matumizi ya rasilimali.

Kuwa na sera na sheria madhubuti za kupambana na tatizo la dawa za kulevya[hariri | hariri chanzo]

  • Kuweka sera ya taifa ya udhibiti wa dawa za kulevya
  • Udhibiti wa dawa za kulevya kupewa kipaumbele katika mipango ya kitaifa
  • Kuboresha sheria za udhibiti wa dawa za kulevya

Kuimarisha uratibu wa udhibiti wa dawa za kulevya[hariri | hariri chanzo]

  • Kuimarisha mfumo wa udhibiti wa dawa za kulevya mfano, mfumo wa utoaji taarifa
  • Kuongeza ushirikiano wa vyombo vinavyojihusisha na udhibiti wa dawa za kulevya
  • Kuendeleza ushirikiano wa kimataifa katika udhibiti wa dawa za kulevya

Ujuzi halisi wa tatizo la dawa za kulevya nchini[hariri | hariri chanzo]

  • Kufanya tafiti kuhusu za dawa za kulevya
  • Kusambaza na kutangaza taarifa za tafiti mbalimbali za dawa za kulevya

Marejeo[hariri | hariri chanzo]

Tazama pia[hariri | hariri chanzo]

Viungo vya Nje[hariri | hariri chanzo]

Makala hii kuhusu mambo ya tiba bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Tume ya Kuratibu Udhibiti wa Dawa za Kulevya kama sababu yake au mahusiano yake na mada nyingine?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.