Saturnus

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Sanamu hii ya Saturnus imepatikana katika Tunisia yaonyeshwa katika makumbusho ya Bardo

Saturnus ni jina la mungu mmojawapo aliyeabudiwa katika Roma ya Kale. Aliaminiwa kuwa mungu aliyehusika mambo ya kilimo na mavuno. Alitolewa sadaka kwa ajili ya kustawi kwa mazao.

Waroma wa Kale walitumia kuhusu Saturnus masimulizi waliopokea kutoka kwa Wagiriki ilhali walimwona kama jina mbadala kwa mungu wa Kigiriki Kronos; huyu alikuwa mwana wa mungu wa mbingu Urano na mungu wa kike wa ardhi Gaia. Alimpindua babake kwa kukata uume wake. Baadaye alihofia ya kwamba watoto wake watampindua vile hivyo alikula watoto wake wote isipokuwa mwana wa sita Jupiter alifichwa mbele yake. Saturnus alipaswa kukimbia akafikia Italia alipowafundisha wenyeji elimu ya kilimo.

Sikukuu ya Saturnus iliitwa "Saturnalia" ni siku kadhaa kuanzia 17 Desemba zilizokuwa sherehe kubwa huko Roma.

Alama yake angani ilikuwa sayari ya sita yaani Zohali inayoitwa hadi leo kwa jina la "Saturn" katika lugha za Ulaya.

Siku ya Jumamosi huitwa "siku ya Saturnus" yaani Saturday hadi leo kwa Kiingereza na Kiholanzi.