Verdiana Masanja

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Verdiana Masanja
Amezaliwa12 Oktoba 1954
UtaifaMtanzania
Majina mengineVerdiana Grace Kashaga
MhitimuChuo Kikuu Cha Dar es Salaam Tanzania, Chuo Kikuu cha Ufundi Cha Berlin, Ujerumani
Kazi yakeProfesa wa Hisabati na Mtafiti
MwenzaHayati Kephas Moses Daniel Masanja
WatotoAngela Carolyn Masanja, Moses Kephas Masanja, Julitha Kephas Masanja-Lusinde, Rabina Kephas Masanja

Verdiana Grace Masanja (alizaliwa mjini Bukoba, nchini Tanzania, 12 Oktoba 1954)[1] ni mwanahisabati na mwanamke wa kwanza Mtanzania kupata shahada ya uzamivu katika Hisabati.

Tangu mwaka 2018 ni profesa wa hisabati kwenye Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela huko Arusha, Tanzania.

Profesa Masanja pia anajulikana kwa kushiriki katika kuinua somo la hisaabati kwa ujumla wake, kuinua masomo ya sayansi, teknolojia, uhandisi na hisabati kwa ujumla wake na hususan kwa mtoto wa kike.

Maisha ya awali[hariri | hariri chanzo]

Verdian Grace Masanja alizaliwa na Mzee Gaspar Lwehumbiza Kalaiti bin Ibrahim Kashaga wa Buhembe Bulibata mjini Bukoba na Bi Julitha Mkaruganyirwa Kalishemela binti wa Arcrad Kasabila wa Nshambya mjini Bukoba, Kaskazini Magharibi mwa Ziwa Victoria, Tanzania karibu na Uganda. Wakati alipozaliwa, Tanzania bara iliitwa Tanganyika Territory ambayo ilikwa chini ya utawala wa Uingereza kama eneo lindwa chini ya mamlaka ya umoja wa mataifa (United Nations Trust Territory under British administration) [2][3]. Ubini wa Masanja aliuchukua baada ya kuolewa na hayati Kephas Moses Daniel Masanja.

Elimu[hariri | hariri chanzo]

Masanja alipata elimu ya msingi katika shule ya awali Nshambya na shule ya msingi Ihungo (darasa la kwanza hadi la nne) zote ziko Bukoba mjini, na shule ya msingi ya kati (middle Primary School) Nyakabungo (sasa inaitwa Milongo) jijini Mwanza. Aliendelea na elimu ya sekondari kwenye shule za sekondari za Chopra (kwa sasa Mwanza) na Rosary (kwa sasa Ngaza), zote zikiwemo jijini Mwanza[4]. Anasemekana kuongoza kwa ufaulu darasani, na alipewa jina la Imani "jike dume". Alipata elimu ya sekondari ya juu Jangwani High School jijini Dar es Salaam. Baada ya hapo, alijiunga na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kwa masomo ya shahada ya kwanza ya hisabati na fizikia ambapo alimaliza mwaka 1976. Tasnifu ya shada ya uzamili iliandikwa chini ya Kichwa Effect of Injection on Developing Laminar Flow of Reiner-Philippoff Fluids in a Circular Pipe[5].

Prof. Verdiana Masanja Akielekezwa jambo wakati wa Warsha ya Astronomia


Baada ya shahada ya uzamili, aliendelea na masomo katika Chuo Kikuu cha Ufundi Berlin, Ujerumani (wakati huo Ujerumani Magharibi), ambapo alipokea shahada ya uzamivu mnamo mwaka wa 1986 na kuandika tasnifu yenye kichwa A numerical study of a Reiner-Rivlin Fluid in an axi-symmetrical circular pipe[6].

Kazi[hariri | hariri chanzo]

Verdina Grace Masanja aliajiriwa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kama msaidizi wa mafunzo (tutorial assistant) baada ya kumaliza shahada ya kwanza tarehe 26 April 1976 an alisaidi waadhiri kwenye hisabati kwa wanafunzi wa Uhadisi (Engineering Mathematics). Alipanda ngazi na kuwa mhadhiri msaidizi tarehe 1 Julai 1978 na alipomaliza alipomaliza shahada ya kwanza na alianza kufundisha hisabati kwa wanafunzi wa shahada ya kwanza wa programu za hisabati, jiolojia na kemia. Alipomaliza shahada ya uzamivu nchini Ujerumani alipanda cheo kuwa mhadhiri. Alifundisha kozi za hesabu kwa wanafunzi wa shahada ka kwanza, uzamivu na uzamili. Pia alisimamia wanafunzi wa shahada za uzamili na uzamivu kwenye tafiti na tasnifu zao[7]. Aliwahi kuongoza idara ya hisabati ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam tangu mwaka 1994 hadi 2000 [8]. Akiwa mwajiriwa wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, alipanda ngazi kufikia Profesa Mwandamizi tarehe 1 Julai 2000. Aliondoka kwenda Rwanda 2006 lakini alibakia kuwa mwajiriwa wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam hadi Desemba 2010.

Tangu mwaka 2006 hadi Desemba 2015, aliajiriwa na Chuo Kikuu cha Rwanda kama Profesa kamili wa hisabati na alifundisha na kushiriki uongozi, ambapo mwaka 2007 aliteuliwa kuwa mkurugenzi wa kitengo cha utafiti mwenye uwajibikaji wa elimu ya uzamili na uzamivu, utafiti, na ushauri. Januari 2016 hadi Oktoba 2017 aliteuliwa kuwa mshauri mwandamizi (sawa na makamu mkuu wa chuo) mwenye uwajibikaji wa mikakati-maendeleo, utafiti na uvumbuzi kwenye Chuo Kikuu cha Kibungo, nchini Rwanda[9].

Mwaka 2018, aliajiriwa kama profesa kamili wa hisabati Shule Kuu ya Ukokotoaji na mawasliano ya sayansi na uhandisi ya Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela[10].

Nje ya kazi, Verdiana Grace Masanja hujishughulisha na kukuza elimu ya hisabati na sayansi kwa ujumla na hususan kwa wasichana na wanawake nchini Tanzania na katika Afrika kwa ujumla.

Kujihusisha na miradi ya elimu[hariri | hariri chanzo]

Aliwahi kushiriki warsha ya Astronomia akiwa kama muelimishaji wa maswala mbalimbali.

Marejeo[hariri | hariri chanzo]

  1. http://mathshistory.st-andrews.ac.uk/Biographies/Masanja.html, iliangaliwa tar. 9 April 2020
  2. http://mathshistory.st-andrews.ac.uk/Biographies/Masanja.html, iliangaliwa tar. 9 April 2020
  3. African Doctorates in Mathematics: A Catalogue, uk. 718, iliangaliwa kupitia google books tar. 1. Desemba 2018
  4. http://mathshistory.st-andrews.ac.uk/Biographies/Masanja.html, iliangaliwa tar. 9 April 2020
  5. http://mathshistory.st-andrews.ac.uk/Biographies/Masanja.html, iliangaliwa tar. 9 April 2020
  6. Verdiana Grace Masanja kwenye tovuti ya Mathematics Genealogy Project ya North Dakota State University, Marekani, iliangaliwa Desemba 2018
  7. http://mathshistory.st-andrews.ac.uk/Biographies/Masanja.html, iliangaliwa tar. 9 April 2020
  8. L.H. Riddle, makala "Verdiana Grace Masanja" katika Biographies of Women Mathematicians, kwenye tovuti ya Agnes Scott College, Memphis, Marekani
  9. http://mathshistory.st-andrews.ac.uk/Biographies/Masanja.html, iliangaliwa tar. 9 April 2020
  10. http://mathshistory.st-andrews.ac.uk/Biographies/Masanja.html, iliangaliwa tar. 9 April 2020

Viungo vya Nje[hariri | hariri chanzo]

Makala hii kuhusu mtu huyo bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Verdiana Masanja kama wasifu wake, habari za maisha au kazi yake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.