Mmeng'enyo

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Mfumo wa Mmeng'enyo wa Chakula wa Binadamu
Tasfiri: utumbo Mwembamba (small intestine), utumbo mpana (large intestine), ini (liver), kongosho (pancrease), ulimi (tongue), tumbo (stomach), tezi za mate (salivary glands), umio (esophagus), puru (rectum), mkundu (anus)

Mmeng'enyo au umeng'enyaji (en:digestion) ni namna jinsi viumbehai humega chakula kwa pande ndogo zaidi halafu kwa dutu zinazoweza kupokelewa na mwili na kuwa virutubisho vyake.

Kazi hii inatekelezwa katika mfumo wa mmeng'enyo wa chakula. Kwa binadamu na wanyama wengi mmengenyo huwa na ngazi mbili

  • kusagasaga chakula kwa meno au pande nyingine ili kupata vipande vidogo zaidi
  • kumeng'enya vipande vya chakula kwa kemikali za mwilini kama vile vimeng’enya mbalimbali na asidi za tumboni ili kupasua molekuli kubwa kama protini kuwa molekuli ndogo zaidi zinazoweza kutumiwa na mwili kutoa nishati au kama vipande vya kujenga mwili mwenyewe. Utumbo huwa na bakteria nyingi za pekee zinazoshirikiana katika mmeng'enyo.

Njia ya mmeng'enyo wa binadamu[hariri | hariri chanzo]

Chakula kinaingia mwilini kwenye mdomo. Hapa kinasagwa kwa kukitafuna na kinachanganywa na mate ambayo ina ndani yake kimeng'enya kinachoanza kupasua wanga na sehemu ya mafuta kwenye chakula.

Kwa umbo la tope kinapelekwa kwenye tumbo ambako mchanganyo wa asidi na kimeng'enya cha pepsini kinapasua hasa molekuli za protini na yote huwa kama ujiuji. Wakati huohuo musuli za tumbo zinakoroga uji wa chakula kwa kujikaza na kulegea mara kwa mara. Hivyo dutu za chakula na kemikali za mwilini kama asidi na vimeng'enya huchanganywa vizuri zaidi. Chakula hukaa tumboni kwa muda wa takriban masaa matatu.[1]

Kutoka hapa uji wa chakula unaendelea katika utumbo wa duodeni na utumbo mwembamba. Vimeng'enya mbalimbali vinaongezwa na sehemu kubwa ya molekuli za mafuta hupasuliwa hapa. Pamoja na sehemu zilizopasuliwa awali molekuli ndogo zinafyonzwa hapa na kuingia kwenye damu. Damu inapeleka molekuli hizi za virutubisho kwenda viungo vya mwili vinavyozitumia. Kwa hiyo kazi kubwa ya mmeng'enyo inatokea kwenye utumbo mwembamba mwenye urefu wa mita sita [2]

Katika hatua inayofuata kwenye utumbo mpana maji na minerli na vitamini kadhaa vinafyonzwa na kuingia katika damu. Mabaki yasiyotumiwa na mwili hukandamizwa na kutoka mwilini kwa njia ya puru na mkundo.

Mchakato huo hutokea vilevile kwa mamalia yote na kimsingi pia kwenye vetebrata kwa jumla.

Marejeo[hariri | hariri chanzo]

  1. Morris, Neil; Ting Morris (1998). Jim Miles, Lynne French, ed. Children's First Encyclopedia (in English). Branka Surla, Rosie Alexander. II Bardfield Centre, Great Bardfield, Essex CM7 4SL: Miles Kelly Publishing Ltd. ISBN 1-84084-332-2. 
  2. My First Book on the Human Body (in English). 4 North Parade, Bath, BA1 1LF, UK: Robert Frederick Ltd. 2004. ISBN 0-7554-3506-0. 

Viungo vya Nje[hariri | hariri chanzo]