Uwanja wa ndege

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Uwanja wa Ndege wa Afonso Pena nchini Brazil

Uwanja wa ndege ni mahali pa kutua na kuruka kwa eropleni. Kiini cha uwanja ni barabara ya ndege zinapoweza kutua na kuruka. Barabara hii pekee yake si uwanja wa ndege peke yake kuna pia majengo kama vile kituo cha abiria wa ndege, majengo ya kupakia mizigo, kutunza fueli,banda la ndege, mnara wa kuongezea ndege pamoja na njia za mawasiliano na sehemu za nje.

Kama uwanja wa ndege pana huduma za uhamiaji na forodha unaweza kuitwa “Uwanja wa ndege wa kimataifa” na mara nyingi ni kubwa kuliko uwanja unaohudumia usafiri ndani ya nchi pekee.

Miundombinu wa uwanja

Barabara za kutua na kuruka (runway)

Nyanja za ndege nyingi ni ndogo zikiwa na barabara ya kutua na kuruka 1 pekee yenye urefu hadi 1 km. Kama zinahudumiwa na ndege ndogo pekee mara nyingi huwa na barabara ya nyasi tu. Nyanja kubwa zinazohudumiwa na makampuni mbalimbali ya ndege huwa na barabara za lami au saruji zaidi ya moja zenye urefu wa 2 – 4 km. Kadri eropleni ni kubwa na nzito inahitaji barabara ndefu zaidi. Barabara ya ndege ndefu duniani iko China yenye kilomita 5.5. Kwenye nyanja za wastani barabara ileile hutumiwa kwa kutua na kuruka lakini kwenye nyanja zenye ndege nyingi sana barabara hizi zimetengwa.

Barabara za kando (taxiway)

Pamoja na barabara za kutua na kuruka uwanja mkubwa unahitaji pia barabara za kando (taxiway) zinazowezesha ndege kutembea kutoka sehemu moja ya uwanja hadi nyingine bila kuzuia matumizi ya barabara ya kutua na kuruka kwa ndege nyingine. Maana kuna umbali wa kilomita 1 au zaidi kutoka kituo cha abiria (terminal) hadi chanzo cha barabara ya kuruka na kutua. Katika nyanja kubwa kuna ndege zinazofika au kuondoka kila baada ya dakika chache kwa hiyo kila wakati kuna ndege zinazotembea kutoka mwisho wa barabara ya kutua (baada ya kufika) hadi kituo cha abiria au kinyume kutoka kituo cha abiria kuelekea chanzo cha barabara ya kuruka.

Muundo wa Uwanja wa Ndege

Kituo cha abiria (terminal)

Kituo cha abiria (terminal) ni jengo ambako abiria hufika ama kwa njia ya usafiri wa umma au kwa magari halafu kuingia kwenye ndege. Ni pia jengo ambako wanafika baada ya kumaliza safari kwa ndege. Kwa hiyo kituo hiki kinapaswa kuwa na nafasi za kuegesha magari pamoja na stendi za basi au hata kituo cha reli ndani au kando yake.

Ndani ya kituo cha abiria kuna sehemu za mapokezi ambako wasafiri huonyesha tiketi, kuandikishwa kwenye orodha ya abiria na kukabidhi mizigo kwa kampuni ya ndege. Halafu wanapita mlango wa polisi au watumishi wa usalama wanaochungulia vitambulisho au pasipoti na kuhakikisha watu wasilete vitu vya hatari.

Hapo Nyanja nyingi huwa na sehemu ya maduka, mikahawa au hoteli ambako abiria wanaweza kununua vitu mbalimbali au kukaa hadi saa ya kuondoka kwa ndege.

Ndani ya uwanja kuna milango au geti za kuondoka na kila eropleni ina geti yake wanapokutana abiria wa safari ileile. Hapa watumishi wanarudia kuangalia tiketi na kuongoza abiria ndani ya ndege.

Kwenye nyanja ndogo ndege zinafika kwenye uwanja mbele ya kituo cha abiria na abiria wenyewe hutembea kwa mguu kati ya kituo na eropleni. Kwenye nyanja kubwa zaidi wanasafirishwa kwa mabasi kati ya jengo na ndege. Nyanja kubwa za kisasa zina pia nafasi nyingi kwa ajili ya ndege kufika kwenye madaraja ya kusogezwa yanayowezesha abiria kutembea moja kwa moja kutoka ndege hadi jengo la kituo au kinyume.

Viwanja vya ndege Africa

1 March 2013

Johannesburgh

Cairo

Lagos

Cape Town

Nairobi

Durban

Addis Ababa

Casablanca

Tunis

Entebbe

Viungo vya nje