Haiku

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru

Haiku ni aina ya shairi ambayo huandikwa hasa katika nchi ya Japani. Matsuo Basho ndiye mwanzilishi wa aina hii ya kipekee ya shairi. Hata hivyo, nchi nyingine mbali na Japani zimeanza kuandika haiku. Malenga toka sehemu nyingi ikitia ndani Kenya wamejitosa katika ukumbi wa uwandishi wa haiku.

Shairi hii huwa na mishororo mitatu na ubeti mmoja pekee. Mshororo wa kwanza huwa na silabi tano, mshororo wa pili huwa na silabi saba na mshororo wa tatu na ambao ndio wa mwisho, huwa na silabi tano. Hivyo kwa jumla, haiku huwa na silabi kumi na saba. Haiku yenye kufuatilia arudhi ya aina hii ni haiku ya kitamaduni. Malenga wengi nchini Japani huandika shairi la kitamaduni lenye kufuatilia mpango wa silabi 5-7-5. Malenga ambao sio wajapani huandika kufuatia mtindo huu. Hata hivyo, kwa sababu ya tofauti iliyopo kati ya lugha ya kijapani na lugha za nchi hizi zingine, malenga wasio wajapani wanaweza kuandika haiku ambazo hazifuatilii mpangilio wa silabi wa 5-7-5.

Jambo la kuzingatia kwa malenga wasio wajapani ni kwamba, haiku zisizofuatilia mpangilio wa 5-7-5 zinatakiwa kuwa fupi. Hii ni kusema kwamba badala ya mshororo wa kwanza kuwa na silabi 5, malenga ajaribu kufupisha mpaka silabi nne au tatu. Hii ni kwa sababu ya tofauti inayopatikana katika kuhesabu silabi.

Kwa mfano:

Neno 'tanka' kwa kawaida, na jinsi ambavyo sisi wa Bantu huhesabu silabi, lina silabi mbili. Hizi ni 'tan' na 'ka'. Hata hivyo, kwa lugha ya kijapani, neno 'tanka' lina silabi tatu! Hizi ni 'ta', 'n' na 'ka'. Kwa sababu hii, malenga ambaye anaandika haiku kwa lugha ya kiingereza anapaswa kufupisha maneno ili asipitishe idadi ya silabi inayotakikana( 5-7-5 jumla ya 17). Hii inaonyesha changamoto kubwa iliyopo kwa malenga wa haiku ambao wangependa kuandika haiku kwa lugha ya kiswahili. Mpaka hivi sasa, unaweza tu kuandika haiku kwa Kiswahili alafu upeane tafsiri yake kwa lugha ya kiingereza; watu wachache ambao husoma na kuelewa kiswahili pekee wanaelewa kwa kina HAIKU ni nini, chanzo chake an jinsi ya kuandika aina hii ya shairi.

Malenga anatakiwa kubuni haiku kutokana na mazingara aliyomo ndani yake. Haiku haipaswi kuwa ya kufikiri bali inapaswa kuwa kama picha ya jambo fulani ambalo malenga ameliona kutoka katika mazingira yake na kisha kubuni haiku. Hivyo basi haiku kwa kiasi kikubwa ni kama picha ya jambo ambalo linahusu mazingira na ambalo malenga amelishuhudia mwenyewe wala si la kufikiria na wakati huo, akabuni haiku.

Tunaposoma haiku kama hadhira, tunapaswa kutembelea njia ambayo malenga alitembelea kimawazo na kuona 'picha' aliyoona. Haiku inaweza kuongelea hali ya anga, msimo uliopo wakati wa kubuniwa kwa haiku hiyo na pia kuhusu mambo ya kila siku ya maisha yetu; mapenzi, kifo, ndoa, tamasha mbalimbali na siku kuu za nchi kama vile Siku kuu ya Madaraka au siku kuu ya wafanyikazi na kadhalika.

Mambo ya Kuzingatia unapoandika Haiku[hariri | hariri chanzo]

1. Andika ubeti mmoja pekee. Muundo wa ubeti huu unapaswa kuwa ule wa: msororo wa kwanza mfupi/mshororo wa pili mrefu kuliko ule wa kwanza/ mshoro wa tatu mfupi kama ule wa kwanza. Unaweza ukizingatia idadi ya silabi ambayo inapaswa kuwa katika mpango wa 5-7-5, au haiku yenye silabi zisizozidi 17 hata kama hautafuatilia mpango wa 5-7-5. Bora muundo uwe ule wa mshororo mfupi/mrefu/mfupi.

2. Zingatia msimu uliopo(KIGO kwa kijapani), unaweza kuwa msimu wa kiangazi au msimu wa mvua, baridi au jua. pia unaweza kuwa wakati wa sikukuu ya Wafanyikazi, Madaraka au wakati wa wanafunzi kurudi shule, au msimu wa matunda kama mandizi, maembe na kadhalika. Jambo la maana ni kwamba haiku yako inapaswa kuwa na kigo; neno moja katika haiku ambalo linaonyesha msimu ambao haiku hiyo iliandikwa. Ili kuonyesha msimu uliopo na badala ya kuutaja, itakuwa vyema iwapo utataja neno linalohusianishwa na msimu huo (SEASON WORD kwa kiingereza).

Kwa mfano, badala ya kutaja msimu wa mvua, unaweza kutaja maneno kama matope, mbu, mafuriko na kadhalika.

3. Tumia kijistari (KIREJI kwa kijapani) ili kuonyesha mahali pa kutua na pia ili kubainisha kati ya wazo la kwanza na wazo la pili. Malenga ana uhuru wa kuweka kireji katika mshororo wa kwanza au wa pili ili kuashiria kituo. Hii ni kusema kwamba kati ya mishororo yote mitatu ya haiku, mishororo miwili inapaswa kusomeka kama mshororo mmoja na kufuatiwa na kireji, kisha mshororo wa tatu kusomeka peke yake. Au mshororo wa kwanza kusomeka peke yake ukifuatiwa na kireji, kisha mshororo wa pili na tatu kusomeka kama mshoro mmoja. Haiku inapaswa kuwa na mawazo mawili (two ideas). Mawazo haya yanatenganishwa na kijistari ili msomaji aweze kujua mahali wazo la kwanza linaishia na wazo la pili kuanzia. Kireji pia humsaidia msomaji ili aweze kusoma haiku kwa njia inayofaa.

Mifano ya haiku[hariri | hariri chanzo]

misty Saturday--

my Sunday-best dripping

in the moonlight


power rationing--

charred spots beside

the candle stick


nursing

a headless doll--

end of holidays


June cold--

dying candles beside the

condolence book


Zingatia muundo wa haiku hizi. Mshoro wa kwanza na wa tatu ni mfupi ikilinganishwa na mshororo wa pili. kila haiku ina neno moja ambalo linaashiria msimu ambao haiku hiyo iliandikwa.Maneno haya yanayoitwa KIGO ni "dripping," power rationing," "holidays," na "June cold" mtawalia. Haiku hizi pia zimeanza kwa herufi ndogo isipokuwa maneno ambayo huchukua herufi kubwa kama majina ya watu au miezi. Ona kireji jinsi kinavyotumika ili kutofautisha mawazo mawili na kuleta mtiririko unaofaa.

Kikundi cha Kenyasaijiki[hariri | hariri chanzo]

Kwa kumalizia, kuna kikundi cha malenga wa haiku nchini Kenya kijulikanacho kama Kenyasaijiki. Malenga katika kikundi hiki wanatia ndani wanafunzi wa shule za upili, vyuo vikuu na wafanyikazi. Wao huandika haiku toka sehemu mbalimbali za nchi ya Kenya na kisha kuzituma kwa barua pepe ili wanachama wote waweze kusoma haiku hizo. Kisa na maana, wanachama wote hupokea haiku hizo na kuzisoma na kuchangia kwa kutoa maoni na marekebisho iwapo yatahitajika. Kila mwaka, kikundi hiki huandaa mkutano (Kukai kwa kijapani) mara moja au mbili na wanachama hawa hukutana na kutiana moyo na kushiriki katika majadiliano ya haiku. Pia katika Kukai huwa na shindano la kuandika haiku bora siku hiyo. Shindano hili hujulikana kama GINKOO kwa kiingereza, na washindi hutuzwa zawadi mbalimbali. Kujiunga ni bure na mtu wa aina yoyote anakaribishwa. Wanachama hawafaidiki kifedha bali hupata kuwa marafiki na watu wa mila na tabaka mbalimbali ulimwenguni pote.

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]