Mwana wa Daudi

Mwana wa Daudi ni jina la heshima la wanaume waliotokana na vizazi vya mfalme Daudi na hivyo kuhusishwa na ahadi alilopewa na nabii Nathani kwamba ukoo wake utatawala milele (2Sam 7:1-29).
Wengi wa nasaba hiyo waliotawala baada ya Daudi walishindwa vibaya katika jukumu lao la kufanya Waisraeli wazidi kuwa waaminifu kwa Mungu pekee, hivyo walisababisha kwanza farakano la kudumu katika taifa lao na hatimaye maangamizi yaliyoacha nchi takatifu bila wakazi waliotarajiwa na bila mtawala kutoka ukoo wa Daudi.
Ndiyo sababu manabii walizidi kuelekeza Wayahudi kutumaini uaminifu wa Mungu utakaotokeza mfalme bora kama chipukizi kutoka kisiki cha Yese, baba wa Daudi.
Hivyo, kwa namna ya pekee, jina hilo lilitumika kwa Yesu aliyetambuliwa na wengi, ama wakati wa maisha yake au baada ya kifo chake, kuwa ndiye Masiya aliyetazamiwa.
Injili ya Mathayo na Injili ya Luka zinasisitiza haki ya Yesu kuitwa hivyo kwa kuorodhesha vizazi kati ya Daudi na Yosefu, mume wa Bikira Maria, mama yake.
| Makala hii kuhusu mambo ya Biblia bado ni mbegu. Je, unajua kitu kuhusu Mwana wa Daudi kama historia yake au athari wake? Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa? Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari. |