Jumatano

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru

Jumatano ni siku ya nne katika juma (wiki) ya siku saba yenye asili ya kiyahudi-kikristo. Iko kati ya siku za Jumanne na Alhamisi.

Siku ya tatu au siku ya nne?[hariri | hariri chanzo]

Kuna nchi zilizobadilisha hesabu ya juma kufuatana na kawaida ya mapumziko ya "wikendi" kwenye siku za Jumamosi/Jumapili. Katika muundo huu Jumatatu hutazamiwa kama siku ya kwanza katika juma ya kazi hivyo inahesabiwa kama siku namba "1" ya wiki katika kalenda hata kama jumuiya za kidini zinasisitiza hesabu ya kibiblia.

Jina la siku kwa Kiswahili na kwa lugha mbalimbali[hariri | hariri chanzo]

Katika lugha ya Kiswahili jina la siku lina namba "5" ndani yake. Hii ni dokezo la asili ya Kiswahili katika utamaduni ya Kiislamu pasipo na athira ya Uyahudi unaoanza hesabu baada ya sikukuu ya Kiislamu ya Ijumaa siku ya sala ya pamoja: Jumamosi kama siku ya kwanza baada ya Ijumaa, Jumapili kama siku ya pili, Jumatatu kama siku ya tatu n.k.. Tabia hii katika Kiswahili ni ya pekee hasa kwa sababu Kiarabu ambacho ni lugha ya Korani takatifu na lugha ya kimataifa ya Waislamu kinafuata hesabu ya Kiyahudi na kuiita أربعاء arba'a (ya nne).

Lugha nyingi za nchi za Kiislamu zafuata kawaida ya Kiarabu na kuiita "siku ya nne", kwa mfano Kiindonesia (Rabu - ya nne) au Kiajemi (Farsi) (چهارشنبه - tchahor shanbe - siku ya nne).

Katika lugha nyingi za Ulaya jina la siku hutunza kumbukumbu ya miungu iliyoabudiwa zamani za dini za Kiroma au Kigermanik kama vile Kifaransa "Mercredi" (siku ya Mercurius) au Kiingereza "Wednesday" (siku ya Wodan).

Makala hii kuhusu mambo ya sayansi bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Jumatano kama historia yake au mahusiano yake na mada nyingine?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.
Siku za juma (wiki)
Jumapili - Jumatatu - Jumanne - Jumatano - Alhamisi - Ijumaa - Jumamosi