Wimbi

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru

Kwa nafaka inayoitwa wimbi tazama wimbi

Mawimbi madogo hutokea baada ya kutupa jiwe kwenye bwawa

Wimbi kwa lugha ya kawaida ni mwendo unaonekana kwenye uso wa maji tukitembea ufukoni mwa bahari. Kwa lugha ya fizikia wimbi halihusu maji pekee bali ni jambo linaloweza kutokea katika kila kitu.

Mfano wa wimbi katika maji[hariri | hariri chanzo]

Tukiweka maji katika bakuli na kupuliza juu yake tunaona mwendo uleule kama ufukoni, yaani tunaona mawimbi madogo. Nishati ya pumzi tunalopuliza juu ya uso wa maji katika bakuli inaanzisha mbembeo wa uso wa maji unaoendelea. Nguvu hii inasababisha vurugo endelevu inayopanuka katika maji. Mwendo wa wimbi unapeleka nishati kutoka mahali pamoja kwende mahali pengine bila kusukuma maji yenyewe.

Mawimbi ya aina nyingi[hariri | hariri chanzo]

Kwa maana hii wimbi ni vurugo endelevu au mbembeo unaopanuka katika mata au kwenye uga ya nishati. Mawimbi ya bahari kwenye ufuko yanaweza kutokana na dhoruba iliyopuliza maji kilomita elfu kadhaa kutoka mahali tunapoyaona. Kwa hiyo kimsingi kila wimbi ni mwendo wa nishati (si ya mata) unaoendelea kwa njia ya mtetemo au mbembeo. Lakini mawimbi ya maji ni sehemu ndogo tu ya mawimbi kwa jumla.

Aina nyingine ya wimbi ni nuru na wimbisauti. Halafu kuna mawimbi mengine yasiyoonekana kwetu, maana hatuna milango ya fahamu kwake. Lakini zimegunduliwa na sayansi ya kisasa na kutumiwa kwa njia ya teknolojia mbalimbali.

Kimsingi wataalamu wametofautisha aina mbili ambayo ni mawimbi ya mata, yanayoitwa pia wimbi makanika (mechanic wave) na ambayo yanahitaji midia kama kiowevu, gesi au mata manga. Kati ya hizi ni wimbosauti, mawimbi katika maji, mawimbi ya tetemeko.

Aina nyingine ya mawimbi zinapita pia katika ombwe (vacuum) pasipo mata na hizi ni hasa mawimbi sumakuumeme. Haya ni pamoja na nuru inayoonekana, infraredi, eksirei na wimbiredio.

Wimbi: Masafa ya mawimbi (wavelength) na tambo (amplitude)

Tabia za wimbi[hariri | hariri chanzo]

Mawimbi huwa na tabia zinazopimika. Hizi ni pamoja na tambo (amplitude), urefu wa wimbi (wavelength), marudio (frequency), fezi (phase) na velositi ya fezi.

Tambo huwa na sehemu ya kilele (fyulisi) na ya bonde (bohori). Mstari unaopita katikati ya kilele na bonde ya wimbi ni mstari anzio (baseline).

Mawimbi ya sumakuumeme hupangwa katika spektra kutokana na tabia hizi za masafa na marudio ya mawimbi.

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]

WikiMedia Commons
WikiMedia Commons
Wikimedia Commons ina media kuhusu:
Simple English Wiktionary
Simple English Wiktionary
Wikamusi ya Kiswahili ina maelezo na tafsiri ya maana ya neno: