Nenda kwa yaliyomo

Muthoni Kirima

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru

Mũthoni Kĩrĩma (1931 – 4 Septemba 2023) alikuwa mwanamke mpiganaji wakati wa vita ya Mau Mau katika miaka ya 1950 dhidi ya ukoloni wa Waingereza. Wanawake wachache wa Mau Mau waliwahi kuwa wapiganaji hai, na Mũthoni alikuwa mwanamke pekee aliyeweza kufikia cheo cha Jemedari Mkuu.[1][2]

Maisha ya awali

[hariri | hariri chanzo]

Mũthoni Kĩrĩma alizaliwa katika kijiji cha Nairutia, Nyeri Kaunti, Kenya, mwaka 1931.[3] Alizaliwa kwa jina la Mũthoni Wihihuini, lenye asili ya jina la babu yake. Mũthoni alipokuwa bado mdogo sana, familia yake ilihamia Karing’ũ kutafuta maisha bora. Safari hiyo aliitaja kuwa ndefu na ngumu kwa msichana mdogo kama yeye. Walisafiri kilomita 15, nusu ya safari akiwa juu ya punda mdogo asiye na tandiko, na nusu nyingine aliitembea kwa miguu. Akiwa Karing’ũ, Mũthoni alianza kujifunza kuhusu Ukristo na akauvutiwa sana imani hiyo. Akiwa mtoto, aliingia kwenye hema la wamisionari pamoja na watoto wengine ili kujifunza Ukristo. Alipofikisha umri wa miaka minane, alianza kujitolea kwa kanisa kwa muda mrefu katika maisha yake.[4]

Uzoefu wake wa vurugu za kibaguzi kati ya walowezi wa Kenya na Wakikuyu ulitokea alipokuwa akifanya kazi za watoto katika shamba la mlowezi wa kizungu. Katika kipindi hiki cha maisha yake, alishuhudia matusi na unyanyasaji wa kihisia, vurugu za kimwili dhidi ya wanaume Wakikuyu, na ukatili wa kingono dhidi ya wanawake Wakikuyu. Hali hii ilichochea azma na ari yake ya kupigania uhuru ili kuwakomboa watu wake na nchi yake.[4] Mwaka 1948, alikutana na mume wake Mũtũngi Gicũhi, ambaye alikuwa mpishi kijana aliyefanya kazi katika shamba hilo hilo la mlowezi. Baada ya ndoa yao,walihamia pembezoni mwa mji wa Nyeri na kuanza maisha yao; Mũthoni akawa mfanyabiashara na mume wake akawa mpishi.[onesha uthibitisho]

Vita Ya Mau Mau

[hariri | hariri chanzo]
kitabu cha zamani kilicho kwenye makumbusho
Chapisho hili la mwaka 1959/60 linasimulia matukio yaliyopelekea kuibuka kwa wapigania uhuru wa Mau Mau

Mũthoni Kĩrĩma alikula kiapo cha Mau Mau kwa mara ya kwanza mwaka 1952.[5] Kuanzia hapo, ilimbidi kuweka sawa majukumu ya mapinduzi na majukumu ya kifamilia. Alianza kwa kutumia mitandao yake kama mfanyabiashara kupata taarifa na habari kuhusu yaliyokuwa yakitokea kwa Mau Mau waliokuwa msituni. Pia alipanga viapo vya watu wengine. Hili lilikuwa ngumu sana kwake kwa sababu wakati huo mume wake hakuwa amechukua kiapo, na alihisi hatia kwa kumdanganya. Hali hii ilibadilika mwaka 1953 wakati mume wake Mũtũngi Gicũhi alipoamua hatimaye kuchukua kiapo na kujiunga na Mau Mau. Siku hiyo hiyo, Mũthoni Kĩrĩma alimpeleka mume wake pamoja na mbuzi kwa baba mkwe wake katika msitu wa Kinaini ambako aliapa kujiunga na wapiganaji wa Mau Mau. Huo ulikuwa mara ya mwisho kumuona mume wake kwa miaka 11, kwani aliishi msituni hadi mwaka 1963.[6]

Siku iliyofuata, Chifu Mũhoya, ambaye alikuwa chifu Mwafrika chini ya utawala wa kikoloni nchini Kenya, alituma askari nyumbani kwa Mũthoni Kĩrĩma kumtafuta mume wake, kwani alikuwa mgombea wa kujiunga na Kamatimũ, kundi la waaminifu kwa serikali chini ya Chifu Mũhoya. Walipomuhoji, aliwaambia kwamba mume wake alikuwa ameenda kuchukua mayai na hakuwa amerudi, hivyo wakaondoka. Baada ya siku tatu, walirudi tena wakishuku kuwa alijiunga na wapiganaji wa Mau Mau. Ili kupata taarifa walizohitaji, walimpiga kikatili bila huruma. Katika mahojiano, anaeleza tukio hilo akisema, “Nilipigwa vibaya. Walinipiga mateke kwa buti zao hadi nilishindwa kabisa kusogea. Damu ilinitoka puani. Waliniacha nimepoteza fahamu.”[7] Anaeleza kuwa tukio hili ndilo lilikuwa hatua ya mabadiliko iliyomfanya atake siyo tu kusaidia Mau Mau akiwa kijijini, bali kuwa mpiganaji wa msituni. Ndipo alipokimbilia msituni na baada ya wiki moja akiwa peke yake, aliwapata wapiganaji wa Mau Mau.[6]

Kĩrĩma alianza maisha yake msituni kama asiye mpiganaji; kama wanawake wengine wengi, alipika na kuwahudumia wapiganaji huku akiwatafutia risasi na mabomu kutoka sokoni. Lakini haraka aliwavuta wenzake kwa ustadi wake wa kutumia silaha na kufikiri kwa haraka. Muda mfupi baadaye, alianza kuongoza vikosi vyake mwenyewe na kusaidia kuvunja mipaka ya kijinsia miongoni mwa wapiganaji wa Mau Mau. Katika mahojiano ya mwaka 2015, mwanamke mkongwe aliyekuwa askari anasema, “Kulikuwa na mwanamke mmoja aliyeitwa Mũthoni, nilikuwa naye. Hakuwa na hofu. Alikuwa akienda vitani pamoja na wanaume kwa sababu hakuwa akiogopa. Alikuwa mwanamke hatari; hata wanaume walimwogopa.”[8]

Mũthoni alikuwa mmoja wa viongozi wanawake wa harakati hizo na alipanda vyeo kwa haraka. Hata hivyo, si kupandishwa vyeo kote kulihusiana na mapigano; wapiganaji wa Mau Mau pia waliwatuza watu kwa mafanikio yasiyo ya kijeshi ili kuhimiza maendeleo ndani ya harakati zao. Alipandishwa cheo mara kadhaa kwa sababu, wakati uhaba wa chakula ulipokuwa tatizo, alijituma zaidi kutafuta chakula kwa ajili ya harakati na kwa askari wake. Matendo kama haya, pamoja na ustadi wake vitani, ndiyo yaliyomfanya apandishwe cheo hadi kuwa field-marshal. Pia alikuwa tabibu hodari na aliwahudumia waliojeruhiwa.[4]

  1. K24TV (1 Juni 2014), Muthoni Kirima, The Only Female Mau Mau Field Marshal, iliwekwa mnamo 8 Desemba 2016{{citation}}: CS1 maint: date auto-translated (link) CS1 maint: numeric names: authors list (link)
  2. "Bitter, betrayed but buoyant". Daily Nation (kwa British English). Iliwekwa mnamo 8 Desemba 2016.{{cite news}}: CS1 maint: date auto-translated (link)
  3. Fuentes, María José Gámez; Puente, Sonia Núñez; Nicolau, Emma Gómez (17 Oktoba 2019). Re-writing Women as Victims: From Theory to Practice. Routledge. ISBN 9781351043588.{{cite book}}: CS1 maint: date auto-translated (link)
  4. 1 2 3 Sammy, Mose. "Freedom fighter Field Marshal Muthoni Kirima takes final bow". The Standard (kwa Kiingereza). Iliwekwa mnamo 2024-01-18.
  5. Haynes, Aaron (12 Februari 2024). "Revolutionaries: Muthoni Kirima". iHeart (Podcast episode). Wamanica Podcast. Wonder Media Network. Iliwekwa mnamo 26 Julai 2024.{{cite web}}: CS1 maint: date auto-translated (link)
  6. 1 2 "Unequivocal, Unquantifiable, a Hero Eternal - A Tribute to Field Marshal Muthoni wa Kirima". African Digital Heritage (kwa American English). 2023-09-21. Iliwekwa mnamo 2025-05-17.
  7. Githethwa, Njuki (2022-03-07). "Profile of Field Marshall Mûthoni wa Kîrîma". Ukombozi Review (kwa American English). Iliwekwa mnamo 2025-05-17.
  8. Davies, Simon (2024-09-06). "Really Interesting People - MUTHONI WA KIRIMA, aged 92". www.reallyinterestingpeople.co.uk (kwa Kiingereza (Uingereza)). Iliwekwa mnamo 2025-05-17.