Papa Gregori VII

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Mt. Gregori VII

Papa Gregori VII, O.S.B. (Soana, Toscana, 1020 hivi – Salerno, Campania, 25 Mei 1085) alikuwa Papa kuanzia tarehe 22 Aprili au 30 Juni 1073 hadi kifo chake ugenini[1].

Jina lake la kuzaliwa lilikuwa Ildebrando[2].

Alimfuata Papa Aleksanda II akafuatwa na Papa Vikta III.

Alitangazwa na Papa Gregori XIII kuwa mwenye heri (1584), halafu (1728) kuwa mtakatifu na Papa Benedikto XIII.

Sikukuu yake huadhimishwa tarehe ya kifo chake[3].

Maisha[hariri | hariri chanzo]

Baada ya kuishi kama mmonaki wa Kibenedikto alichangia sana urekebisho wa Kanisa kama kardinali na balozi wa Papa.

Kisha kuchaguliwa mwenyewe kuwa Papa alipigania kwa nguvu zote utakatifu wa ukuhani na uhuru wa Kanisa Katoliki dhidi ya mamlaka ya serikali, akifungua njia kwa Mapapa waliofuata. Ni kwamba wakati huohuo kaizari Heinrich IV wa Ujerumani aliwahi kumsimika askofu mmoja nchini Ujerumani kufuatana na desturi ya huko. Kumbe Papa aliona haki yake ya kuteua maaskofu imeingiliwa, hivyo akatafuta na kupata tamko la wakubwa wa Kanisa huko Italia, kuwa washauri wa mfalme watengwe na Kanisa.

Mfalme alikasirika akaita maaskofu wa Ujerumani waliamua Papa huyo asiwe Papa tena. [4] Wakati Gregori VII aliposikia hayo alimtenga Heinrich IV na Kanisa, alitangaza kuwa hakuwa mfalme tena akafuta viapo ambavyo watu walikuwa wamemwapia mfalme.

Kutengwa kwa mfalme kulisababisha hisia kali huko Ujerumani na Italia. Babu wa mfalme Henry III aliwahi kuwaondoa mamlakani Mapapa watatu, lakini wakati Henry IV alipojaribu kuiga mfano huo, hakuungwa mkono na watu.

Hali ikawa mbaya sana kwa mfalme. Papa alimtenga mfalme katika Kanisa. Alipiga marufuku askofu au padre yeyote kumruhusu katika ibada au kumhudumia kwa namna yoyote. Ilibainika kuwa ilibidi apate msamaha kutoka kwa Papa. Mwanzoni alijaribu kufanya hivyo kwa kutuma balozi. Baada ya Papa kumkataa balozi huyo, mfalme alikwenda Italia mwenyewe.

Alimkuta Papa huko Canossa akapiga magoti mbele ya ngome ya Papa na kuomba msamaha. Kwa kuonyesha unyenyekevu vile alimfanya Papa kumsamehe na kumrudisha katika jumuiya ya Kanisa.

Wakubwa huko Ujerumani waliwahi kutumia nafasi ya kutengwa kwa mfalme kanisani ili kumtangaza mfalme mpinzani. Papa aliamua kumuunga mkono huyo mfalme wa upinzani akamtenga Heinrich upya mwaka 1080.

Lakini baada ya miezi michache yule mfalme mpinzani alifariki dunia, hivyo Heinrich alianza kupigania upya kuwa mfalme.

Mnamo 1081 alianzisha vita dhidi ya Papa Gregori VII nchini Italia. Aliitisha mkutano wa maaskofu waliomwunga mkono na mkutano huo ulitangaza kufukuzwa kwa Papa Gregori wakamchagau Antipapa. Jeshi la mfalme Heinrich liliingia Roma mnamo mwaka 1084, kumtangaza papa mpya aliyeweka taji la ukaizari kwenye kichwa cha mfalme.

Hatimaye mfalme alipaswa kuondoka Roma tena, Papa Gregori aliaga dunia uhamishoni[5].

Tazama pia[hariri | hariri chanzo]

Maandishi yake[hariri | hariri chanzo]

Barua zake nyingi kwa mtetezi wake, Matilda wa Toscana zinapatikana katika:

Tanbihi[hariri | hariri chanzo]

Marejeo[hariri | hariri chanzo]

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]

Makala hii kuhusu Papa fulani bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Papa Gregori VII kama wasifu wake, habari za maisha au kazi yake?
Je, unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuiongezea habari.