Sumaku

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Sumaku yenye umbo la pao

Sumaku ni gimba inayotoa uga sumaku wa kuvuta magimba ya metali kwake au kuyasukuma mbali nayo. Nguvu hii inaitwa uga sumaku haionekani kwa macho lakini inapimwa.


Sumaku asilia na sumaku zinazotengenezwa[hariri | hariri chanzo]

Sumaku asilia ni vipande vya madini ya maginetiti vinavyoweza kuvuta na kushika vitu vya chuma. Kama kipande cha chuma au feleji ya kawaida inashikwa kwa muda fulani na sumaku asilia itaonyesha pia tabia za sumaku. Watu wamejifunza kutumia uwezo wa sumaku na kutengeneza sumaku hasa pamoja na umeme na kutengeneza vifaa vyenye uwezo mkubwa wa kisumaku vinavyotumiwa katika teknolojia mbalimbali.

Vumbi ya chuma juu ya karatasi inajipanga katika mistari maalumu kama sumaku iko chini ya karatasi hii

Tabia za sumaku[hariri | hariri chanzo]

Usumaku ni tabia katika mada inayopatikana kiasili kufuatana na kanuni za fizikia.

  • kila sumaku huwa na ncha mbili zinazoitwa ncha hasi (negativi) na ncha chanya (positivi).
  • kama sumaku mbili zinakaribiana zikitazamana kwa ncha tofauti zinavutana na kukaa pamoja kwa nguvu. Lakini zikikaribiana na kutazamana kwa ncha ileile (zote mbili kwa ncha hasi au ncha chanya) zinasukumana zikikataa kugusana.
  • sumaku ikipitishwa joto inapungua nguvu yake lakini ikipozwa inaongeza nguvu ya kisumaku.
  • kipande cha chuma kinachokuwa kisumaku baada ya kukaa pamoja na sumaku kitapungua nguvu yake ya kisumaku polepole.
  • waya au simu inayopitishwa na umeme huwa na uga sumaku kando lake.
  • kwa kuviringisha waya nje ya chuma sumaku na kupitisha umeme mle nguvu kubwa ya kisumaku inapatikana. Mbinu huu ni msingi wa kutumia sumakuumeme katika mashine nyingi.

Aloi za chuma na feleji huvutana na sumaku. Lakini metali kama shaba, zinki au alumini hazivutwi nazo.

Historia[hariri | hariri chanzo]

Watu wa kale walitambua tayari tabia za sumaku asilia. Kuna ushahidi katika maandiko ya mwanafalsa mgiriki Thales wa Milet; Wagiriki wa kale waliita mawe yenye tabia hii "mawe ya magnesia" kutokana na mji wa Asia Ndogo yalipopatikana. Jina hili lilikuwa msingi wa jina "magnet" linalotumiwa katika lugha nyingi.

Wachina ni watu wa kwanza waliotambua matumizi ya sumaku kwa manufaa ya kibinadamu. Tangu karne ya 11 walitumia sindano ya magnetiti yenye tabia ya kisumaku iliyolea juu ya maji ndani ya dira. Ncha za sindano sumaku huathiriwa na uga sumaku wa dunia na ncha zake zinatazama kaskazini au kusini. Kwa msaada wa dira mabaharia waliweza kuvuka bahari na kulenga pwani la mbali lisiloonekana mara moja bila kupoteza njia.

Wazungu wa Ulaya walibuni mbinu huohuo kidogo baadaye tangu karne ya 12.

1819 profesa Mdenmark Hans Christian Oersted alitambua uhusiano kati ya umeme na usumaku alipoona ya kwamba umeme unaathiri sindano ya dira. Mwingereza Michael Faraday alifuata kwa kutengeneza kifaa kinachozungusha kipitishi umeme kwa sumaku; hii ilikuwa msingi kwa kubuni injini ya umeme iliyotengenezwa na wengine baadaye na 1866 injinia Mjerumani Werner Siemens alitengenea mashine ya kutengeneza umeme iliyoweka msingi kwa mapinduzi ya pili ya viwandani. Leo hii umeme ni nguvu ya kimsingi wa teknolojia ya kisasa.

Kurasa nyingine[hariri | hariri chanzo]