Ming'oko

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Picha ya mmea wa mng'oko (mtipu) kuonyesha jani lake.

Ming'oko ni aina ya viazi vilivyo na mnasaba na kiazi kikuu. Hutumiwa kama chakula katika maeneo ya Kusini mwa Tanzania hususani katika Mkoa wa Mtwara. Ming'oko hukua juu ya mizizi ya mmea utambaao unaoitwa mtipu (Dioscorea hirtiflora).

Ming'oko kwa kawaida huwa haipandwi, huvunwa tu katika misitu kama yavunwavyo tunda pori.

Upatikanaji[hariri | hariri chanzo]

Katika mkoa wa Mtwara ming'oko hupatikana sana katika vijiji kama Mtimbwilimbwi, Nanyamba (Nambahu) na kadhalika.

Mtipu hupatikana na hustawi hasa katika mapori au misitu ambayo imekaa miaka mingi sana bila ya kufanywa shughuli za kilimo.

Ming'oko pia imekuwa ikitumika kama biashara kutokana na kupendwa kwake, huwa inauzwa mibichi au ambayo tayari imeshapikwa.

Matayarisho[hariri | hariri chanzo]

Ming'oko ikishavunwa husafishwa na kupikwa na maji na chumvi kama kiungo pekee. Ikishaiva huwekwa katika sahani au ungo, tayari kwa kuliwa.

Watu wengi hupenda kula pamoja na pilipili iliyosagwa na chumvi pamoja.

Ming'oko pia hupondwa ili kuwa chakula kiitwacho kiasili kule kusini chikandanga.

Wakati mwingine hupondwa pamoja na unga hasa wa mhogo pamoja na viungo vingine ili kutumika kama mboga iitwayo nnabuhulie kule Mtwara: ni neno la lugha ya Kimakonde cha Mtwara linalomaanisha "msile kwa mboga nyingi".

Ladha[hariri | hariri chanzo]

Ming'oko haina ladha bainifu, ina asili tu ya ubaridi ambapo ikiliwa pamoja na chumvi au pilipili inaburudisha.

Makala hii kuhusu utamaduni wa Tanzania bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Ming'oko kama historia yake au mahusiano yake na mada nyingine?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.