Nenda kwa yaliyomo

Roger Bannister

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Roger Bannister 1953.

Roger Bannister (23 Machi 1929 - 3 Machi 2018) alikuwa daktari wa mfumo wa fahamu na mwanariadha wa mbio za masafa mafupi na ya kati kutoka Uingereza.

Alikuwa mtoto wa pili kati ya watoto wanne katika familia yake. Wazazi wake walikuwa Wilfred Bannister, ambaye alikuwa mwalimu wa shule ya upili na Alice Bannister ambaye alikuwa mama wa nyumbani. Alikulia katika mazingira yenye msisitizo mkubwa wa elimu. Na wazazi wake walikuwa wakali sana juu ya suala zima la elimu. Akiwa bwana mdogo alionyesha shauku kubwa katika michezo na masomo.

Bannister akiwa katika shule ya upili ya wavulana ya Harrow, aliendelea kung’ara kwa kuonyesha shauku kubwa juu ya masomo na michezo. Alikuwa mcheza mpira mzuri na mwanariadha bora. Baada ya kumaliza shule ya sekondari, aliendelea na masomo yake katika Chuo Kikuu cha Oxford, ambako alisomea masomo ya tiba. Pamoja na hayo, alipenda kushiriki katika mbio za masafa mafupi na kati.

Mnamo Mei 6, 1954, Roger Bannister aliweka rekodi ya kihistoria kwa kuwa mtu wa kwanza kukimbia maili moja kwa muda wa chini ya dakika nne. Tukio hili lilifanyika kwenye Uwanja wa Michezo wa Iffley Road huko Oxford. Alikimbia maili moja kwa muda wa dakika 3:59.4, akivunja rekodi iliyowekwa na mtangulizi wake, Gunder Hägg wa Sweden. Mafanikio haya yalileta sifa kubwa kwake na yalikuwa hatua muhimu katika historia ya riadha.

Baada ya mafanikio yake katika riadha, Bannister aliendelea na masomo yake ya tiba na baadaye akawa daktari mashuhuri wa mfumo wa fahamu. Alifanya kazi katika hospitali mbalimbali na kuchangia sana katika utafiti wa magonjwa ya fahamu. Aliandika vitabu kadhaa kuhusu tiba na riadha, na pia alitoa mihadhara katika vyuo vikuu mbalimbali. Bannister aliheshimika sana katika nyanja zote mbili za riadha na tiba.

Roger Bannister alifariki dunia tarehe 3 Machi 2018, akiwa na umri wa miaka 88.