Globu ya Dunia

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Globu kubwa ya Dunia inachorwa katika karakana.

Globu ya Dunia (kutoka Kiingereza: globe) ni ramani ya Dunia iliyochorwa juu ya tufe. Ni kama mfano wa Dunia yetu unaolenga kuiga umbo lake halisi.

Globu huwa na faida kulinganishwa na ramani ya kawaida ilhali inaonyesha umbo la eneo pamoja na umbali na pembe. Ramani za Dunia yote haziwezi kuunganisha sifa hizo kwa sababu kadiri eneo lilivyo mbali na ikweta, mtupo wa umbo la tufe linabadilisha emba na umbali kwenye ramani bapa.

Historia[hariri | hariri chanzo]

Globu ya Dunia ndogo ya mezani.

Umbo la Dunia lilitambuliwa kuwa kama tufe tangu Hipparchus wakati wa karne ya 3 KK. Mfano wa kwanza wa globu ya Dunia inayojulikana ni ile ya mtaalamu wa Ugiriki wa Kale, Crates wa Mallus huko Cilicia (leo Uturuki), mnamo karne ya 2 KK.[1]

Kuna mifano kadhaa iliyotengenezwa na wanajiografia Waislamu wa kale, kwa mfano zamani za khalifa Al-Ma'mun katika karne ya 9 BK.[2][3]

Globu ya Dunia ya kale iliyohifadhiwa hadi sasa ni ile iliyotengenezwa na Martin Behaim wa Nürnberg, Ujerumani, mnamo mwaka 1492. Amerika ilionyeshwa kwa mara ya kwanza kwenye globu ya Dunia na Martin Waldseemueller mnamo 1507.

Utengenezaji[hariri | hariri chanzo]

Kanda za pembembili zilizochapishwa kwa utengenezaji wa globu ya Waldseemüller, 1507.

Globu za Dunia huandaliwa kwa kugawa ramani ya Dunia katika kanda nyembamba zenye pembe mbili juu na chini. Ziko pana kiasi kwenye eneo la ikweta na kuwa nyembamba kadri zinavyokaribia ncha za kusini na kaskazini. Kanda hizo hukatwa na kufungwa kwenye tufe.

Tufe hutobolewa na mhimili wa mzunguko baina ya ncha mbili na kuwekwa katika stendi kwa kuinama pembe ya 23.5°.

Tazama pia[hariri | hariri chanzo]

Marejeo[hariri | hariri chanzo]

  1. Earth Globe
  2. Meri, Josef W. Medieval Islamic Civilization: An Encyclopedia. Psychology Press. pp. 138–139. ISBN 978-0-415-96690-0. 
  3. Covington, Richard (2007), "Nakala iliyohifadhiwa", Saudi Aramco World, May-June 2007: 17–21, archived from the original on 2008-05-12, retrieved 2008-07-06