Msaada:Tafsiri

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru

Tafsiri ni njia mojawapo ya kutunga makala katika Wikipedia ya Kiswahili (swwiki). Mara nyingi tutatumia makala za Wikipedia ya Kiingereza (enwiki) au Simple Wikipedia (simple - inajaribu kutumia Kiingereza chepesi, lakini wakati mwingine wepesi wake ni maelezo ya kitoto tu).

Kabla ya kutafsiri[hariri | hariri chanzo]

Kuna mambo kadhaa tunayohitaji kuyaangalia kabla ya kutafsiri:

  • Je makala ya enwiki inafaa? Hata katika enwiki kuna makala mbaya! Wakati mwingine makala, kwa namna ya pekee kuhusu habari za Afrika, zinaweza kuwa zimetungwa miaka ya nyuma, hivyo si sahihi tena (mfano: wakati wa kuanzisha ukurasa huu mwaka 2021, makala ya enwiki en:Bagamoyo Port ya 2018 inaeleza maendeleo ya mradi ambao kumbe umesimamishwa tangu mwaka 2019).
  • Je inaeleweka? Je, inatumia lugha ngumu? Usipoelewa lugha, acha! Heri kutotafsiri kuliko kutafsiri habari ambazo si kweli au hazieleweki!
  • Je makala ni ndefu sana? Utaona mwenyewe: si rahisi kutafsiri matini ndefu. Angalia kama makala ina utangulizi unaoleta hitimisho ya habari kuu, pengine huo unaweza kutosha kwa kuanza mada. Kama hitimisho haina marejeo / tanbihi, lazima uzitafute baadaye katika matini inayofuata ambayo hutatafsiri.
  • Je makala ya enwiki inatumia sentensi ndefu zenye muundo tata? Usitafsiri neno kwa neno! Utahitaji kutafakari kwanza, halafu pengine kumega sentensi sehemusehemu na kutunga sentensi 2, 3 au zaidi kwa Kiswahili.

Hifadhi katika sehemu yako kwanza[hariri | hariri chanzo]

  • Tunakushauri kutunga makala zako mwanzoni ndani ya sehemu yako ya mtumiaji (userspace), na kumwomba mwingine kuzisoma. Baadaye unaweza kuzihamisha katika sehemu ya makala.
    • Hapo utafungua ukurasa wako wa mtumiaji. Kwenye URL (juu kabisa) utaona "https://sw.wikipedia.org/wiki/Mtumiaji:JINA".
    • Sasa utaongeza kwenye URL mstari wa "/" halafu jina la makala, itakuwa hivyo:
      • "https://sw.wikipedia.org/wiki/Mtumiaji:JINA/madayangu"
      • Bofya "Weka Chanzo" , utaona dirisha tupu, tunga makala na kuihifadhi. Uko huru kufanya makosa au majaribio maana uko katika sehemu yako.
      • Chini ya makala weka, pamoja na jamii nyingine, jamii yako [[Jamii:Mtumiaji:JINA]]. Jamii hii itakusaidia kukuta makala yako baadaye, kama umesahau jina kamili. Usiongeze jamii nyingine.
  • Ukiwa na uhakika kwamba makala iko katika hali nzuri (pamoja na jamii, interwiki, fomati), uipeleke kwenye sehemu za makala. Hapo unabofya juu ya makala "Zaidi" ("more"), "Hamisha" utaona ukurasa mpya. Chini ya "Kuhamisha ukurasa", "Kuelekeza jina jipya / Kichwa cha habari kipya:" andika jina jipya upande wa kulia badala yale yaliyopo. Upande wa Kushoto fungua menyu badilisha "Mtaumiaji" iwe "(Kuu)".
      • Mwishoni utaondoa jamii yako [[Jamii:Mtumiaji:JINA]] (kazi yake ni kuikuta makala tu, jina lako kama mwanzilishaji limehifadhiwa milele kwenye historia ya makala, na michango yako yote utaona chini ya "Michango" juu ya ukurasa wako) . Halafu utaongeza jamii zinazotakiwa!.

(Ona: Msaada:Jamii)

Programu za kutafsiri[hariri | hariri chanzo]

Ona pia: Msaada:Tafsiri ya kompyuta

  • katika sanduku ya "Karibu" uliambiwa ni mwiko kumwaga matini kutoka google-translate au programu nyingine za kutafsiri. Ukifanya hivyo unaweza kuzuiwa haraka sana ukimwaga matokeo moja kwa moja.
  • Sababu ya kutangaza mwiko ni matokeo mabaya ya programu hizo. Zote zimeboreshwa kiasi, lakini bado zinaleta matokeo mabaya kwa Kiswahili. Tuna makala nyingi mno zilizotungwa kwa namna hiyo, nazo zinasababisha kazi kubwa kwa wanawikipedia wengine. Zinaharibu sifa ya Wikipedia yetu. Hapa tumeamua kuzizuia na pia kuzuia wachangiaji wanaopuuza utaratibu.
  • Hata hivyo ni azimio la kila mtu akiketi mbele ya kompyuta yake atumie programu hizi au la. Ukiweza kutumia matokeo ya programu kama pendekezo tu na kuondoa hitilafu hakuna upingamizi.

Kabla ya kutumia programu ya kutafsiri:[hariri | hariri chanzo]

  • Soma matini ya Kiingereza, tafakari unachotaka kusema kwa Kiswahili
  • Vunja sentensi ndefu za Kiingereza na kuzigawa kwa sentensi kadhaa za Kiswahili, kwa maneno yako. Programu zote zinashindwa kutafsiri sentensi ndefu.
  • Usifuate muundo wa sentensi ya Kiingereza kama ni tofauti na muundo wa Kiswahili. Mara nyingi Kiswahili kinatumia vitenzi ambako lugha za kizungu hutumia nomino pekee.
  • usikubali pendekezo la programu kwa maneno ya Kiingereza ambayo hujui au huna uhakika nayo. Utafute kwanza visawe vya Kiingereza (kwa mfano hapa), tafakari neno lina maana gani katika matini yako halafu utafute neno la Kiswahili.
  • Ujipatie Kamusi za TUKI English-Kiswahili na Kiswahili-English au nyingine. Zinapatikana mara kwa mara kwenye inteneti kwa kupakua kama pdf. Au ujaribu kurasa za kutafsiri tofauti kando-kando, pamoja na google kuna https://sw.glosbe.com.

Google translate[hariri | hariri chanzo]

  • Ukitumia google translate, ukumbuke daima udhaifu wake:
  • tafsiri yake inachanganya maneno, unaweza kupata maana ya kinyume kabisa! Hapo ni lazima usome kwa makini sana kila neno.
  • inatafsiri neno-kwa-neno. Hivyo inapanga sentensi au maelezo kwa namna isiyolingana na lugha ya pili na kuvifanya havieleweki. Hapo LAZIMA UTAFAKARI, washa bongo na andika sentensi inayoeleweka kwa bibi yako au kwa mtoto wa miaka 6. Kata habari ya Kiingereza kwa sentensi 2 au zaidi, usitumie tu maneno kwa tafsiri lakini tunga maelezo badala yake. Kama sentensi ya Kiingereza ina kitenzi mwishoni baada ya mfululizo wa maelezo lazima uiweke kwenye sehemu ya mwanzo.

Wikipedia Content Translation[hariri | hariri chanzo]

  • Kuna njia ya pili, ambayo haina tafsiri bora, lakini inaweza kusaidia upande wa fomati ya makala:
  • hii ni wenzo wa Maalum:ContentTranslation. Ukifungua ukurasa huo, utafika kwenye programu ya Wikipedia. Utachagua lugha asili ya makala (ama enwiki au simple) na lugha ya pili kama Kiswahili.
  • Hapa tahadhari ni takriban sawa kama kwenye google translate. Kasoro zake ni kidogo zaidi, inaweza kupendekeza makosa kidogo zaidi, lakini kimsingi makosa ni yaleyale.
  • Baada ya kumaliza ni lazima ufungue makala upya na kupitilia yote katika hali ya "Hariri"; hata ikisaidia fomati bado inasababisha vurugu katika fomati kadhaa.