Libreville

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Muonekano wa Mji wa Libreville


Jiji la Libreville
Nchi Gabon
Mahali pa Libreville mkoani Estuaire
Nyumba ya uchansella mjini Libreville

Libreville ni mji mkuu na mji mkubwa nchini Gabon. Iko kwenye pwani la Atlantiki kiasi ndani ya mdomo wa mto Komo au mto Gabon. Kuna bandari.

Libreville ina wakazi 578,000 (2005). Jina la “Libreville” lina maana ya “mji huru” au “mji wa watu huru” kutokana na historia yake.

Historia[hariri | hariri chanzo]

Libreville ilianzishwa na Wafaransa kama kituo cha biashara kwa jina la Gabon kufuatana na mto uliopo baada ya kununua ardhi tangu 1839 BK. Wakati ule wenyeji wa eneo walikuwa hasa Wampongwe. 1843 Wafaransa walijenga boma la Fort Aumale kama bandari ya kijeshi.

Mwaka 1848 idadi ya wakazi iliongezeka ghafla kwa watumwa waliowekwa huru. Wakati ule meli za kijeshi za Ufaransa zilishirikiana na Waingerezea katika majaribio ya kukomesha biashara ya watumwa. Walikamata meli ya L'Elizia na kupeleka mzigo wake wa watumwa Gabon walipopewa uhuru. Wakati ule kituo kilipanuka kuwa mji mdogo ukapewa jina la Libreville kwa kuiga mji wa “Freetown” huko Sierra Leone ambako Waingerezea waliwahi kupangisha watumwa waliopewa uhuru.

Tangu 1866 ikawa makao makuu ya jimbo la Gabon. katika karne ya 20 ikawa bandari kuu ya Afrika ya Ikweta ya Kifaransa ikaendelea kukua polepole. Tangu uhuru wa Gabon mwaka 1960 imekuwa mji mkuu wa nchi hii.

Mji[hariri | hariri chanzo]

Kuna mitaa ndani ya mji ya Batterie IV, Quartier Louis, Mont-Bouët, Nombakélé, Glass (Uzunguni), Olaumi (mtaa wa viwanda) na Lalala. Mtaa wa Owendo kusini ya mji pana bandari na kituo cha reli.

Libreville ina makumbusho ya kitaifa yenye vinyago vingi vya utamaduni wa wananchi. Soko kuu ni Marché du Mont-Bouët mashariki ya kitovu cha mji. Libreville kuna vyuo vikuu vya Université Omar Bongo (UOB), Université des Sciences de la Santé, Chuo cha Ufundi Omar Bongo Ondimba Technical School na taasisi mbalimbali ndogo. Uwanja wa ndege wa kimataifa kiko nje ya mji.