Uga sumaku wa Dunia

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Uga sumaku wa Dunia katika uigaji wa kompyuta. Mistari inaonyesha mistari ya uga sumaku, ya buluu pale ambako uga sumaku unaelekea kitovu cha Dunia, njano pale ambako inaelekea mbali na kitovu. Mistari mingi ya karibu iko kwenye kiini cha Dunia

Uga sumaku wa Dunia (kwa Kiingereza: geomagnetic field, Earth's magnetic field) ni uga sumaku ambao unazunguka Dunia. Unaenea kuanzia kiini cha Dunia hadi anga-nje unapoathiriana na upepo wa Jua (mkondo wa chembe zenye chaji kutoka Jua). Ugasumaku wa Dunia unakinga uhai duniani dhidi ya mnururisho haribifu kutoka anga-nje

Uga sumaku wa Dunia unaundwa na mzunguko wa Dunia; mzunguko huo unasababisha mikondo ya umeme kutokea kwenye kiini cha Dunia ambako joto la ndani linatoka nje.[1] Uga sumaku huo si wa kudumu ukijulikana umeshabadilika mara kadhaa katika historia ya Dunia.[2]

Uga sumaku wa Dunia huwa na ncha sumaku zinazopatikana karibu na ncha za kijiografia za Dunia. Ncha sumaku huhama mara kwa mara; kwenye mwaka 2007 ncha sumaku ya kaskazini ilikuwa na umbali wa km 960 kutoka ncha ya kijiografia ikiendelea kuhama takriban kilomita 50 kila mwaka[3]. Dira hutumia uga sumaku huo kudokeza nchani, lakini ilhali kuna tofauti kati ya ncha sumaku ya kaskazini na ncha ya kijiografia ya kaskazini ni lazima kujua tofauti hiyo kwa mwongozo wa safari za meli au ndege.

Kinga ya uhai[hariri | hariri chanzo]

Uga sumaku wa Dunia unakengeusha upepo wa Jua ambao ni mkondo vya chembe kutoka Jua. Kama upepo wa Jua ungeweza kupiga angahewa moja kwa moja ungeondoa tabaka la ozoni linalozuia mnururisho haribifu wa urujuanimno kufika kwenye uso wa ardhi[4]. Utafiti wa sayari ya Mirihi umeonyesha kwamba kupotea kwa uga sumaku wa sayari hiyo kulisababisha kupotea kwa gesi karibu zote za angahewa ya Mirihi[5].

Duniani uga sumaku wake unashika chembe hizo katika eneo la Ukanda wa Van Allen ambako vinazunguka sayari yetu kwa umbali wa kilomita 700 au zaidi bila kupiga uso wa Dunia.

Tanbihi[hariri | hariri chanzo]

  1. Zvereva T.I. (2012). "Motion of the Earth's magnetic poles in the last decade". Geomagnetism and Aeronomy 52 (2): 278–286. 
  2. Dergachev V.A. et al. (2012). "Impact of the geomagnetic field and solar radiation on climate change". Geomagnetism and Aeronomy 52 (8): 959–976. 
  3. L. R. Newitt, A. Chulliat, and J.-J. Orgeval, Location of the North Magnetic Pole in April 2007 Archived 5 Agosti 2020 at the Wayback Machine., Earth Planets Space, 61, 703–710, 2009
  4. Shlermeler, Quirin (3 March 2005). "Solar wind hammers the ozone layer". News@nature. doi:10.1038/news050228-12. 
  5. "Solar wind ripping chunks off Mars", Cosmos Online, 25 November 2008. Retrieved on 21 October 2013. Archived from the original on 4 March 2016. 
Makala hii kuhusu mambo ya sayansi bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Uga sumaku wa Dunia kama historia yake au mahusiano yake na mada nyingine?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.