Majadiliano ya mtumiaji:NIVOLALELA

Yaliyomo ya ukurasa hayatumiki katika lugha nyingine.
Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
              UFISADI
 Neno hili kwa kawaida lina maana ya maovu au uharibifu wa aina yoyote ile.Aidha laweza kuleta maana ya matumizi ya madaraka au mamlaka katika ofisi za umma au za kibinafsi kwa manufaa ya mtu binafsi au kundi la watu.Wanaojihusisha katika ufisadi hujulikana kama mafisadi au kwa umoja mfisadi.
 Ufisadi unaweza kugawanywa katika viwango viwili vikuu.Mosi kuna ufisadi wa kiwango cha chini.Hizi ni sakata zinazohusisha watu wa kila siku na wa kawaida katika jamii.Kuna mifano anuwai ya ufisadi wa kiwango cha chini.Maafisa wa trafiki katika barabara hupokea milungura kutoka kwa wenye magari yaliyo na kasoro ili wasiadhibiwe kulingana na sheria.Hii hupelekea abiria kupakiwa mithili ya magunia ya kabeji jambo ambalo huchangia kuongezeka kwa ajali za barabarani zinazowaua watu wengi.Tamaa ya madereva hawa kupata pesa zaidi kutokana na kubeba abiria wengi kupita kiasi huwapelekea kupoteza kazi zao na maisha yao vilevile.
 Ufisadi huonekana wakati raia anapokosa kupewa huduma inavyotakikana.Sakata za watu kuto kitu kidogo ili faili zao zipatikane ofisini si jambo la ajabu.Watoaji huduma hospitalini na katika zahanati za umma hutuma wagonjwa katika kliniki zao au za marafiki zao ili wapate kiinua mgongo badala ya kuwahudumia inavyotakikana.Maafisa wa kuchunguza ubora wa bidhaa hupokea rushwa ili kuruhusu bibhaa zisizostahili kutumika kuendelea kutumika.Jambo hili huwa tishio kwa maisha ya wananchi wanaoendelea kutumia bidhaa hizi bila kujua hatari inayowakodolea macho.
 Aina ya pili ya sakata za ufisadi ni zile zilizofikia kiwango cha kimataifa.Kwa kawida hizi huhusisha utoaji na upokeaji wa mabilioni ya pesa. zabuni za ujenzi wa barabara hutolewa kwa makontrakta waliotayari kutoa chai.Huduma zingine zilizoadhiriwa na ufisadi ni zile za bima kwa mashirika au makampuni makubwa,zabuni za uagizaji wa bidhaa zinazohitajika kwa wingi kama magari ya serikali,madawa na kadhalika.Vilevile vituo vya forodha wakati mizigo inaingia au kutoka nchi moja kwenda nyingine vimeadhiriwa na ufisadi.
 Kuna mambo kadhaa yanayoimarisha na kukuza ufisadi katika nchi .Mojawapo wa mambo haya ni tamaa inayowasukuma watu kunyakua vya umma au vya wengine kiharamu.Aidha sheria dhaifu za nchi nyingi huchangia pakubwa kwa kuwa mafisadi hufahamu kuwa serikali hizi haziwatafanya lolote.Hivyo wao hupata motisha ya kuendeleza ufisadi.Wao hawachukuliwi hatua yoyote kwa sababu ya cheo au nafasi yao katika jamii.Viongozi wa nchi huchangia kukuza ufisadi kwa njia moja au nyingine.Wao hutumia vikaragosi wao kutekeleza shughuli zao za kifisadi.Wakati mwingi utapata kuwa,wanaotumiwa kutekeleza sakata hizi ni marafiki wa viongozi hao.Viongozi hawa pia huwapopea nyadhifa wafanyikazi wadogo kazinikwa kuwa ni jamaa au marafiki zao.Hivyo basi utenda kazi huadhiriwa,pesa kutumiwa vibaya na hatimaye umma hunyimwa huduma inayostahili.
 Njia nyingine inayochangia kustawisha ufisadi ni usimamizi mbaya wa fedha na mali ya umma.Mara nyingi utapata kwamba hakuna utaratibu mzuri wa matumizi ya pesa za umma,hesabu za matumizi hufanywa vibaya au kutokuwepo.Hivyo basi ufisadi hupata fursa mwafaka kupenyeza na kusakini.
 Madhara ya ufisadi hayahesabiki.Umma hupoteza pesa nyingi sana.Si ajabu kupata miradi ya umma iliyokwama au magofu ya nyumba za umma ambazo hazijakamilika ingawaje kandarasi ililipwa kitambo.Wahisani wa nchi husika hususia kutoa misaada kwa nchi hizi.Umaskini husakini na kukita mizizi.Vilevile wawekezaji wa kutoka nje na wa nchi hizo husika hulimatia kuwekeza nchini humo.Wao huhamia nchi zisizofisadi.Hivyo basi uchumi wa nchi husika huzorota na wananchi huishi katika dhiki na taabu isiyokadirika.Maadili ya jamii hudhoofika na wananchi kuendeleza ufisadi zaidi.Wao hupuuza kutekeleza wajibu wao ,kwa mfano,kulipa kodi,jambo linalonyima serikali fedha zinazotumiwa katika utoaji wa huduma kama za afya,elimu na kadhalika kwa watu wake.
 Kuna njia kadhaa zinazoweza kutumiwa kukabiliana na ufisadi.Sharti wananchi watambua hasara za ufisadi,wawajibike na kushikana bega kwa bega kukabiliana na ufisadi.Serikali lazima iweke utaratibu wa kupambana na ufisadi,kwa mfano,kuanzisha vikosi maaalum vya kupambana na ufisadi.Bunge lazima lipitishe sheria za kukabiliana na ufisadi vilivyo.Vijana pia wanapaswa kujiunga na kampeni za kukomesha ufisadi na kuihamasisha jamii kuhusu madhara ya ufisadi kwa kuielimisha.Kwa vyovyote vile sharti kimelea hiki cha ufisadi tukiangamize kutoka nchi zetu  kwa kuwa ufisadi ni kizingiti kikubwa cha maendeleo na ufanisi wa nchi yoyote ile.