Niccolo Machiavelli

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru

Taswira ya Macchiavelli na Santi di Tito

Niccolo Machiavelli (3 Mei 146921 Juni 1527) alikuwa was a mwanasiasa, mwandishi na mwanafalsafa nchini Italia.

Machiavelli anajulikana duniani kwa maandiko yake ambamo alieleza siasa kama mbinu wa kutafuta na kutetea utawala bila kujali maadili au tofauti kati ya mema na mabaya.

Machiavelli alizaliwa mjini Firenze akaendelea kuishi hapa. Alijiunga na utumishi wa serikali ya jamhuri ya Firenze wakati watemi wa Medici walipofukuzwa mjini. Akawa katibu wa serikali na balozi yake katika safari mbalimbali za kutembelea watawala wa nje.

Kitabu ambacho kimekuwa maarufu cha Machiavelli ni "Il Principe" (tamka: il prin-chi-pe) au "Mtawala". Hapa alieleza masharti kwa kiongozi wa kisiasa.

Aliandika ya kwamba kuna vipindi vigumu katika maisha ya mataifa na madola ambako kiongozi wa kisiasa anahitajika atakayeshika utawala na kutengeneza upya misingi ya dola. Katika utekelezaji wa kazi hii anapaswa kushinda kwa namna yoyote akiondoa vizuizi na kushinda kila upinzani. Hatakiwi kubanwa na masharti wala sheria wa maadili. Machivelli aliandika ya kwamba ni afadhali kama mtawala anapendwa na kuhofiwa na wananchi wakati uleule. Ila tu kama anapaswa kuchagua kama atapendwa au atahofiwa kwa sababu haiwezekani kuwa na pande zote mbili wakati moja ni heri akihofiwa. Pia ni ushauri wa Machiavelli ya kwamba matendo ya kinyama yatekelezwa haraka na vikali kwa sababu yatasahauliwa; lakini mema yatolewe polepole na kidogo-kidogo ili yakumbukwe kwa muda mrefu. Mtawala anatakiwa kutetea kanuni za mema mbele ya watu hata kama yeye mwenyewe atatenda kinyume chake lakini ikiwezekana kwa siri.

Haya yote yatakiwa machoni pa Machiavelli kwa shabaha ya juu ambayo ni heri ya umma. Utawala wa kiongozi mmoja uwe kipindi tu na shabaha iwe jamhuri inayofuata sheria zake. Ila tu katika vipindi vya matatizo uongozi mkali unapaswa kuwepo.