Faka

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Faka (Alphecca) katika kundinyota yake ya Kasi ya Masakini – Corona Borealis jinsi inavyoonekana kwa mtazamaji wa Afrika ya Mashariki

Faka (ing. na lat. Alphecca pia α Alpha Coronae Borealis, kifupi Alpha CrB, α CrB) ni nyota angavu zaidi katika kundinyota la Kasi ya Masakini (Corona Borealis). Ni pia nyota angavu ya 14 kwenye anga ya usiku. Mwangaza unaoonekana unacheza kati ya mag 0.75 na 0.95.


Jina

Faka ilijulikana kwa mabaharia Waswahili tangu miaka mingi wakifuata njia yao baharini wakati wa usiku kwa msaada wa nyota. [1]. Walipokea jina hili kutoka kwa Waarabu wanaosema hapa فكة fakka ambayo ni kifupi cha jina kamili نير الفكه nayir al-fakka . „Fakka“ inamaanisha „iliyovunjika" waliona hapa bakuli iliyokatika maana duara ya nyota za kundinyota yake si kamili, „nayir“ inamaanisha „inayong’aa“. Zamani „fakka“ ilitaja kundinyota yote ya Kasi ya Masakini lakini sasa jina hili hutumiwa kwa nyota angavu zaidi tu au.

Kwa matumizi ya kimataifa Umoja wa Kimataifa wa Astronomia ulifuata mapokeo ya Waarabu na kuorodhesha nyota hii kwa jina la "Alphecca" [2] (kutoka al-fakka).

Kutokana na urithi wa Roma ya Kale kuna pia jina la Gemma (lat. kwa kito au almasi) [3]

Tabia

Faka - Alphecca ni nyotamaradufu yenye mwangaza unaoonekana wa Vmag 2.2. Iko kwa umbali na Dunia wa miakanuru 75. Nyota zake mbili zinazoonekana katika darubini kubwa zinaitwa α CrB A (Faka A) na α CrB B (Faka B), zote mbili ni nyota za safu kuu. Zinazungukana katika muda wa siku 17.36.

Masi ya Faka A ni M☉ 2.58 na nusukipenyo chake R☉ 3 (vizio vya kulinganisha na Jua letu) . Mwangaza halisi ni +0.16 ikiwa katika kundi la spektra A0 V.

Nyota ya Faka B ina masi ya M☉ 0.92 na nusukipenyo cha R☉ 0.9 (vizio vya kulinganisha na Jua letu) . Mwangaza halisi ni +5.05 ikiwa katika kundi la spektra G5. [4]

Tanbihi

  1. ling. Knappert 1993
  2. Naming Stars, tovuti ya Umoja wa Kimataifa wa Astronomia (Ukia), iliangaliwa Novemba 2017
  3. Allen, Richard Hinckley: Star-Names and their Meanings (1899) uk. 178
  4. Tomkin, J.; Popper, D. M. (June 1986), uk. 1435

Viungo vya Nje


Marejeo

  • Allen, Richard Hinckley: Star-Names and their Meanings; kwa G. E. Stechert New York, Leipzig, London, Paris 1899, ukurasa 59 (online kwenye archive.org)
  • Knappert, Jan: The Swahili Names of Stars, Planets and Constellations; The Indian Ocean Review September 1993 Volume 6 No. 3 September 1993, kurasa 6-7, ISSN 1031-2331
  • Lane, Edward William : An Arabic - English Lexicon by in eight parts – 1872 (Perseus Collection Arabic Materials Digitized Text Version v1.1 of reprint Beirut – Lebanon 1968) online hapa

Tomkin, J.; Popper, D. M. (June 1986). "Rediscussion of eclipsing binaries. XV - Alpha Coronae Borealis, a main-sequence system with components of types A and G". Astronomical Journal. 91: 1428. online hapa