Kisukuku

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Kiunzi cha mifupa cha Ichthyosauria (sauri ya bahari) kilichopatikana Ujerumani kusini aliyeishi takriban miaka milioni 200 - 100 iliyopita
Trilobiti walikuwa viumbe vya miaka milioni 444 iliyopita.
Mti uliokuwa jiwe
Archeopteryx ni ndege wa kwanza anayejulikana kutokana na visukuku akifanana bado na reptilia lakini anaonyesha manyoa tayari

Kisukuku (kwa Kiingereza: fossil) ni mabaki ya kiumbehai (mmea au mnyama) kutoka zamani za miaka 10,000 au zaidi. Visukuku vingi vina umri wa miaka milioni kadhaa.

Mabaki yanapatikana kwa umbo tofautitofauti, hasa kama:

  • visukuku vya kijiwe vinavyoweza kutupa picha ya viumbehai vya nyakati zilizopita, na
  • visukuku vya makaa na mafuta ambavyo ni chanzo muhimu cha nishati.

Visukuku vya kijiwe[hariri | hariri chanzo]

Mara nyingi miili ya wanyama na mimea imehifadhiwa kwa umbo la jiwe. Ni kama picha au hata sanamu ya kiumbe kile. Mifano bora imepatikana pale ambapo mmea au mwili wa mnyama ulianguka katika matope laini na kuzama chini haraka. Ndani ya matope laini mwili haukuoza shauri la uhaba wa oksijeni na uhaba wa bakteria. Polepole maji ya matope yaliingia ndani ya mwili na kujaza nafasi zilizojazwa awali na kiowevu cha seli wakati kiumbe kilipokuwa hai. Maji ya matope yalipeleka pia minerali mbalimbali ndani ya mwili. Jinsi mwendo huu ulivyoweza kuendelea bila kuzuiwa, polepole hata seli ziliweza kujazwa kwa vipande vidogo vya matope na minerali nyingine. Kama baada ya miaka mingi matope yalikauka, hata matope ndani ya seli za mwili ulikauka lakini kwa kutunza umbo la seli hizi. Kama ganda la matope liliendelea kufunikwa na tabaka za udongo wa juu, shindikizo la juu lilianza kubadilisha ule udongo kuwa jiwe na mwamba mashapo kabisa.

Kama mwili wenyewe umeshaoza hadi kiunzi cha mifupa kilifunikwa kuna pia visukuku vya mifupa tu. Viumbe kama konokono mara nyingi viliacha visukuku vya umbo la nje pekee, kwa sababu miili yao ni laini sana, hivyo ilipotea haraka, na ganda lao halikubali maji yenye minerali kuingia ndani yake.

Sehemu ambako mazingira yalifaa kwa kutokea kwa visukuku huitwa na wataalamu "Lagerstätte" (la-ger-ste-te, neno la Kijerumani) na hapa mifano mingi imewahi kuchimbwa. Kutokana na mwendo wa gandunia (yaani kukunjwa kwa ganda la dunia) sehemu hizi zinaweza kupatikana chini ya ardhi au juu mlimani.

Kwa njia hii ilitokea mifano kamili ya miili ya spishi zisizopatikana tena duniani. Wataalamu hulinganisha visukuku na wanyama au mimea ya leo na hapo wanapata picha juu ya mabadiliko ya spishi. Nadharia ya mageuko ya spishi iliathiriwa sana na matokeo ya utafiti wa visukuku.

Aina ya pekee ya visukuku ni wadudu waliofungwa ndani ya utomvu wa miti uliobadilika baadaye kuwa kaharabu.

Visukuku vya makaa na mafuta[hariri | hariri chanzo]

Sehemu kubwa ya mimea ya kale haikugeuka kuwa visukuku vya kijiwe bali mabaki yao yalibadilika wakati yalipokaa kama tabaka juu ya uso wa ardhi yalifunikwa kwa udongo na kubadilishwa kwa shindikizo na joto.

Makaa yote yaliyopo chini ya ardhi ni matokeo ya mchakato huo; ndani ya makaa wakati mwingine sehemu za miti bado zinaonekana lakini zimebadilishwa kuwa makaa. Hivyo asili ya makaa ni hasa misitu ya kale na miti yake.

Mafuta ya petroli yametokana na algae na mimea mingine ya baharini. Baada ya kufa mabaki yao yalizama chini hadi sakafu ya bahari. Kutokana na uhaba wa oksijeni hapo chini mabaki hayakuoza na tabaka nene za matope zilitokea. Kama maganda haya yalifunikwa polepole na udongo na minerali nyingine kulitokea mchakato wa mabadiliko kutokana na shindikizo na joto. Mchakato huu ulibadilisha matope ya mimea kuwa mafuta ya petroli. Hapa ilitokea pia gesi. Pale ambako gesi hii ilifungwa chini ya takaba ya miamba isiyopitika tunakuta siku hizi akiba za gesi asilia zinazofikiwa kwa kutoboa miamba na kupeleka gesi kwa mabomba pale inapohitajika kutumiwa.

Tazama pia[hariri | hariri chanzo]

Makala hii kuhusu mambo ya sayansi bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Kisukuku kama historia yake au mahusiano yake na mada nyingine?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.