Ustaarabu

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru

Ustaarabu ni aina ya utamaduni uliyoendelea.

Ustaarabu wa Misri ya Kale ulibuni majengo ya piramidi miaka 5000 iliyopita.

Katika fani ya historia "ustaarabu" (kwa Kiingereza civilization) ni hali ya jamii iliyoendelea juu ya kuishi katika jumuiya ndogo zinazojitegema katika mahitaji yote. Kwenye hali ya ustaarabu watu wanashirikiana katika eneo kubwa zaidi, huwa na namna ya serikali. Shughuli zinagawanywa kati ya vikundi, matabaka na kazi mbalimbali chini ya kanuni na sheria zinazosimamiwa na mtawala au serikali.

Katika historia ustaarabu kwa maana hii ulitokea penye kilimo ambako wakulima walianza kutoa sehemu ya mapato yao kwa mtawala au serikali fulani. Mapato hayo yalitumiwa kugharamia jeshi au silaha kwa kutetea jamii, mafundi na wasanii, ujenzi wa mahekalu, maboma, mifereji ya umwagiliaji mashamba, ghala kwa mazao n.k.

Miji ilitokea ambako sehemu ya watu haikuzalisha vyakula bali kushughulika na kazi za pekee.

Mahitaji ya kusimamia na kupanga kodi na mahitaji mengine ya utawala yalisababisha kutokea kwa mbinu za kutunza kumbukumbu, hivyo vyanzo vya kuandika na kuhesabu.

Kwa maana hii "ustaarabu" hutazamiwa tofauti na maisha katika hali ya jumuiya ndogo ambako watu huishi katika koo ndogo za wakusanyaji, au makabila madogo yanayofuata zaidi mila na desturi lakini hawana mamlaka ya juu inayogharamiwa na wote.

Kati ya ustaarabu wa kwanza zinazojulikana katika historia kuna Mesopotamia, Misri ya Kale, Uhindi na China ambako ugawaji wa maji ya mito mikubwa katika mazingira yabisi yalikuwa msingi wa ushirikiano wa watu katika maeneo makubwa.

Makala hii kuhusu mambo ya kihistoria bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Ustaarabu kama enzi zake au matokeo yake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.