Majadiliano:Papa Fransisko

Yaliyomo ya ukurasa hayatumiki katika lugha nyingine.
Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Papa fransisko alizaliwa tarehe 17 Desemba 1936 huko Buenos Aires, mji mkuu wa Argentina, hivyo ni papa wa kwanza kutokea bara la Amerika. Pia ni wa kwanza kutoka Shirika la Yesu.

Baada ya masomo ya kemia na kipindi kifupi cha kazi, tarehe 11 Machi 1958 aliitikia wito wa kitawa na wa kipadri, akaweka nadhiri za muda tarehe 12 Machi 1960, akapata upadrisho tarehe 13 Desemba 1969.

Tarehe 22 Aprili 1973 aliweka nadhiri za daima.

Kati ya miaka 1973 na 1979 alikuwa mkuu wa shirika nchini Argentina.

Mwaka 1992 alichaguliwa kuwa askofu msaidizi wa Buenos Aires akapewa daraja hiyo tarehe 27 Juni mwaka huo, halafu akawa askofu mkuu wa Buenos Aires tarehe 28 Februari 1998, pia askofu wa Wakatoliki wa Mashariki wa Argentina wasio na askofu wa kwao tarehe 6 Novemba 1998, akateuliwa kuwa kardinali tarehe 21 Februari 2001.

Kati ya miaka 2005 na 2011 alikuwa rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki la Argentina.

Alichaguliwa Papa tarehe 13 Machi 2013, wiki mbili baada ya mtangulizi wake kung'atuka.

Tofauti na kawaida, alijichagulia jina lisilowahi kutumiwa na mapapa waliomtangulia. Chaguo hilo linaelekeza nia ya kufuata kwa namna fulani roho ya Fransisko wa Asizi.

Hata kabla ya kuchaguliwa alijulikana kwa unyenyekevu na ufukara wake, pamoja na juhudi za kutetea haki za wanyonge, imani sahihi na maadili ya Kanisa.

Tabia hizo alizileta katika ngazi ya juu ya Kanisa Katoliki, akijivutia mioyo ya watu wengi.

Tarehe 13 Aprili 2013 alichagua Jopo la Makardinali 8 kutoka mabara yote limsaidie kuongoza Kanisa na kurekebisha idara na ofisi zake huko Vatikano.

Tarehe 29 Juni 2013, Papa Fransisko alitoa waraka wake wa kwanza, "Lumen Fidei", kuhusu imani; huo ulifuatwa tarehe 24 Novemba 2013 na "Evangelii Gaudium" kuhusu uinjilishaji.

Tarehe 18 Juni 2015, alitoa barua ensiklika kwa watu wote "Laudato si'" kuhusu mazingira, mabadiliko ya hali ya hewa na maendeleo ya kufaa. Barua hiyo ilipokewa vizuri na wengi.