Matendo ya huruma

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Matendo ya Huruma, mchoro wa Msanii wa Alkmaar, Alkmaar, Uholanzi, 1504 hivi.

Matendo ya huruma ni orodha ya shughuli ambazo katika mapokeo ya Ukristo huangaliwa kama hatua za kuonyesha upendo.

Matendo ya huruma katika Injili[hariri | hariri chanzo]

Msingi wake ni hotuba ya Yesu kufuatana na Injili ya Mathayo 25:31-46 ambako aliorodhesha matendo sita yatakayoangaliwa wakati wa hukumu.

Maneno ya Yesu mwenyewe[hariri | hariri chanzo]

31 "Wakati Mwana wa Mtu atakapokuja katika utukufu wake na malaika wote wakiwa pamoja naye, hapo ataketi juu ya kiti chake cha enzi kitukufu,

32 na mataifa yote yatakusanyika mbele yake, naye atawatenganisha watu kama mchungaji anavyotenganisha kondoo na mbuzi.

33 Atawaweka kondoo upande wake wa kulia na mbuzi upande wake wa kushoto.

34 "Kisha Mfalme atawaambia wale walio upande wake wa kulia, `Njoni enyi mliobarikiwa na Baba yangu; pokeeni Ufalme mliotayarishiwa tangu kuumbwa kwa ulimwengu.

35 Maana nilikuwa na njaa nanyi mkanipa chakula; nilikuwa na kiu nanyi mkanipa maji; nilikuwa mgeni nanyi mkanikaribisha;

36 nilikuwa uchi, mkanivika; nilikuwa mgonjwa nanyi mkaja kunitazama; nilikuwa gerezani nanyi mkaja kunitembelea.`

37 Hapo, hao watu wema watamjibu mfalme `Bwana, ni lini tulikuona mwenye njaa nasi tukakupa chakula, au ukiwa na kiu nasi tukakunywesha maji?

38 Ni lini tulikuona ukiwa mgeni nasi tukakukaribisha, au bila nguo nasi tukakuvika?

39 Ni lini tulikuona ukiwa mgonjwa au mfungwa nasi tukaja kukutazama?`

40 Mfalme atawajibu, `Kweli nawaambieni, kila kitu mlichomtendea mmojawapo wa hawa ndugu zangu wadogo, mlinitendea mimi.`

41 "Kisha atawaambia wale walio upande wake wa kushoto, `Ondokeni mbele yangu enyi mliolaaniwa! Nendeni katika moto wa milele aliotayarishiwa Ibilisi na malaika wake.

42 Maana nilikuwa na njaa nanyi hamkunipa chakula; nilikuwa na kiu nanyi hamkunipa maji.

43 Nilikuwa mgeni nanyi hamkunikaribisha; nilikuwa mgonjwa na mfungwa nanyi hamkuja kunitazama.`

44 "Hapo nao watajibu, `Bwana, ni lini tulikuona ukiwa na njaa au kiu, ukiwa mgeni au bila nguo, ukiwa mgonjwa au mfungwa, nasi hatukuja kukuhudumia?`

45 Naye atawajibu, `Nawaambieni kweli, kila mlipokataa kumtendea mambo haya mmojawapo wa hawa wadogo, mlikataa kunitendea mimi.`

46 Basi, hawa watakwenda kwenye adhabu ya milele, lakini wale waadilifu watakwenda kwenye uzima wa milele."

Kutokana na maneno hayo, yaliorodheshwa matendo sita yafuatayo:

  1. Kulisha wenye njaa
  2. Kunywesha wenye kiu
  3. Kukaribisha wageni
  4. Kuvika walio uchi
  5. Kuhudumia wagonjwa
  6. Kutembelea wafungwa

Tangu karne ya nne kazi moja iliongezwa ambayo ni

  • 7. Kuzika wafu [1]

kutokana na mafundisho ya Kitabu cha Tobiti 1:17-20, lakini pia Math 26:6-13 ambapo Yesu alisema, "Mbona mnamsumbua huyu mama? Yeye amenitendea jambo jema. Maskini mnao daima pamoja nanyi, lakini mimi sitakuwapo pamoja nanyi daima. Huyu mama amenimiminia marashi ili kunitayarisha kwa maziko. Nawaambieni kweli, popote ambapo hii Habari Njema itahubiriwa ulimwenguni, kitendo hiki alichofanya mama huyu kitatajwa kwa kumkumbuka yeye."

Matendo saba ya huruma yalifundishwa kama wajibu wa Wakristo kwa karne nyingi. Kuna picha nyingi katika sanaa ya Kikristo zinazoeleza shughuli hizi.

Ni kwamba Yesu aliwaambia wafuasi wake: "Ninyi ni mwanga wa ulimwengu! Mji uliojengwa juu ya mlima hauwezi kufichika. Wala watu hawawashi taa na kuifunika kwa chungu, ila huiweka juu ya kinara ili iwaangazie wote waliomo nyumbani. Vivyo hivyo, ni lazima mwanga wenu uangaze mbele ya watu, ili wayaone matendo yenu mema, wamtukuze Baba yenu aliye mbinguni." (Math 5:14-16)

Mwishoni mwa hiyo Hotuba ya mlimani alifafanua na kusisitiza: "Si kila aniambiaye, `Bwana, Bwana,` ataingia katika Ufalme wa mbinguni; ila ni yule tu anayetimiza mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni. Wengi wataniambia Siku ile ya hukumu: `Bwana, Bwana! kwa jina lako tulitangaza ujumbe wako, na kwa jina lako tuliwatoa pepo na kufanya miujiza mingi.` Hapo nitawaambia: `Sikuwajua ninyi kamwe; ondokeni mbele yangu, enyi watenda maovu.` (Math 7:21-23).

Kinachotakiwa ni hasa huruma: "Heri walio na huruma, maana watahurumiwa". (Math 5:7).

Waraka wa Yakobo, ukiwa kama mwangwi wa hotuba hiyo, unasema: "Maana, Mungu hatakuwa na huruma atakapomhukumu mtu asiyekuwa na huruma. Lakini huruma hushinda hukumu. Ndugu zangu, kuna faida gani mtu kusema ana imani, lakini haonyeshi kwa vitendo? Je, hiyo imani yawezaje kumwokoa? Tuseme kaka au dada hana nguo au chakula. Yafaa kitu gani ninyi kuwaambia hao: "Nendeni salama mkaote moto na kushiba," bila kuwapatia mahitaji yao ya maisha? Vivyo hivyo, imani peke yake bila matendo imekufa. Lakini mtu anaweza kusema: "Wewe unayo imani, mimi ninayo matendo!" Haya! Nionyeshe jinsi mtu anavyoweza kuwa na imani bila matendo, nami nitakuonyesha imani yangu kwa matendo yangu". (Yak 2:13-18).

Matendo ya huruma katika Kanisa Katoliki[hariri | hariri chanzo]

Kanisa Katoliki linasisitiza katika mafundisho yake umuhimu wa matendo kama yale yanayofanyika kutokana na huruma na ambayo Ukristo unawadai waamini, kwa sababu ni lazima aliyepokea huruma ya Mungu awashirikishe wengine kwa kuwahurumia.[2][3][4]

Katika Katekisimu ya Kanisa Katoliki yameorodheshwa katika makundi mawili: 7 ya kimwili (yaliyosisitizwa na Yesu alipodokeza hukumu ya mwisho, likiongezwa la kuzika wafu[5][6]) na 7 ya kiroho, kadiri yanavyolenga faida ya binadamu upande wa mwili au upande wa roho kwanza.[5][6][7]

Matendo ya huruma ya kimwili[hariri | hariri chanzo]

  1. Kulisha wenye njaa
  2. Kunywesha wenye kiu
  3. Kuvika walio uchi
  4. Kukaribisha wageni
  5. Kuhudumia wagonjwa
  6. Kutembelea wafunga
  7. Kuzika wafu

Matendo ya huruma ya kiroho[hariri | hariri chanzo]

  1. Kuelimisha wajinga
  2. Kushauri wenye shaka
  3. Kuonya wakosefu
  4. Kuvumilia wasumbufu
  5. Kusamehe kwa moyo
  6. Kufariji wenye huzuni
  7. Kuwaombea wazima na wafu[6]

Tanbihi[hariri | hariri chanzo]

  1. Hatua hii imetokana na maandiko ya Babu wa Kanisa Laktansio (250325 BK)
  2. Pope John Paul II, Dives in misericordia, §14, Libreria Editrice Vaticana, November 30, 1980
  3. John Stephen Bowden. Encyclopedia of Chrl=http://books.google.com/books?id=NGAUAQAAIAAJ&q=works+of+mercy+methodism&dq=works+of+mercy+methodism&hl=en&ei=FT0TTrqAO4jl0QHH_dS-Dg&sa=X&oi=book_result&ct=result&resnum=6&ved=0CEMQ6AEwBQ. Oxford University Press. Works of mercy are, therefore, not merely good deeds but also channels through which Christians receive God's grace.  Check date values in: |accessdate= (help);
  4. John Wesley. The Works of the Reverend John Wesley, A.M., Volume VI. J. Emory & B. Waugh; J. Collord, New York. uk. 46. Iliwekwa mnamo 5 July 2011. Why, that both repentance, rightly understood, and the practice of all good works, — works of piety, as well as works of mercy, (now properly so called, since they spring from faith,) are, in some sense, necessary to sanctification.  Check date values in: |accessdate= (help)
  5. 5.0 5.1 The works of mercy by James F. Keenan 2004 ISBN 0-7425-3220-8 pages 9-12
  6. 6.0 6.1 6.2 Catholic encyclopedia: Corporal and Spiritual Works of Mercy
  7. Mercies Remembered by Matthew R Mauriello 2011 ISBN 1-61215-005-5 page 149-160

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]

Wikimedia Commons ina media kuhusu:
Makala hii kuhusu dini ya Ukristo bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Matendo ya huruma kama historia yake, matokeo au athari zake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.