Ranavalona I

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Ranavalona I, malkia 1828-1861

Malkia Ranavalona I wa Wamerina alikuwa binamu na mke wa kwanza wa mfalme Radama I, akatawala baada ya kifo cha mume wake (1828) hadi kifo chake mwenyewe (1861).

Kwa kuwa alisaidiwa kupata umalkia na makabila na wakuu wa majeshi ambao Radama aliwaondoa madarakani katika harakati zake za kukijenga kisiwa hicho upya, washauri wake walikuwa watu waliozipinga sera muhimu za mfalme aliyefariki.

Mkazo wa sera za Ranavolona ulikuwa kuulinda uhuru wa Bukini dhidi ya athari za kigeni, hasa zile zilizoathiri asasi za kitaifa, mila na desturi. Kuhusu sera ya mambo ya nje, aliegemea zaidi katika kuitoa nchi yake kutoka kwenye athari za Waingereza, hasa katika nyanja za siasa na dini.

Malkia Ranavalona aliendelea na upanuzi ambao Radama I aliuanzisha na kuuimarisha utawala wake katika majimbo aliyoyateka. Kabila la Wasakalava liliendelea kuupinga utawala wake.

Hatimaye majeshi ya serikali yalipowashinda machifu wa Sakalava, walikimbia na watu wao na kwenda kwenye visiwa vya jirani ambapo walijiweka kwenye hifadhi ya Wafaransa. Hali hiyo baadaye ilikuwa ndiyo msingi wa madai ya Wafaransa kwa majimbo yaliyoko magharibi mwa Bukini.

Utawala wake unaweza kuelezwa katika namna mbili. Kwa upande mmoja, ulikuwa ni utawala wenye vitisho kwa wamisionari na watu wengine waliotekwa na kuwa chini ya utawala wa Kimerina. Kwa upande mwingine, ulikuwa kipindi cha maendeleo makubwa ya viwanda, na ambacho kiliimarisha elimu ya Kizungu na kuiweka nchi katika mwelekeo wa usasa.

Kwa jumla, kwa raia zake wengi, Ranavalona alikuwa ishara ya utaifa wa Kimalagasi.

Ranavalona alifariki mwaka 1861 baada ya kumtangaza Rakoto Radama kuwa ndiye atakayetawala baada yake.

Makala hii kuhusu mwanasiasa fulani bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Ranavalona I kama wasifu wake, habari za maisha au kazi yake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.