Vita baridi

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Pande mbili za vita baridi katika Ulaya: washiriki wa Marekani (buluu) na wa Umoja wa Kisovyeti (nyekundu)

Vita baridi ilikuwa kipindi cha ugomvi kati ya makundi mawili ya nchi duniani miaka 1945 - 1989. Upande mmoja zilikuwa nchi zilizoshikama na Marekani: kati ya nchi hizo, nyingi zilikuwa ni za Ulaya Magharibi ambazo zilishikana na Umoja wa Kujihami uliojulikana kama NATO. Upande mwingine nchi zilizoshikamana na Umoja wa Kisovyeti na madola ya Ulaya ya Mashariki.

Vita baridi badala ya vita moto[hariri | hariri chanzo]

Pande zote mbili ziliunda majeshi makubwa na kuwa na silaha nyingi, lakini hazikuanzisha vita moja kwa moja, ila zilijaribu kutishana na kupeana matatizo kwa njia nyingi. Kipindi hiki kilikuwa na maandalizi ya vita lakini vita vya kijeshi havikuanza. Sababu muhimu ya kutoingia katika mapigano ya wazi ilikuwa akiba kubwa ya silaha za nyuklia kila upande na wote walijua ya kwamba vita vingeleta uharibifu mkubwa kabisa kwa nchi zote zilizoshiriki, hata kwa dunia yote.

Chanzo kilikuwa farakano kati ya washindi wa Vita Kuu ya Pili ya Dunia[hariri | hariri chanzo]

Vita baridi vilianza baada ya vita kuu ya pili ya dunia. Marekani, Uingereza na Ufaransa zilikuwa nchi washindi wa vita hii dhidi ya Ujerumani. Urusi ulikuwa na siasa ya kikomunisti lakini washindi wengine walifuata siasa ya kidemokrasia pamoja na uchumi wa kibepari. Ikumbukwe kuwa, Urusi ilijitoa kwenye vita vya kwanza vya dunia baada ya kufanya mapinduzi ya Kikomunisti mwaka 1917 hivyo kuachana na ushiriki wa vita hivyo vya mabepari.

Nchi za Ulaya ya Mashariki pamoja na sehemu za Ulaya ya Kati zilikaliwa na jeshi la Kisovyeti lililowahi kuwafukuza Wajerumani katika maeneo haya. Wasovyeti walianza kuunda serikali zilizoshikamana nao mara nyingi kwa njia ya uchaguzi bandia na kwa kuwalazimisha wanasiasa wa nchi kama Poland, Chekoslovakia au Hungaria kutii madai yao. Wapinzani walikamatwa na kufungwa. Katika kila nchi chama cha kikomunisti kiliingizwa katika serikali na vyama vingine vya kisiasa kuwekwa chini ya usimamizi wa Wakomunisti au washauri Wasovyeti. Mwaka 1946 kiongozi Mwingereza Winston Churchill alilalamika ya kwamba "pazia la chuma" ilitandikwa katika Ulaya kuanzia Stettin upande wa kaskazini hadi Trieste upande wa kusini na nyuma yake uhuru ulikandamizwa.

Viongozi wa nchi za magharibi waliona maendeleo yale kama tishio hata kwa nchi zao ambako vyama vya kikomunisti vililenga pia kushika utawala lakini kwa jumla zilishindwa bila usaidizi wa kijeshi jinsi ilivyokuwa upande wa mashariki. Hapa nchi za Ulaya ya Magharibi zilishikamana pamoja kuzuia uenezaji wa enzi ya Kisovyeti katika nchi zao.

Uhusiano mbaya ulianza mara baada ya ushindi ukaonekana kabisa miaka 1948-1949 ambapo Wasovyeti walijaribu kuwalazimisha Wamarekani na wenzao kuondoka katika Berlin ya Magharibi kwa kufunga barabara zote zlizounganisha mji huo na Ujerumani ya Magharibi na kuzuia vyakula visifike mjini tena. Marekani iliweza kulisha wakazi kwa njia ya daraja la angani na ndege zilileta bidhaa.

Kabla ya tukio hili majaribio la Umoja wa Kisovyeti la kupanua upeo wake kwa kusaidia wanamgambo wakomunisti katika Ugiriki na Uajemi kuanzia 1946 yalileta uchungu. Sababu nyingine za kuunda wasiwasi zilikuwa majaribio ya majasusi Warusi waliotafuta siri za silaha za kinyuklia za Marekani.

Ukuta wa Berlin ilikuwa kielelezo cha pazia la chuma katika Ulaya.

NATO na Mapatano ya Warshawa[hariri | hariri chanzo]

Nchi za Magharibi ziliunda mwungano wa kijeshi wa NATO (North Atlantic Treaty Organization) wakiahidi kushikamana kama nchi yoyote ingeshambuliwa kutoka nje.

Wasovyeti walijibu kwa kuunganisha nchi zilizokuwa chini ya usimamizi wao katika Mapatano ya Warshawa.

Maungano haya ya kijeshi yalifuatwa na mapatano ya kiuchumi kila upande.

Nchi zilizoanzisha NATO zilikuwa: Marekani, Uingereza, Ufaransa, Italia, Ureno, Uholanzi, Ubelgiji, Luxemburg, Norwei, Denmark, Iceland, Austria na Kanada. Mwaka 1954 Ujerumani ya Magharibi ilipokewa pia. Uturuki na Ugiriki zilijiunga pia.

Nchi za Mapatano ya Warshawa zilikuwa: Umoja wa Kisoveti, Albania, Bulgaria, Poland, Romania, Chekoslovakia, Hungaria na Ujerumani ya Mashariki.

Kila upande ulikuwa na nchi mbalimbali zilizoshirikiana nao bila kijiunga rasmi na mapatano yale. Umoja wa Kisoveti ilishikamana na Kuba, China, Korea ya Kaskazini na Mongolia. Marekani iliendelea kuwa na mapatano ya kijeshi na nchi nyingi kama Uajemi, Pakistan na Taiwan.

Makombora maelfu kama SS20 hii ya kisovyeti yalikuwa tayari kurusha mabomu ya kinyuklia.

Tishio la vita vya nyuklia[hariri | hariri chanzo]

Mwaka 1945 Marekani ilikuwa nchi pekee duniani yenye silaha za nyuklia. Lakini Umoja wa Kisovyeti iliweza kufuata na mwaka 1949 ikalipua bomu la nyuklia.

Kila upande uliendelea kutengeneza akiba kubwa ya silaha hizi. Hadi miaka ya 1980 idadi ya silaha hizo ilitosha kuharibu uhai wote duniani mara kadhaa.

Viongozi wa kijeshi na wa kisiasa walijua ya kwamba kulikuwa na uwezo wa kuharibu kabisa maadui. Lakini walijua pia ya kwamba hata maadui wale walikuwa na uwezo huohuo na kila mmoja alijiandaa kabisa kurusha mabomu mengi kabla ya kufa mwenyewe.

Kwa njia hii hofu ya kifo cha kinyuklia ilizuia kuanzishwa kwa vita moto kati ya pande mbili.

Lakini hofu hii haikuzuia vita katika nchi mbalimbali ambako Wasovyeti na Marekani walisaidia upande mmoja dhidi ya marafiki wa upande mwingine. Mifano ya vita hivyo ni Vita ya Korea na Vita ya Vietnam au pia vita mbalimbali katika Afrika.

Athira ya vita baridi duniani mnamo mwaka 1980
Buluu neusi: Nchi za NATO
Buluu nyeupe:Nchi zilikuwa na mapatano ya kijeshi na Marekani
Nyekundu kali: Nchi za mapatano ya Warshawa
Nyekundu wastani: Nchi za kisoshalisti zenye makubaliano nao
Nyekundu nyeupe:Mchi zenye mapatanao mengine na Umoja wa Kisovyeti;
Kijivu: Nchi zisizofungamana na upande wowote

Athira ya vita baridi katika Afrika[hariri | hariri chanzo]

Maendeleo ya Afrika yaliathiriwa pia na vita baridi. Kwa jumla kila upande ulijaribu kuvuta nchi changa za Afrika upande wake. Kama serikali ilipatana na upande mmoja, upande mwingine mara nyingi ulikuwa tayari kusaidia wapinzani wa ndani kwa msaada wa silaha na pesa.

Wapigania uhuru katika makoloni ya Ureno kama Msumbiji au Angola walipata msaada wa silaha na pesa kutoka nchi za mashariki kwa sababu Ureno ilikuwa nchi ya NATO. Wapinzani hao walitazamwa na magharibi kama Wakomunisti na mawakala wa Wasovyeti, hivyo Marekani ilisaidia Afrika Kusini ingawa siasa ya ubaguzi wa rangi ilivunja haki za binadamu.

Madikteta wengi wa Afrika walipata usaidizi wa upande mmoja au mwingine wakitangaza tu kushikamana nao. Serikali ya Mobutu Sese Seko katika Kongo ilisaidiwa na nchi za magharibi kwa sababu Mobutu alijitangaza kama adui wa Ukomunisti. Haile Mengistu Mariam wa Ethiopia alipata silaha na washauri kutoka upande wa mashariki na polisi ya siri ya Ujerumani ya Mashariki ilitoa ushauri kwa wapelelezi wa Ethiopia jinsi ya kutafuta wapinzani wa ndani.

Hata kama serikali fulani ya Afrika iliharibu uchumi na kuvunja haki za binadamu iliweza kutegemea usaidizi kutoka kwa upande mmoja wa vita baridi ikijitangaza iko upande wake. Siad Barre alikuwa na mapatano na Umoja wa Kisovyeti hivyo Somalia ilihesabiwa kati ya nchi za upande wa Kikomunisti. Baada ya Ethiopia kupatana na Wasovyeti pia tangu mwaka 1974, Somalia iliyokuwa na fitina na jirani yake kuhusu eneo la Ogaden ilihamia upande wa Marekani ikasaidiwa nayo.

Viongozi mbalimbali waliopigania uhuru walipata kimbilio katika nchi za mashariki wakapata nafasi ya kusoma na kujifunza matumizi ya silaha. Hii ilikuwa sababu moja kwa nini wengi walielekea itikadi ya Usoshalisti na kujaribu mbinu za kisiasa na kiuchumi kufuatana na mfano wa Wakomunisti wa Ulaya hata kama siasa yao haikuwa na matokeo mazuri kwao nyumbani.

Mwisho 1989[hariri | hariri chanzo]

Mashindano ya kuongeza silaha mpya yalishinda uwezo wa uchumi wa nchi za kikomunisti. Katika miaka ya 1970 ilionekana ya kwamba uchumi wao ulibaki nyuma. Teknolojia mpya hazikuenea kwa sababu utawala wa kidikteta ulijaribu kusimamia mawasiliano yote kwa njia ya polisi na maendeleo yalikwama. Uchumi ulioongozwa na serikali haukuweza kushindana na nguvu ya ubepari.

Umoja wa Kisovyeti ulitia nguvu jeshi na maendeleo ya silaha lakini uwezo wa kiuchumi haukutosha.

Katika miaka ya 1980 ilionekana ya kwamba nchi za mashariki zilibaki nyuma sana. Katika nchi kadhaa wananchi walidai haki za binadamu. Poland iliona harakati ya wafanyakazi waliokataa uongozi wa Wakomunisti wakaanzisha chama cha Solidarnocz na kusababisha utawala wa kijeshi badala ya chama.

Michael Gorbachov wa Umoja wa Kisovyeti na rais Ronald Reagan wa Marekani wakitia sahihi mapatano ya kupunguza silaha za kinyuklia mwaka 1997.

Kiongozi mpya wa Umoja wa Kisovyeti Mikhail Gorbachov alielewa hatari ya kuporomoka kwa uchumi wake akatafuta uelewano na Marekani ili kupunguza gharama za jeshi. Siasa mpya ya glasnost iliruhusu kutoa maoni mbalimbali ikaruhusu pia kiwango fulani cha upinzani dhidi ya viongozi. Gorbachov aliamua kutotisha tena nchi zilizoshikamana na Umoja wa Kisovyeti kwa mashambulio ya kijeshi jinsi ilivyokuwa awali.

Hapo nguvu za upinzani zilipata kipaumbele katika nchi kama Hungaria na Poland na viongozi wapya walielekea kuongeza haki za kidemokrasia wakakubali vyama vipya na magazeti huru. Mwaka 1989 wananchi wa Ujerumani ya Mashariki walianza kuandamana wakalazimisha uongozi wa chama cha Kikomunisti kujiuzulu na viongozi wapya walifungua ukuta wa Berlin uliowahi kutenganisha pande mbili za mji huu kwa miaka 38.

Anguko la ukuta wa Berlin lilikuwa dalili ya mwisho wa vita baridi na pia utawala wa Kikomunisti katika nchi za Ulaya. Kote katika nchi za Kikomunistis serikali ilianguka na viongozi wapya walichaguiwa na wananachi.