Mkimbizi

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Kambi ya wakimbizi wa Rwanda nchini Zaire mnamo mwaka 1994
Wakimbizi Wapalestina wakiondoka katika vijiji vyao katika Galilaya mnamo mwaka 1948

Mkimbizi ni mtu aliyeondoka kwao kwa sababu ya kulazimishwa, kufukuzwa au kwa hofu ya kuteswa.

Kuna mapatano ya kimataifa yanayoratibu hali hiyo. Chini ya Mkataba wa Umoja wa Mataifa kuhusu Hadhi ya Wakimbizi kutoka mwaka 1951, mkimbizi ni mtu ambaye (kulingana na ufafanuzi rasmi katika makala 1a ya mkataba huo), kutokana na hofu ya kweli ya kuteswa kwa sababu ya rangi, dini, utaifa, uanachama wa kikundi fulani cha kijamii, au maoni ya kisiasa, yumo nje ya nchi yake, na ameshindwa au, kutokana na hofu hiyo, hana nia ya kutegemea ulinzi wa nchi hiyo.[1]

Dhana ya mkimbizi ilipanuliwa na Itifaki ya 1967 ya Mkataba huo na mikataba ya kikanda katika Afrika na Amerika ya Kilatini kuwajumuisha watu waliokimbia vita au vurugu nyingine katika nchi zao za asili.

Wakimbizi walifafanuliwa kama kundi la kisheria katika kukabiliana na idadi kubwa ya watu waliokuwa wakikimbia Ulaya Mashariki kufuatia Vita Vikuu vya Pili vya Dunia.

Shirika la kimataifa linaloongoza juhudi za kuwalinda wakimbizi linaitwa Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi (kifupi kwa lugha ya Kiingereza: UNHCR), na liliwahesabu wakimbizi 8,400,000 duniani mwanzoni mwa mwaka 2006. Hii ilikuwa idadi ya chini kabisa tangu mwaka 1980.[2]

Isipokuwa wakimbizi 4,600,000 wa Kipalestina chini ya mamlaka ya Chombo cha Umoja wa Mataifa cha Kazi ya Wokozi kwa ajili ya Wakimbizi wa Kipalestina katika eneo la Mashariki ya Karibu (UNWRA kwa lugha ya Kiingereza), ambalo ni kundi la pekee lililopewa hadhi ya ukimbizi kwa wazawa kulingana na ufafanuzi wa hapo juu.[3]

Kamati ya Marekani kwa ajili ya Wakimbizi na Wahamiaji duniani inakadiria jumla ya wakimbizi kuwa 62,000,000 na inakadiria kuwa kuna zaidi ya watu 34,000,000 waliohamishwa makwao kutokana na vita, ikiwemo wale ambao wamebaki ndani ya mipaka ya taifa.

Wakimbizi wengi ambao huhama nchi zao hutafuta ukimbizi katika nchi jirani na kwao.

"Suluhisho la kudumu" kwa idadi kubwa ya wakimbizi, kama ilivyofafanuliwa na UNHCR na serikali ni: kuwarejesha kwa hiari yao kwenye nchi zao za asili; kuwajumuisha ndani ya nchi ya ukimbizi; na kuwapa makazi katika nchi ya tatu.[4]

Kufikia tarehe 31 Desemba 2005, nchi zilizokuwa vyanzo vikubwa vya wakimbizi zilikuwa Afghanistan, Iraq, Myanmar, Sudan, na Mamlaka ya Kitaifa ya Palestina.

Nchi yenye idadi kubwa ya waliohamishwa makwao nchini mwao ni Sudan, ambapo idadi hiyo ni watu milioni 5 kufikia mwaka 2006, ikiwa na wakimbizi na watu wasiokuwa na makao 800,000. Wakazi wote walipohesabika, Azerbaijan ilikuwa na idadi kuu ya watu waliofukuzwa kutoka makwao ulimwenguni kote.[5]

Wakimbizi na wengineo kwa eneo miaka 2008 - 2018
Eneo
(kadiri ya Umoja wa Mataifa)
2018[6] 2017[7] 2016[8] 2014[9] 2013[10] 2012[11] 2011[12] 2010[13] 2009[14] 2008[15]
Afrika 6,775,502 6,687,326 5,531,693 4,126,800 3,377,700 3,068,300 2,924,100 2,408,700 2,300,100 2,332,900
Asia 10,111,523 9,945,930 8,608,597 7,942,100 6,317,500 5,060,100 5,104,100 5,715,800 5,620,500 5,706,400
Ulaya 2,760,771 2,602,942 2,300,833 1,500,500 1,152,800 1,522,100 1,534,400 1,587,400 1,628,100 1,613,400
Amerika ya Kilatini na KaribI 215,924 252,288 322,403 352,700 382,000 380,700 377,800 373,900 367,400 350,300
Amerika Kaskazini 427,350 391,907 370,291 416,400 424,000 425,800 429,600 430,100 444,900 453,200
Australia na Pasifiki 69,492 60,954 53,671 46,800 45,300 41,000 34,800 33,800 35,600 33,600
Jumla 20,360,562 19,941,347 17,187,488 14,385,300 11,699,300 10,498,000 10,404,800 10,549,700 10,396,600 10,489,800

Historia[hariri | hariri chanzo]

Dhana kwamba mtu ambaye alikimbia kwenda pahali patakatifu hangeweza kuumizwa bila kusababisha adhabu ya kimungu, ilieleweka na Wagiriki na Wamisri wa kale. Hata hivyo, haki ya kutafuta hifadhi katika kanisa au mahali pengine patakatifu, iliandikwa kwa mara ya kwanza kisheria na Mfalme Ethelbert wa Kent miaka 600 Kabla ya Kuzaliwa kwa Yesu. Sheria sawa na hiyo zilitekelezwa kote Ulaya katika Zama za Kati. Dhana ifananayo na hiyo ya uhamisho wa kisiasa pia ina historia ndefu: Ovid alitumwa Tomis na Voltaire alilazimishwa aende uhamishoni Uingereza. Kupitia Amani ya Westfalia ya mwaka wa 1648, mataifa yalitambua uhuru wa kila taifa. Hata hivyo, haikuwa mpaka ujio wa utaifa ya kiromani mwishoni mwa karne ya kumi na nane barani Ulaya ndipo utaifa ulipokuwa maarufu kiasi kwamba maneno "nchi ya utaifa" yalimaanisha kuwa watu waliokuwa wakiivuka mipaka walitakiwa kuonyesha vitambulisho.

Waarmenia milioni moja walikimbia nchi ya Uturuki kati ya mwaka 1915 na 1923 wakitoroka mateso na mauaji ya kimbari.

Neno "mkimbizi" wakati mwingine hutumiwa na watu ambao wanaweza kuwa wanaufuata ufafanuzi ambao ungepatikana ikiwa Mkataba wa 1951 ungetumika kwa miaka ya nyuma. Kuna wengi ambao wangefaa kuitwa wakimbizi. Kwa mfano, baada ya Sheria ya Fontainebleau ya mnamo mwaka wa 1685 ilipopiga marufuku Uprotestanti nchini Ufaransa, mamia ya maelfu ya Wayugenoti walihamia Uingereza, Uholanzi, Uswidi, Afrika Kusini, Ujerumani na Prussia. Mawimbi ya mauaji ya makundi ya kisiasa yaliikumba Ulaya ya Mashariki, yakipelekea uhamisho mkubwa wa Wayahudi (zaidi ya milioni 2 ya Wayahudi wa Kirusi walihama katika kipindi cha miaka ya 1881 na 1920).

Tangu karne ya 19, watu wengi wa Kiislamu (ambao huitwa "Muhacir" chini ya ufafanuzi wa kijumla) walitoka eneo la Balkans, Caucasus, Crimea na Krete,[16] na kukimbilia Uturuki ya leo ambapo waliunda tabia za msingi za nchi hiyo.[17] Vita vya Balkans vya 1912-1913 vilisababisha watu 800,000 kuondoka makwao.[18] Makundi Mbalimbali ya watu yalitambuliwa rasmi kama wakimbizi kuanzia wakati wa Vita Vikuu vya Kwanza vya Dunia.

Uratibu wa kwanza wa kimataifa kuhusu masuala ya wakimbizi uliendeshwa na Ubalozi wa Wakimbizi wa Shirikisho la Mataifa. Ubalozi huo, uliongozwa na Fridtjof Nansen, na ulianzishwa mnamo mwaka wa 1921 kuwasaidia watu takriban 1,500,000 waliokimbia Mapinduzi ya Kirusi ya mwaka wa 1917 na vita vya wenyewe kwa wenyewe vilivyofuata (1917-1921), wengi wao wakiwa matajiri waliokuwa wakikimbia serikali ya Kikomiunisti. Mnamo mwaka wa 1923, mamlaka ya Ubalozi yaliongezwa na kujumuisha zaidi ya Waarmenia milioni moja ambao waliondoka kutoka Asia Ndogo ya Kituruki mnamo mwaka wa 1915 na 1923 kutokana na mfululizo wa matukio ambayo sasa yanajulikana kama mauaji ya Kimbari ya Waarmenia. Katika miaka kadhaa iliyofuata, mamlaka yaliongezwa kuwajumuisha wakimbizi Waashuri na Waturuki.[19] Katika matukio haya yote, mkimbizi alifafanuliwa kuwa mtu katika kundi ambalo Shirikisho la Mataifa lilikuwa limekubali kupitia mamlaka yake, kinyume na mtu ambaye ufafanuzi wa kijumla ulitumika kwake.

Mnamo mwaka wa 1923 kubadilishana kwa wakazi kati ya Ugiriki na Uturuki kulihusisha watu takriban milioni mbili, wengi wao wakiwa wamelazimishwa kufanywa wakimbizi na kunyimwa uraia kisheria kutoka makwao walipokuwa wamekaa kwa karne nyingi au hata milenia, katika mkataba uliokuzwa na kusimamiwa na jumuiya ya kimataifa kama sehemu ya Mkataba wa Lausanne.

Bunge la nchini Marekani lilipitisha Sheria ya Dharura ya Kikuota mnamo mwaka wa 1921, ikifuatiwa na Sheria ya Uhamiaji ya mnamo mwaka wa 1924. Sheria ya Uhamiaji ya mwaka wa 1924 ililenga kudhibiti zaidi watu wa Ulaya ya Kusini na Mashariki, hasa Wayahudi, Waitaliano na Waslavu, waliokuwa wameanza kuingia nchini humo kwa idadi kubwa kuanzia miaka ya 1890.[20] Wengi wa wakimbizi wa Ulaya (hasa Wayahudi na Waslavu) waliokuwa wakikimbia Stalin, Wanaksi na Vita Vikuu vya Pili vya Dunia walizuiwa kuingia Marekani.[21]

Mnamo mwaka wa 1930, Ofisi ya Kimataifa ya Nansen ya Wakimbizi ilianzishwa kama chombo cha kuchukua nafasi ya Tume. Mafanikio yake mashuhuri yalikuwa pasipoti ya Nansen, iliyokuwa pasipoti kwa ajili ya wakimbizi, na iliyofanya Ofisi hiyo kutunukiwa Tuzo la Amani la Nobel la mwaka wa 1938. Ofisi ya Nansen ilikumbwa na uhaba wa fedha, kuongezeka kwa idadi ya wakimbizi na kukataa kwa wanachama wa Shirikisho la Mataifa kuiruhusu Ofisi kuwasaidia wananchi wao. Hata hivyo, iliweza kuyashawishi mataifa kumi na manne kutia saini Mkataba wa Wakimbizi wa 1933, chombo dhaifu cha haki za kibinadamu, na kuwasaidia wakimbizi zaidi ya milioni moja.

Watoto wakijitayarisha kuokolewa kutoka Uhisapania wakati wa Vita vya Wenyewe kwa Wenyewe vya Uhispania kati ya mwaka wa 1936 na 1939.

Kuibuka kwa Unaksi kulisababisha ongezeko kubwa la wakimbizi kutoka Ujerumani kuliosababisha Shirikisho kuunda Ubalozi kuwashughulikia Wakimbizi waliokuwa wanatoka Ujerumani mnamo mwaka wa 1933. Mamlaka ya Ubalozi huu hatimaye yalipanuliwa kujumuisha watu kutoka Austria na Sudetenland. Wacheki 150,000 walifurushwa kutoka makazi yao baada ya tarehe 1 Oktoba 1938, wakati jeshi la Kijerumani lilipoingia katika maeneo ya mpakani ya Chekoslovakia wakizisalimu silaha zao kwa mujibu wa Mkataba wa Munich.[22]

Tarehe 31 Desemba 1938, Ofisi ya Nansen na Ubalozi zote zilivunjwa na badala yake Ofisi ya Ubalozi wa Wakimbizi chini ya Ulinzi wa Shirikisho ikaundwa.[19] Tukio hili lilikuwa sambamba na kukimbia kwa laki kadhaa ya Waripablikani wa Kihispania kwenda Ufaransa baada ya kushindwa na Wanataifa mnamo mwaka wa 1939 katika Vita Vya Wenyewe kwa Wenyewe vya Uhispania.[23]

Vita Vikuu vya Pili vya Dunia na Ubalozi wa Umoja wa Mataifa wa Wakimbizi[hariri | hariri chanzo]

Vita na migogoro ya kisiasa wakati wa Vita Vikuu vya Pili vya Dunia ilisababisha kiasi kikubwa cha uhamisho wa lazima (angalia Vita Vikuu vya Pili vya Dunia, ukombozi na kufukuzwa). Mnamo mwaka wa 1943, Muungano wa nchi Rafiki uliunda Shirika la Umoja wa Mataifa la Msaada na Kuanzisha Maisha Mapya (UNRRA kwa lugha ya Kiingereza) ili kutoa misaada kwa maeneo yaliyokombolewa kutoka nguvu za Kiaksisi, ikiwemo maeneo ya Ulaya na Uchina. Juhudi hizi zilijumuisha kuwarudisha zaidi ya wakimbizi milioni saba, ambao wakati huo walijulikana kama watu waliofukuzwa kutoka makwao, hadi katika nchi zao za kiasili na kuanzisha makambi ya watu waliotimuliwa makwao ya wakimbizi milioni moja ambayo walikataa kurudishwa nyumbani.

Katika miezi ya mwisho ya Vita Vikuu vya Pili vya Dunia takriban raia milioni tano wa Kijerumani kutoka mikoa ya Ujerumani ya Prussia ya Mashariki, Pomerania na Silesia walikimbia ushambulizi wa Jeshi Lekundu na wakawa wakimbizi katika maeneo ya Mecklenburg, Brandenburg na Saxony. Baada ya kukombolewa kwa Wehrmacht mnamo Mei 1945, Muungano wa nchi rafiki ulichukua Ujerumani katika mipaka jinsi ilivyokuwa tarehe 31 Desemba 1937 (Azimio la Berlin la tarehe 5 Juni, mwaka 1945), lakini kuanzia mwaka wa 1945 Wapolandi walikuwa wameanza kuwafukuza raia wa Kijerumani waliokuwa wamebaki (utakaso wa kikabila) na kwa kipindi kifupi muungano wa nchi rafiki ulipokutana mjini Potsdam tarehe 17 Julai mwaka wa 1945 katika Mkutano wa Potsdam, hali ya ukimbizi iliyokuwa na vurugu nyingi ilizikabili nchi zilizokuwa na nguvu, ambazo, kwa mujibu wa Ibara ya IX ya Itifaki ya Potsdam ya tarehe 2 Agosti mwaka wa 1945 ilihifadhi mapema robo moja ya eneo la Ujerumani chini ya utawala wa Kipolandi; kwa mujibu wa Ibara ya XIII ya itifaki, raia wajerumani waliobaki nchini Poland, Chekoslovakia na Hungaria walikuwa wahamishwe Magharibi kwa namna "taratibu na yenye kuzingatia utu".

Ingawa haikukubalika na Muungano wa nchi rafiki zilizokutana mjini Potsdam, mamia ya maelfu ya raia wa kabila la Kijerumani waliokuwa wakiishi nchini Yugoslavia na Romania walifukuzwa nchini humo kufanya kazi ya utumwa katika nchi ya Umoja wa Kisovyeti na hatimaye kufukuzwa hadi Ujerumani iliyokuwa iliyotawaliwa, Ujerumani iliyokuwa chini ya nchi rafiki na hatimaye hadi Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kijerumani, Austria na Shirikisho la Jamhuri ya Ujerumani. Huu ulikuwa uhamisho mkubwa zaidi katika historia. Wajerumani milioni 15 waliathirika, na zaidi ya milioni mbili walikufa kufukuzwa kwa raia wa Kijerumani[24]. (Angalia Wajerumani kuhama kutoka Ulaya ya Mashariki.) Kati ya mwisho wa Vita Vikuu vya Pili vya Dunia na ujenzi wa Ukuta wa Berlin mnamo mwaka wa 1961, zaidi ya wakimbizi 563,700 kutoka Ujerumani ya Mashariki walisafiri hadi Ujerumani ya Magharibi wakitoroka uvamizi wa Kirusi.

Pia, mamilioni ya watu ambao awali walikuwa raia wa Kirusi walirudishwa kwa nguvu (dhidi ya mapenzi yao) hadi USSR.[25] Mnamo tarehe 11 Februari mwaka wa 1945, katika hitimisho la Mkutano wa Yalta, Marekani na Uingereza zilitia saini Mkataba wa Kuwarejesha raia hadi nchi ya Umoja wa Kisovyeti.[26] Tafsiri ya Mkataba huu ilisababisha kurudishwa kwa lazima kwa Wasovyeti wote bila kuijali nia yao. Wakati vita vilipomalizika mnamo Mei mwaka wa 1945, wenye mamlaka nchini Uingereza na Marekani waliamuru majeshi yao yaliokuwa Ulaya wakati huo kuwarudisha hadi Umoja wa Kisovyeti mamilioni ya wakazi wa zamani wa Umoja wa Kisovyeti, pamoja na watu wengi ambao walikuwa wametoka nchini Urusi na kupata uraia tofauti miaka mingi hapo awali. Oparesheni za kuwarudisha raia makwao kwa lazima zilifanyika kati ya mwaka wa 1945 hadi mwaka wa 1947.[27]

Vita Vikuu vya Pili vya Dunia vilipokamilika, kulikuwa na zaidi ya watu milioni 5 "waliotimuliwa" kutoka Umoja wa Kisovyeti katika Ulaya ya Magharibi. Takriban milioni 3 walikuwa wafanyikazi wa lazima (Ostarbeiters)[28] nchini Ujerumani na maeneo yaliyovamiwa.[29][30] Wafungwa wa Kivita (POW's kwa lugha ya Kiingereza) wa Urusi na wanaume Wavlasovu waliwekwa chini ya mamlaka ya SMERSH (Kifo kwa Majasusi). Kufikia mwisho wa vita, kati ya wale wafungwa wa vita milioni 5.7 wa Kisovyeti waliokuwa wamekamatwa na Wajerumani, milioni 3.5 walikuwa wamefariki wangali kifungoni mikononi mwa Wajerumani.[31][32] Manusura baada ya kurudi nchi ya Umoja wa Kisovyeti walitazamwa kama wasaliti (Angalia Amri Nambari 270).[33][34] Zaidi ya wanajeshi milioni 1.5 wa Jeshi Jekundu walinusurika kifo na kufungwa na Wajerumani waliowatuma kwenda jela za Gulagi.[35][36]

Poland na Ukraine ya Kisovyeti zilifanya ubadilishanaji wa raia- wa Kipolandi ambao waliishi mashariki ya mpaka uliokuwa umeundwa na Poland na Wasovyeti walifukuzwa kwenda nchini Poland (takriban watu 2,100,000) (Tazama Kurudishwa Nyumbani kwa Wapolandi) na Wayukreni walioishi magharibi mwa mpaka kati ya Poland na Umoja wa Kisovyeti walihamishwa hadi Ukraine ya Kisovyeti. Uhamisho wa raia kwenda Ukraine ya Kisovyeti ulifanyika kuanzia Septemba mwaka wa 1944 hadi Mei mwaka wa 1946 (takriban watu 450,000) (angalia Kurudishwa nyumbani kwa Wayukreni). Baadhi ya Wayukreni (takriban watu 200,000) walihama kutoka Poland ya kusini-mashariki kwa hiari yao (kati ya 1944 na 1945).[37]

UNRRA iliundwa mnamo mwaka wa 1947, wakati ilipoanza kusimamiwa na Shirika la Kimataifa la Wakimbizi lililokuwa limeanzishwa upya. Ingawa makabidhiano awali yalikuwa yamepangwa kufanyika mwanzoni mwa 1947, hayakuweza kutokea hadi Julai mwaka wa 1947.[38] Shirika la Kimataifa la Wakimbizi lilikuwa shirika la muda tu la Umoja wa Mataifa (UN kwa Kiingereza), ambalo lenyewe lilikuwa limeundwa mwaka wa 1945, likiwa na mamlaka makuu ya kumaliza kazi ya UNRRA ya kuwarejesha au kuwapea makao mapya wakimbizi wa Ulaya. Lilifutiliwa mbali mnamo mwaka wa 1952 baada ya kuwatafutia makao mapya wakimbizi milioni moja.[39] Ufafanuzi wa mkimbizi wakati huu ulikuwa mtu binafsi mwenye pasipoti ya Nansen au "Cheti cha Uwezo" zilizotolewa na Shirika la Kimataifa la Wakimbizi.

Ubalozi wa Umoja wa Mataifa wa Wakimbizi[hariri | hariri chanzo]

Ukiwa na makao yake makuu mjini Geneva, Uswidi, Ofisi ya Ubalozi wa Umoja wa Mataifa wa Wakimbizi (UNHCR kwa kiingereza) (ulioundwa mnamo tarehe 14 Desemba 1950) hulinda na kuwasaidia wakimbizi baada ya ombi la serikali au la Umoja wa Mataifa na huwasaidia kurudi kwao au huwasaidia kutafuta makazi upya. Wakimbizi wote duniani wamo chini ya mamlaka ya Ubalozi wa Umoja wa Mataifa wa Wakimbizi isipokuwa Wapalestina wa Kiarabu waliokimbia lile lililokuja kuwa taifa la Kiyahudi kati ya 1947 na 1948 (angalia hapa chini). Hata hivyo, Wapalestina ambao walikimbia baada maeneo ya Kipalestina baada ya mwaka 1948 (kwa mfano, wakati wa vita vya siku sita vya 1967) wamo chini ya mamlaka ya UNHCR.

UNHCR hutoa ulinzi na msaada sio tu kwa wakimbizi, lakini pia kwa makundi mengine ya watu waliofukuzwa makwao au ambao yana mahitaji fulani. Hawa ni pamoja na wanaotafuta hifadhi, wakimbizi waliorudi nyumbani lakini ambao bado wanahitaji msaada kuyajenga maisha yao upya, jamii za ndani za raia zilizoathirika moja kwa moja na kuhama kwa wakimbizi, watu wasiokuwa na taifa na kinachojulikana kama watu waliokimbia makazi ndani ya nchi yao ("IDPs" kwa Kiingereza). Waliokimbia makazi ndani ya nchi yao ni raia ambao wamefurushwa kutoka makazi yao, lakini ambao bado hawajafika nchi jirani na kwa hivyo, wakitofautishwa na wakimbizi, hawalindwi na sheria ya kimataifa na huenda ikawa vigumu kwao kupokea msaada wa aina yoyote. Kwa sababu hali ya vita imebadilika katika miongo michache iliyopita, idadi ya migogoro inayofanyika ndani ya nchi fulani inazidi vita kati ya nchi mbalimbali, idadi ya waliokimbia makazi yao imeongezeka kwa kiasi kikubwa kiasi cha kufikia takriban watu milioni 5 duniani kote.

Ilikuja baada ya Shirika la Kimataifa la Wakimbizi la hapo awali na hata kabla ya hilo, Shirika la Umoja wa Mataifa la Kusimamia Usaidizi na Uanzishaji Upya wa Maisha (ambalo lenyewe lilikuja baada ya Ubalozi wa Wakimbizi wa Shirikisho la Umoja wa Mataifa).

Ubalozi wa Umoja wa Mataifa wa Wakimbizi ulitunukiwa Tuzo la Amani la Nobel katika miaka ya 1954 na 1981. Mamlaka ya shirikisho hilo ni kuongoza na kuratibu hatua za kimataifa za kuwalinda wakimbizi na kutatua matatizo ya wakimbizi duniani kote. Lengo lake msingi ni kulinda haki na ustawi wa wakimbizi. Linanuia kuhakikisha kwamba kila mtu anaweza kupewa haki ya kutafuta hifadhi na kupata kimbilio salama katika Jimbo jingine, na chaguo la kurudi nyumbani kwa hiari, kutangamana na wenyeji au kuishi katika nchi ya tatu.

Watu wengi mashuhuri wanahusika na shirika hilo kama Mabalozi wa Fadhila wa Ubalozi wa Umoja wa Mataifa wa Wakimbizi, kwa sasa wachache kati yao wakiwa Angelina Jolie, Giorgio Armani na wengineo. Mtu binafsi ambaye alichangisha pesa zaidi katika kuimba kwake na kazi ya kujitolea kwa niaba ya Ubalozi wa Umoja wa Mataifa wa Wakimbizi alikuwa ni Luciano Pavarotti[6]..

Mamlaka ya Ubalozi wa Umoja wa Mataifa wa Wakimbizi yamezidi kupanuliwa kujumuisha kulinda pamoja na kutoa msaada wa kibinadamu kwa wale ambao inawatambua kuwa watu wengine "wanaofaa kusaidiwa," ikiwa ni pamoja na watu waliokimbia makazi yao kimataifa jambo ambalo ni sambamba na ufafanuzi wa kisheria wa mkimbizi chini ya Mkataba wa Wakimbizi wa 1951 na Itifaki ya 1967, Mkataba wa Shirika la Umoja wa Afrika la 1969 , au mkataba wowote mwingine ikiwa walitoka nchi yao, lakini bado wanabaki katika nchi yao ya asili. Kwa hivyo Ubalozi wa Umoja wa Mataifa wa Wakimbizi una mishoni nchini Kolombia, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Serbia na Montenegro na Ivory Coast ili kusaidia na kutoa huduma kwa wale waliokimbia makazi yao.

Tangu tarehe 1 Januari 2006 kuna wakimbizi 20,751,900 duniani.

Asia – 8,603,600

Afrika – 5,169,300

Ulaya – 3,666,700

Amerika ya Kilatini na Karibiani – 2,513,000

Amerika ya Kaskazini – 716,800

Osheania - 82,500


Wakimbizi ni kundi dogo la jamii pana ya watu wasiokuwa na makao. Wakimbizi wa kimazingira (watu waliokimbia makazi yao kwa sababu ya matatizo ya kimazingira kama vile ukame) hawajumuishwi katika ufafanuzi wa "wakimbizi" chini ya sheria ya kimataifa, kama vile watu waliokimbia makazi yao. Kulingana na sheria ya wakimbizi ya kimataifa, mkimbizi ni mtu ambaye anatafuta kimbilio katika nchi geni kwa sababu ya vita na uhasama, au kwa sababu ya hofu ya mateso "kwa sababu ya rangi, dini, utaifa, maoni ya kisiasa, au uanachama katika kundi fulani la kijamii" (kwa kutumia istilahi kutoka sheria ya Marekani).

Hadi ombi la kimbilio likubaliwe, mtu huyo anaitwa "mtafuta hifadhi". Ni tu baada ya kutambua mahitaji ya kulindwa ya mtafuta hifadhi, ndipo yeye anajulikana rasmi kama mkimbizi na ana usalama wa hali ya ukimbizi, hali ambayo inaambatana na haki na wajibu fulani kwa mujibu wa sheria ya nchi inayompokea.

Uamuzi bayana ikiwa mtu ni mkimbizi au la kwa kawaida ni jukumu la vyombo fulani vya serikali ndani ya nchi inayomtunza mkimbizi. Hili linaweza kusababisha hali ambapo nchi haitatambua hadhi ya ukimbizi ya watafuta hifadhi wala kuwaona kama wahamiaji halali na kuwafanya kama wahamiaji haramu.

Kwa upande mwingine, maombi laghai katika mazingira yenye utekelezaji ambao si wa makini unaweza kusababisha hali ya ukimbizi isiyofaa, itakayosababisha kuondosha rasilimali kutoka kwa wale wenye mahitaji ya kweli.Kigezo:Inahitaji kuhakikishwa Asilimia ya wakimbizi wanaotafuta hifadhi wasiotimiza mahitaji maalum ya kimataifa ya wakimbizi, na ambao inafaa wapewe makazi mapya inatofautiana kutoka nchi moja hadi nyingine. Waombaji hifadhi wasiofuzu mara nyingi hufukuzwa makwao, wakati mwingine baada ya kufungwa au kuzuiliwa, jinsi inavyofanywa nchini Uingereza.

Madai ya kutafuta hifadhi, pia yanaweza kufanywa mkimbizi anapowasili katika nchi aliyokimbilia, kwa kawaida baada ya kuwasili bila ruhusa. Baadhi ya serikali huwahimili na kuwakubali wakimbizi wa aina hii; serikali nyingine hazitayakataa madai hayo tu, bali huweza kuwakamata au kuwaweka kizuizini wanaojaribu kutafuta hifadhi.

Mashirika yasiyo ya kiserikali yanayojishughulisha na wakimbizi na wanaotafuta hifadhi yamedokeza ugumu kwa watu waliofukuzwa kutoka makazi yao kutafuta hifadhi katika nchi zilizostawi. Kwani sera za uhamiaji za nchi hizi mara nyingi hulenga na kupambana na uhamiaji usiokuwa wa kawaida na uimarishaji wa udhibiti wa mipaka unawafanya watu waliofukuzwa kutoka makwao washindwe kuingia katika eneo ambalo wangeweza kuwasilisha madai ya kutafuta hifadhi. Ukosefu wa fursa za kuzipata kisheria taratibu za hifadhi unaweza kulazimisha wanaotafuta hifadhi mara nyingi kufanya majaribio ghali au ya kihatari ili kuingia kinyume cha sheria.

Kuwapa wakimbizi makazi mapya[hariri | hariri chanzo]

Jimbo Kuota (2001) Mwaka wa wa kuanzishwa
Marekani 80,000 1980
Kanada 11,000 1978
Australia 10,000 Haijulikani
Norway 1,500 Haijulikani
Uswidi 1,375 1950
New Zealand 750 1979
Finland 750 1979
Denmark 517 1989
Uholanzi 500 1984

Kuwapa wakimbizi makazi mapya kunahusisha kuwasaidia wakimbizi ambao hawawezi kurudi salama nyumbani katika nchi za tatu.[40][41] Ubalozi wa Umoja wa Mataifa wa Wakimbizi kwa muda mrefu umetambua kwamba kuwapa wakimbizi makazi mapya kama mojawapo ya "masuluhisho ya kudumu" yasiyofaa kuchaguliwa kwa kawaida.[42] Hata hivyo, mwezi Aprili mwaka 2000 Balozi wa Umoja wa Mataifa wa Wakimbizi, Sadako Ogata, alisema:

Kuwapa wakimbizi makazi mapya hakuwezi tena kutazamwa kama suluhisho la mwisho la kudumu; mara kwa mara, ndilo suluhisho la "kipekee" kwa wakimbizi

—Sadako Ogata, Balozi wa Umoja wa Mataifa wa Wakimbizi, Aprili mwaka wa 2000 [42]

Ubalozi wa Umoja wa Mtaifa wa Wakimbizi ulipendekeza kuwa zaidi ya wakimbizi 121,000 watiliwe maanani wakati wa kutafuta makazi mapya ya wakimbizi mnamo mwaka wa 2008. Hii ilikuwa ni idadi kubwa zaidi kwa kipindi cha miaka 15. Mnamo mwaka wa 2007, watu 98,999 walipendekezwa. Ubalozi wa Umoja wa Mtaifa wa Wakimbizi ulipendekeza wakimbizi 33,512 kutoka Iraq, 30388 kutoka Burma/ Myanmar na 23,516 kutoka Bhutan mnamo mwaka wa 2008.[41]

Kuhusiana na kuwapa makao mapya waliotoka, mnamo mwaka wa 2008 wakimbizi 65,548 walipewa makao mapya katika nchi 26, ongezeko kutoka idadi ya 49,868 ya mwaka wa 2007.[41] Idadi kubwa zaidi ya waliosaidiwa na Ubalozi wa Umoja wa Mataifa wa Wakimbizi kutoka walikuwa kutoka nchi za Thailand (16.807), Nepal (8.165), Syria (7.153), Jordan (6.704) na Malaysia (5.865).[41] Kumbuka kwamba hizi zilikuwa nchi za kutoka ambapo wakimbizi walipewa makao mapya, si nchi zao za kiasili.

Idadi kubwa ya nchi za tatu zina mikakati maalum za kuwapa wakimbizi makao mapya zikishirikiana na Ubalozi wa Umoja wa Mataifa wa Wakimbizi. Ukubwa wa harakati hizi umeonyeshwa katika jedwali.[42] Harakati kubwa zaidi zinaendeshwa na nchi za Marekani, Kanada na Australia. Nchi nyingi za Ulaya zinaendesha harakati sawa lakini ndogo na mnamo mwaka wa 2004 Uingereza ilianzisha harakati yake yenyewe, inayojulikana kama Mpango wa Kulinda Lango[42] ikiwa na kuota ya awali ya 500 (2004), ambayo ilizidi hadi 750 katika mwaka wa kifedha wa 2009/09.[43] Mnamo Septemba mwaka wa 2009, Tume ya Ulaya ilizindua mipango ya harakati mpya za makazi mapya ya pamoja ya Tume ya Ulaya. Mpango huo ungehusisha nchi wanachama za Tume ya Ulaya ambapo zingefaa kuamua kwa pamoja wakimbizi ambao wangefaa kupewa kipaumbele. Nchi wanachama zingepokea €4,000 kutoka Mfuko wa Ulaya wa Wakimbizi kwa kila mkimbizi aliyepewa makao.[44]

Sheria ya wakimbizi[hariri | hariri chanzo]

Chini ya sheria ya kimataifa, wakimbizi ni watu ambao:

  • wamo nje ya nchi yao ya kitaifa au makazi waliyoyazoea;
  • wana hofu ya kweli ya kuteswa kwa sababu ya rangi, dini, utaifa, uanachama katika kundi fulani la kijamii au maoni ya kisiasa na
  • hawawezi au hawataki kujitoa ili walindwe na nchi hiyo, au kurudi huko, kwa hofu ya mateso.

Sheria ya wakimbizi inajumuisha sheria ya kimila, kanuni msingi, na vifaa vya kimataifa vya kisheria. Haya ni pamoja na:

  • Mkataba wa Umoja wa Mataifa unaohusiana na Hadhi ya Wakimbizi wa mwaka 1951; pia inajulikana kama Mkataba wa Geneva;

Makambi ya wakimbizi[hariri | hariri chanzo]

Kambi nchini Guinea ya wakimbizi kutoka Sierra Leone.

Makambi ya wakimbizi ni mahali palipojengwa na serikali au mashirika yasiyokuwa ya kiserikali (kama vile Shirika la Kimataifa la Msalaba Mwekendu (ICRC kwa lugha ya Kiingereza)) kupokea wakimbizi. Watu wanaweza kukaa katika kambi hizi, wakipokea chakula cha kidharura na msaada wa kimatibabu, hadi wakati ambapo itakuwa salama kurudi makwao au mpaka watakapochukuliwa na watu wengine waliotoka nje ya kambi hizo. Katika baadhi ya matukio, mara nyingi baada ya miaka kadhaa, nchi nyingine huamua kwamba kamwe haitakuwa salama kuwarudisha watu hawa, na wao hupewa makazi mapya katika "nchi za tatu," mbali na mipaka waliyoivuka. Hata hivyo, mara nyingi, wakimbizi hupewa makazi mapya. Katika muda huo wote, wanakumbwa na hatari za magonjwa, watoto kufanywa kuwa majeshi, kuajiriwa katika shughuli za kigaidi, na kubakwa.

Kimataifa, takriban nchi 17 (Australia, Benin, Brazili, Burkina Faso, Kanada, Chile, Denimaki, Finland, Iceland, Jamhuri ya Ireland, Mexico, Uholanzi, New Zealand, Norway, Uswidi, Uingereza, na Marekani [7]) mara kwa mara hukubali wakimbizi wa kikuota kutoka maeneo kama vile makambi ya wakimbizi. Kawaida watu hawa ni watu ambao wametoroka vita. Katika miaka ya hivi karibuni, wakimbizi wengi wa kikuota wametoka Iran, Afghanistan, Iraq, Liberia, Somalia, na Sudan, nchi ziliizokumbwa na vita na mapinduzi mbalimbali, na Yugoslavia ya zamani, kutokana na Vita vya Kiyugoslavia.

Kulingana na Agence France-Presse, Ujapani iliwakubali watu kumi tu kuingia nchini kama wakimbizi mnamo mwaka wa 2003, idadi ya watu ya chini kabisa nchi hiyo iliyowakubali kuingia nchini tangu mwaka wa 1997 ilipomkubali mtu mmoja pekee. Ijapokuwa iliwanyima hadhi ya ukimbizi, Ujapani iliwakubali watu 16 zaidi mwaka huo ikitumia misingi maalum ya kibinadamu - pia takwimu ya chini kabisa tangu mwaka wa 1997, ambapo iliwakubali watu watatu. Kwa kulinganisha, watu 336 waliomba kupewa hadhi ya ukimbizi nchini Ujapani mwaka huo, takwimu ya juu zaidi katika muda wa miaka miwili. Mashirika mbalimbali ya kimataifa, pamoja na Ubalozi wa Umoja wa Mataifa wa Wakimbizi, zimeomba nchi ya Ujapani kuwakubali wakimbizi zaidi.[45]

Marekani iliwachukua wakimbizi 85,010 kwa ajili ya kuwapa makazi mapya, kulingana na Ubalozi wa Umoja wa Mataifa wa Wakimbizi. New Zealand iliwakubali wakimbizi 1,140 mnamo mwaka wa 1999.

Watu wa meli[hariri | hariri chanzo]

Neno "watu wa meli" lilikuja kutumika kawaida katika miaka ya 1970 wakati msafara mkubwa wa wakimbizi wa Kivietinamu ulipohama kutoka Vietnam kufuatia Vita vya Vietnam.

Maneno hayo yanatumika sana kuashiria uhamiaji kutoka Cuba, Haiti, Moroko, Vietnam au Albania. Wao mara nyingi uyahatarisha maisha yao katika meli zilizoundwa shaghalabaghala na zilizosongamana ili kutoroka uonevu au umaskini katika mataifa yao ya nyumbani. Matukio yaliyotokana na Vita vya Vietnam yaliwafanya watu wengi nchini Cambodia, Laos, na hasa Vietnam kuwa wakimbizi mwishoni mwa miaka ya 1970 na 1980. Mnamo mwaka wa 2001, watafuta hifadhi 353 waliokuwa wakisafiri kwa meli kutoka Indonesia hadi Australia walikufa maji chombo chao kilipozama.

Hatari kuu kwa mtu wa meli ni kwamba meli wanazozitumia kusafiri zinaweza kuwa chochote ambacho kinaelea majini na kinachoweza kutosha kuwabeba abiria. Ingawa meli ya aina hiyo zilizoundwa shaghalabaghala zinaweza kusababisha janga, mnamo mwaka wa 2003 kundi dogo la wakimbizi 5 wa Kikiuba lilijaribu (bila kufaulu, lakini bila kupatwa na madhara yoyote) kufika jimbo la Florida likitumia lori la aina ya kubebea mizigo la miaka ya 1950 lililofanywa kuelea kutumia mapipa ya mafuta yaliyofungiliwa katika sehemu za upande.

Watu wa meli mara nyingi ni chanzo cha utata katika taifa ambapo wananuia kutafuta makao, kama vile Marekani, New Zealand, Ujerumani, Ufaransa, Urusi, Canada, Italia, Ujapani, Korea ya Kusini, Uhispania na Australia. Watu wa meli mara nyingi huzuiwa kwa kutumia nguvu kutowasili wanapotaka kufika, kama mfano Sheria ya Kipasifiki ya Australia (ambayo ilidumu kuanzia mwaka wa 2001 hadi mwaka wa 2008), au wanalazimishwa kuingia kizuizini baada ya wao kuwasili. Kuwekwa kizuizini kwa lazima nchini Australia kutakomeshwa, ilivyotangazwa na serikali ya Kazi ya Kevin Rudd mnamo Julai mwaka 2008, isipokuwa mtafuta hifadhi anayeonekana kuwa na uwezekano wa kuhatarisha usalama wa jamii kwa upana, kama vile kuhatarisha jamii kiafya.[46][47]

Shida ya wakimbizi kihistoria na wakati wa sasa[hariri | hariri chanzo]

Hali ya wakimbizi katika eneo la Mashariki ya Kati[hariri | hariri chanzo]

Wakimbizi wa Kipalestina[hariri | hariri chanzo]

Kufuatia Israeli kufanywa kuwa taifa mnamo mwaka wa 1948, Vita vya kwanza kati ya Waarabu na Waisraeli vilianza. Wapalestina wengi tayari walikuwa wakimbizi, na Kutoka kwa Wapalestina] kuliendelea katika kipindi chote cha Vita Vya 1948 dhidi ya Waarabu na Waisraeli na baada ya mpango wa kusitisha vita ambao ulikomesha vita hivyo. Wengi wao wamebaki kuwa wakimbizi kwa vizazi vingi kwani hawakuwaruhusiwa kurudi makwao wala kufanya makao katika nchi za Kiarabu ambapo walikuwa wakiishi. Hali ya wakimbizi na kuwepo kwa makambi mengi ya wakimbizi inaendelea kuwa chanzo cha msuguano katika mgogoro wa Waarabu na Israel.

Makisio ya mwisho ya idadi ya wakimbizi yalikuwa 711,000 kulingana na Tume ya Umoja wa Mataifa ya Upatanisho. Wakimbizi wa Kipalestina kutoka mwaka wa 1948 na wazao wao hawashughulikiwi na Mkataba wa mwaka wa 1951 wa Umoja wa Mataifa unaohusiana na Hadhi ya Wakimbizi, bali wanashughulikiwa na Chombo cha Umoja wa Mataifa cha Usaidizi na Kazi cha Wakimbizi wa Kipalestina katika eneo la Mashariki ya Karibu (UNRWA kwa lugha ya Kiingereza), ambalo liliunda vigezo vyake vyenyewe vya uanishaji wa wakimbizi. tovuti ya UNRWA:

Wakimbizi wa Kipalestina ni watu ambao makazi yao ya kawaida yalikuwa Palestina kati ya mwezi Juni mwaka wa 1946 na mwezi Mei mwaka wa 1948, na ambao walipoteza nyumba zao na mbinu za kujipatia riziki kama matokeo ya mgogoro kati ya Waarabu na Israeli mnamo mwaka wa 1948. Huduma za UNWRA zinapatikana kwa wale wote wanaoishi katika eneo lake la kazi na ambao wanawiana na ufafanuzi huu, ambao wameandikishwa na Shirika na ambao wanahitaji msaada. Ufafanuzi wa UNWRA wa mkimbizi pia unajumuisha wazao wa watu ambao walikuwa wakimbizi mnamo mwaka wa 1948.

Kwa hivyo wao ndio idadi ya kipekee ya wakimbizi iliyofafanuliwa kisheria kujumuisha wazao wa wakimbizi, ikiwemo wengine ambao pia vinginevyo wanaweza kutazamwa kama watu wasiokuwa na makao.

Mnamo mwezi Desemba mwaka wa 2005, Wanatakwimu wa Dunia wa Wakimbizi wa Kamati ya Marekani ya Wakimbizi na Wahamiaji walikadiria idadi jumla ya wakimbizi wa Kipalestina kuwa 2,966,100.

Wakimbizi wa Kiyahudi[hariri | hariri chanzo]

Kati ya Vita Vikuu vya Kwanza vya Dunia na vya Pili, uhamiaji wa Wayahudi kuelekea Palestina ulihimizwa na harakati ya Kizayuni iliyokuwa inazidi kukuwa lakini ulikatazwa na mamlaka ya Uingereza katika eneo la Palestina. Nchini Ulaya, mateso dhidi ya Wanaksi yalifikia kilele Mauaji ya Kimbari ya Wayahudi yalipotendeka na pia mauaji ya halaiki ya Wayahudi wengi wa barani Ulaya yalipofanyika.

Mkutano wa Evian, Mkutano wa Bermuda, na mikutano mingine ilishindwa kutatua tatizo la kuwapa makao idadi kubwa ya wakimbizi wa Kiyahudi kutoka Ulaya iliyovamiwa na Wanaksi. Kufuatia kuundwa kwake mnamo mwaka wa 1948, kulingana na Mpango wa Ugawaji wa Umoja wa Mataifa wa 1947, Israeli ilitumia Sheria ya Kurejea, ikiwapa uraia wa Kiisraeli wahamiaji wowote wa Kiyahudi. Takriban wakimbizi 700,000 walifurika kuingia nchini humo, na walipewa makazi katika miji ya mahema iliyoitwa ma'abarot. Baada ya Kufutiliwa mbali kwa Umoja wa Kisovyeti, uhamiaji wa pili mkubwa wa Wayahudi wa Kirusi 700,000 ulikimbilia Israeli kati ya 1990 na 1995.

Wayahudi wameishi katika kile ambacho sasa ni majimbo ya Kiarabu angalau tangu kifungoni nchini Babeli (597 KK). Kukataa kwa dunia ya Kiarabu kukubali kuwepo kwa nchi ya Wayahudi kulisababisha kuongezeka kwa ubaguzi na ukatili dhidi ya Wayahudi. Mnamo mwaka wa 1948, shirikisho la Uarabu lilitangaza Wayahudi kuwa raia adui. Akaunti za benki za Kiyahudi na mali ya Kiyahudi yalinyakuliwa, Wayahudi walikamatwa na kufutwa kazi, na masinagogi yalishambuliwa.[48] Katika miaka ya mwanzo baada ya uhuru wa Israel idadi ya Wayahudi katika nchi za Kiarabu ilipungua kwa kiwango kubwa: nchini Yemen, kutoka 55,000 hadi 4,000; Iraq kutoka 135,000 hadi 6000; Aden kutoka 8,000 hadi 800; Misri kutoka 80,000 hadi 50,000, Libya kutoka 38,000 hadi 4,000; na Syria kutoka 30,000 hadi 5000.[48]

Kulingana na takwimu rasmi za Kiarabu, Wayahudi 856,000 walihama kutoka makazi yao katika nchi za Kiarabu tangu mwaka wa 1948 hadi miaka ya mapema ya 1970. Takriban 600,000 kati yao walipata makazi mapya nchini Israeli. Wazao wao, na wale wa Wayahudi wa kutoka nchi ya Iran na Uturuki, sasa hujumuisha idadi ya milioni 3.06 kati ya raia wa Israeli wa Kiyahudi walio kati ya milioni 5.4 na 5.8.[49] Taabu za Wayahudi katika nchi za Kiarabu ilizidi kuwa mbaya zaidi kufuatia Vita vya Siku Sita vya mwaka wa 1967, vilivyosababisha kutoka kwa idadi kubwa ya Wayahudi waliobaki. Wayahudi wachache sana wanaishi katika nchi za Kiarabu kwa sasa.

Mnamo mwaka wa 2007, maazimio sawa (H.Res.185 na S.Res.85) yalipendekezwa na Bunge la Marekani, ili:

Kuifanya iwe wazi kuwa Serikali ya Marekani inaunga mkono msimamo kuwa, kama sehemu muhimu ya mpango wowote mpana wa amani, masuala ya wakimbizi na ukiukaji mkubwa wa haki za binadamu wa watu wanaopatikana kwa idadi chache katika nchi za Kiarabu na Kiislamu katika Mashariki ya Kati, Afrika Kaskazini na Ghuba la Kiajemi lazima yatatuliwe kupitia njia inayojumuisha (A) uzingatifu wa haki halali za wakimbizi wote waliofukuzwa kutoka nchi za Kiarabu na Kiislamu katika Mashariki ya Kati, Afrika Kaskazini na Ghuba la Kiajemi; na (B) Kutilia maanani hasara za Wayahudi, Wakristo, na makundi mengine yenye watu wachache kama matokeo ya migogoro ya Kiarabu na Kiisraeli. S. Res. 85

Maazimio haya yalijadiliwa mnamo tarehe 19 Julai, mwaka wa 2007 katika mkutano wa nyumba mbili za Bunge za Haki za Binadamu zilipojiandaa kupiga kura.

Wakimbizi wa Kiafrika nchini Israeli[hariri | hariri chanzo]

Tangu mwaka wa 2003, takriban wahamiaji 10,000 wasiokuwa Wayahudi kutoka nchi mbalimbali za Kiafrika wameingia nchini Israeli kinyume cha sheria.[50] Takriban wakimbizi 600 kutoka kanda ya Darfur ya Sudan wamepewa hadhi ya ukimbizi. Wakimbizi wengine 2,000 kutokana na vita kati ya Eritrea na Ethiopia wamepewa ruhusa ya kuwa wakazi kwa muda kwa misingi ya kibinadamu. Nchi ya Israeli haipendi kuwatambua kama wakimbizi kwa hofu ya kuziaibisha nchi za Eritrea na Ethiopia.[50] Wahamiaji waliosalia wanaishi nchini Israeli kinyume cha sheria. Mnamo mwaka wa 2007, Israeli iliwafukuza wakimbizi 48 hadi Misri baada ya wao kufanikiwa kuuvuka mpaka, ishirini kati yao walifukuzwa hadi nchi ya Sudan na serikali ya Misri, kwa mujibu wa Shirika la Kimataifa la Msamaha. Mnamo mwezi Agosti mwaka wa 2008 Wanajeshi wa Ulinzi wa Israeli waliwafukuza nchini watafuta hifadhi wengine 91 wa Kiafrika mpakani. Katika kipindi chote cha mwaka huu, polisi wa Kimisri wamewapiga risasi na kuwauwa angalau watafuta hifadhi 20 wa Kiafrika waliokuwa wakijaribu kuingia Israel.[51]

Wakimbizi wa Kirohingya nchini Bangladesh kutoka Burma[hariri | hariri chanzo]

Bangladesh huwa makao ya zaidi ya wakimbizi 250,000 Waislamu wa Kirohingya waliolazimishwa kutoka magharibi mwa Burma (Myanmar) walipokimbia kati ya miaka ya 1991-1992 ili kuyaepuka mateso ya majeshi ya Kiburma. Wengi wameishi hapo kwa karibu miaka ishirini. Serikali ya Kibangladeshi inawagawanya wakimbizi wa Kirohingya katika makundi mawili - wakimbizi wanaotambulika na wanaoishi katika kambi rasmi na wakimbizi wasiotambulika na wanaoishi katika maeneo yasiyokuwa ya kirasmi au miongoni mwa jamii za Kibangladeshi.

Wapatao wakimbizi 30,000 wa Kirohingya ni wakazi wa kambi mbili katika maeneo ya Nayapara na Kutupalong ya Cox, Wilaya ya Bazar nchini Bangladesh. Wakazi wa kambi hizi wanapata huduma za msingi, walioko nje hawapati huduma hizo. Mabadiliko nchini Burma bado yakiwa mbali, lazima Bangladesh iyafahamu mahitaji ya kipindi kirefu ya wakimbizi wote wa Kirohingya nchini, na kuyaruhusu mashirika ya kimataifa kupanua huduma ambazo zitafaidi Warohingya na vilevile jamii. Shirika la Umoja wa Mataifa la Wakimbizi, UNHCR limekuwa likiwabagua wakimbizi wa Kirohingya kutoka nchini za Burma na Bangladesh.

Shirika hilo limekuwa likiwasaidia wakimbizi wa Kirohingya wanaoishi katika makambi. Kwa upande mwingine, shirika hilo halipokei maombi kwa ajili ya hadhi ya ukimbizi kutoka Warohingya wanaowasili upya. Jambo hili linaashiria kuwa shirika hilo linayakiuka mamlaka yake. Kampeni ya kikatili ya utakaso wa kikabila wa Waislamu katika Jimbo la Arakan IliYofanywa na majeshi ya Kiburma katika kipindi cha miaka ya 1991 na 1992 umesababisha maelfu ya watu wazuiliwe katika makambi ya wakimbizi nchini Bangladesh na makumi ya maelfu kurudishwa makwao ambapo watakandamizwa zaidi. Madai mengi ya mateso ya kidini yameenea, kutumikishwa kufanya kazi ya lazima na kunyimwa uraia wa Warohingya wengi waliolazimishwa kurudi Burma tangu mwaka wa 1996.

Wengi wamekimbia tena hadi Bangladeshi kutafuta kazi au makao, au kukimbia uonevu unaotendwa dhidi yao na jeshi la Burma, na baadhi yao wanalazimishwa na vikosi vya usalama vya Burma kuivuka mipaka. Katika miezi michache iliyopita, dhuluma dhidi ya Warohingya katika Jimbo la Arakan imeendelea, ikijumuisha sheria kali za usajili zinazozidi kuwanyima Warohingya uraia, vikwazo vya kutembea, unyakuzi wa ardhi na kuondolewa kutoka ardhi kwa lazima ili kutayarisha njia kwa makazi ya Waburma wa Kibudha, kukithiri kwa kutumikishwa kufanya kazi ya lazima katika miradi miundombinu na kufungwa kwa baadhi ya misikiti, tisa ikihesabika katika kijiji cha Buthidaung ya Kaskazini cha jimbo la Arakan Magharibi katika nusu ya mwisho wa mwaka wa 2006.[52][53][54]

Wakimbizi kutoka Vita vya Aljeria[hariri | hariri chanzo]

Vita vya kupigania Uhuru vya Aljeria (1954-1962) viliwang'oa zaidi ya Waalijeria milioni 2, ambao walilazimishwa kuhamia makambi ya kifaransa au kukimbia hadi nchi ya Morocco, Tunisia, na mikoa ya ndani ya Aljeria.

Wakazi wenye asili ya Ulaya, Pieds-Noirs kwa lugha ya Kifaransa, walijumuisha 10.4% ya idadi jumla ya watu wa Aljeria mnamo mwaka wa 1962. Katika miezi michache tu mnamo mwaka wa 1962, 900,000 kati yao walikimbia nchi hiyo, idadi hiyo ikiwa ndiyo idadi kubwa zaidi ya watu kuhamishwa hadi nchini Ulaya tangu Vita Vikuu vya Pili vya Dunia. Msemo uliotumika katika propaganda ya shirika la FLN likitaja jamii ya Pied-noirs ulikuwa "sanduku au jeneza" ("La valise ou le cercueil" kwa lugha ya Kifaransa).[55][56]

Yordani[hariri | hariri chanzo]

Yordani ina mojawapo ya idadi ukubwa zaidi duniani ya wahamiaji huku baadhi ya vyanzo vikidadisi asilimia ya wahamiaji kuwa 60%. Kuelewana kwa dini mbalimbali nchini Yordani, utulivu wa kisiasa, na mafanikio ya kiuchumi umefanya Yordani kuwavutia wale wanaokimbia vurugu na mateso. Yordani pia ina ubora wa maisha wa juu ikilinganishwa na nchi nyingine katika kanda na ikiwa na kiwango kikubwa cha watu wanaoweza kusoma, miundombinu bora ya afya, na mazingira huru ya kijamii na kiuchumi. Yordani ina idadi kubwa ya wahamiaji. Wakimbizi wa Kipalestina hujumuisha karibu nusu ya idadi ya wakazi wa Yordani, hata hivyo wametangamana na jamii ya Kiyordani. Idadi ya wakimbizi kutoka Irak ni kati ya 750,000 na milioni 1 wengi wao wakiishi mjini Amman. Yordani pia ina watu wachache wa Kiarmeni, Kichechen, na Kikirikassa.

Lebanon[hariri | hariri chanzo]

Inakadiriwa kuwa takriban watu 900,000, wanaowakilisha humusi moja ya idadi ya watu kabla ya vita, walilazimishwa kuyahama makazi yao wakati wa Vita vya Wenyewe kwa Wenyewe vya Lebanon (1975-90).[57]

Vita vya mwaka 2006 vya Lebanon viliwaacha Walebanoni takriban milioni moja [58] na Waisraeli takriban 500,000, bila makao ingawa wengi wao mwishowe waliweza kurudi makwao.[59]

Hamu ya Walebanoni kuhamia nchi zingine imeongezeka tangu mwanzo wa vita. Zaidi ya humusi moja ya Washia, robo moja ya Wasunni, na karibu nusu ya Wamaronaiti wameonyesha hamu ya kutaka kuondoka nchini Lebanon. Karibu theluthi moja ya Wamaronaiti kama hao tayari wamewakilisha maombi yao ya viza kwa mabalozi ya kigeni, na Wakristo wengine 60,000 tayari wamekimbia kutoka Lebanon, tangu Aprili mwaka wa 2007. Wakristo wa Kilebanoni wana wasiwasi kwamba ushawishi wao unapungua, wanaogopa kupanda dhahiri kwa Uislamu haramu, na wana wasiwasi kuhusu uwezekano wa uhasama dhidi ya Wasunni na Washia.[60]

Sahara ya Magharibi[hariri | hariri chanzo]

Inakadiriwa kuwa zaidi ya Wasahrawi 150,000 - watu kutoka eneo linalopiganiwa la Sahara ya Magharibi - wameishi katika makambi matano ya wakimbizi karibu na Tindouf katika sehemu ya Algeria ya Jangwa la Sahara tangu mwaka wa 1975.[61][62] Ubalozi wa Umoja wa Mataifa wa Wakimbizi na Shirika la Kimataifa la Chakula (WFP kwa lugha ya Kiingereza) hivi sasa yanahusika katika kusaidia wanachokitaja kuwa "wakimbizi 90,000 wanaoishi katika mazingira magumu zaidi", bila kutoa makisio ya jumla ya idadi ya wakimbizi.[63]

Nagorno Karabakh[hariri | hariri chanzo]

Mgogoro wa Nagorno Karabakh umesababisha watu 528,000 kufukuzwa kutoka makazi (takwimu hii haijumuishi watoto wanaozaliwa kwa watu hawa waliokimbia makazi yao) Waazerbaijani kutoka Armenia walinyakua maeneo mengi ikiwemo Nagorno Karabakh, Waazeri 220,000 na Wakurdi 18,000 walikimbia kutoka Armenia hadi nchi ya Azerbaijan tangu mwaka wa 1988 hadi mwaka wa 1989.[64] Watu 280,000 - karibu watu wote wa kabila la Kiaarmeni - walikimbilia Azerbaijan wakati wa vita vya kati ya mwaka 1988 na mwaka 1993 kuhusu kanda iliyozozaniwa ya Nagorno-Karabakh.[65] Wakati Azerbaijan na Armenia hatimaye zilikubali kusitisha mapigano mnamo mwaka wa 1994, takriban watu 17,000 walikuwa wameuawa, 50,000 walikuwa wamejeruhiwa, na zaidi ya milioni kuachwa bila makao.[66]

Uturuki[hariri | hariri chanzo]

Kati ya miaka ya 1984 na 1999, PKK na Majeshi ya Uturuki yalipigana vita, na idadi ya watu ilipungua katika maeneo mengi ya mashambani katika sehemu ya kusini-mashariki, huku raia wa Kikurdi wakihamia vituo vyenye usalama kama vile Diyarbakir, Van, na Şırnak, na pia kuelekea miji ya magharibi mwa Uturuki na hata magharibi mwa Ulaya. Sababu ya idadi ya watu kupungua ilikuwa mauaji ya PKK yaliyotendwa dhidi ya koo za Kikurdi walizoshindwa kudhibiti, umaskini wa eneo la kusini-mashariki, na oparesheni za kijeshi za nchi ya Uturuki.[67] Shirika la Kulinda Haki za Binadamu lina kumbukumbu ya matukio mengi ambapo majeshi ya Kituruki yaliwafukuza wakazi wa vijiji kwa lazima, huku yakiharibu nyumba na vifaa ili kuzuia wenyeji hao kurudi. Takriban vijiji 3,000 vya Kikurdi viliharibiwa, vikiwakilisha kufukuzwa kwa watu 378,000 kutoka makazi yao.[68][69][70][71]

Wakimbizi kutoka vita vya Irak[hariri | hariri chanzo]

Vita vya Iran na Irak kati ya mwaka wa 1980 hadi mwaka wa 1988, Irak kuivamia Kuwait mnamo mwaka wa 1990, Vita vya Kwanza vya Ghuba na migogoro ya baadaye yote ilisababisha kuongezeka kwa mamia ya maelfu kama sio mamilioni ya wakimbizi. Iran pia ilitoa hifadhi kwa wakimbizi 1,400,000 wa Kiirak waliokuwa wameng'olewa kutoka makwao kutokana na Vita vya Ghuba ya Kiajemi (1990-91). Angalau Wakurdi milioni moja wa Irak walipoteza makazi yao wakati wa Kampeni ya Al-Anfal (1986-1989).

Vita vinavyoendelea vya Irak vimeongeza mamilioni ya wakimbizi na watu waliotimuliwa kutoka makazi yao. Tangu 2007 Wairaki ndio watu wengi zaidi waliopoteza makazi yao na kuwa wakimbizi kuliko wakazi wa nchi yoyote. Zaidi ya watu 4,700,000, zaidi ya 16% ya wakazi wa Irak, wameng'olewa kutoka makwao.[72] Kati ya hawa, karibu milioni 2 wamekimbia Irak na kujaza nchi zingine, na inakadiriwa kuwa milioni 2.7 ni wakimbizi nchini Irak, huku karibu Wairaki 100,000 wakikimbia na kuingia nchi za Syria na Yordani kila mwezi.[73][74][75] Ni 1% ya jumla pekee ya wakazi wote wa Irak waliopoteza makazi inayokadiriwa kuishi katika nchi za Magharibi.[76]

Takriban 40% ya Wairaki wa daraja la kati wanaaminika kukimbia, Umoja wa Mataifa umesema. Wengi wao wanatoroka kwa sababu ya utaratibu wa mateso na hawana nia ya kurudi. Kila aina ya watu, kutoka wahadhiri wa vyuo vikuu hadi waokaji, wamelengwa na wanamigambo, wapiganaji na wahalifu. Takriban waalimu wa shule 331 waliwawa katika miezi minne ya kwanza ya mwaka wa 2006, kulingana na Shirika la Ulinzi wa Haki za Kibinadamu, na angalau madaktari 2,000 wa Kiiraki wameuawa na 250 kutekwa nyara tangu uvamizi wa Marekani wa mwaka 2003.[77] Wakimbizi wa Irak nchini Syria na Yordani huishi katika jamii maskini ambapo hawasaidiwi vilivyo na nchi za kimataifa ili kupunguza shida zao na ambapo wanapata ulinzi mdogo sana wa kisheria.[78] Nchini Syria pekee inakadiriwa kuwa wasichana na wanawake 50,000 wa Kiiraki, wengi wao wajane, wanalazimishwa kufanya ukahaba ili wajipatie riziki.[79][80]

Kulingana na Shirika la Kimataifa la Wakimbizi lenye makao yake mjini Washington, kati ya wakimbizi milioni 4.2 wachache kuliko 800 wameruhusiwa kuingia Marekani tangu uvamizi wa 2003. Uswidi imewakubali 18,000 na Australia imewapa wakimbizi takriban 6,000 makao mapya.[81] Kufikia mwaka wa 2006 Uswidi ilikuwa imewapa ulinzi wakimbizi wengi kuliko nchi zote za Ulaya kwa jumla. Hata hivyo, kufuatia wito ambao hukujibiwa kwa wanachama wenzake wa Ulaya wa kushikamana zaidi, Mnamo Julai 2007 Uswidi ilianzisha sera kali zaidi kwa watafuta hifadhi wa Kiiraki, sera ambayo inatarajiwa kupunguza kiwango cha utambuzi mnamo mwaka wa 2008.[82]

Tangu Septemba mwaka wa 2007 Syria iliamua kutekeleza mpango mkali wa utoaji viza ili kupunguza idadi ya Wairaki waliokuwa wakiingia nchini humo kwa idadi ya takriban 5,000 kila siku. Kufanya hivyo kulikata njia ya kipekee ya kutoroka ya maelfu ya wakimbizi waliokuwa wakikimbia vita vya wenyewe kwa wenyewe nchini Irak. Amri ya serikali ambao ilianza kutekelezwa mnamo tarehe 10 Septemba, mwaka wa 2007 inakataza wamiliki pasipoti wa Kiiraki kuingia nchini Syria isipokuwa wale ambao ni wafanyabiashara na wasomi. Kabla ya wakati huo, Syria ilikuwa nchi pekee iliyokuwa imepinga kanuni kali dhidi ya kuwakubali wakimbizi wa Kiiraki kuingia.[83][84]

Makundi ya kidini yenye watu wachache zaidi katika eneo la Mashariki ya Kati[hariri | hariri chanzo]

Ingawa Wakristo Waashuru wanawakilisha chini ya 5% ya idadi ya wakazi wa Irak, wao hujumuisha 40% ya idadi ya watu wanaokimbia Irak, kwa mujibu wa Ubalozi wa Umoja wa Mataifa wa Wakimbizi.[85][86] Katika karne ya 16, Wakristo walikuwa nusu ya wakazi wote wa Irak.[87] Mwaka wa 1987, sensa ya mwisho ya Irak ilipofanywa, Wakristo milioni 1.4 walihesabiwa.[88] Lakini kwa sababu vita vya sasa vimeongeza uhasama wa Waislamu, idadi ya Wakristo imeshuka hadi takriban 500,000, ambao wapatao 250,000 wanaishi mjini Baghdad.[89]

Isitoshe, jamii ndogo za Wamandayo na Wayazidi zinakabiliana na hatari ya kuangamizwa kutokana na utakaso wa kikabila unaofanywa na wanamgambo wa Kiislamu.[90][91] Vitongoji vizima mjini Baghdad vilitakaswa kikabila na wanamgambo wa Kishia na wa Kisunni.[92][93] Picha za setelaiti zinaonyesha kuwa utakaso wa kikabila nchini Irak ulikuwa sababu muhimu ya mafanikio "kuongezeka".[94]

Msimamo wa serikali ya Marekani kuhusu wakimbizi ni kwamba kuna ukandamizaji wa makundi ya kidini yenye watu wachache katika eneo la Mashariki ya Kati na nchini Pakistan hasa Wakristo, Wahindu, na vilevile madhehebu ya Kiislamu ya Ahmadiya na Zikri. Nchini Sudan ambapo Uislamu ndiyo dini rasmi ya nchi, Waislamu hushikilia wadhifa mkubwa serikalini na wao hudhibiti shughuli za Wakristo, wafuasi wa dini za jadi za kiasili za Kiafrika na wengine wasiokuwa Waislamu [8]. Suala la wakimbizi wa Kiyahudi, wa Kikristo na wengineo kutoka nchi za Kiarabu na Kiislamu liliwasilishwa mnamo Machi mwaka wa 2007 mbele ya Bunge la Marekani [9][dead link].

Katika Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, Wakristo wachache wananchi wanalalamikia ukosefu wa uhuru wa dini katika nchi za Kiislamu zenye wafuasi wachache [95], huku Wabahá'í vilevile wakiyakimbia mateso ya kidini [96].

Kuhama kwa wakimbizi Barani Asia[hariri | hariri chanzo]

Afghanistan[hariri | hariri chanzo]

Tangu Urusi ivamie nchi ya Afghanistan mnamo mwaka wa 1979 hadi miaka ya mapema 1990, Vita vya Afghanistan (1978-92) vilisababisha zaidi ya wakimbizi milioni sita kukimbia kuelekea nchi jirani za Pakistan na Iran, na kuifanya Afghanistan iwe nchi yenye kuzalisha wakimbizi wengi zaidi duniani. Katika kilele cha Afghanistan kuvamiwa na Wasovyeti, takriban wakimbizi milioni saba wa Kiafghanistani walikimbilia usalama nchini Pakistan, hivyo kuifanya Pakistan nchi ya kipekee kuwahi kuwa na idadi kubwa kama hiyo ya wakimbizi.

Idadi ya wakimbizi ilipanda na kushuka kulingana na mawimbi ya vita, huku maelfu zaidi wakikimbia baada ya kundi la Taliban kuyachukua mamlaka mnamo mwaka wa 1996. Uvamizi wa Marekani wa nchi ya Afghanistan mnamo mwaka wa 2001 na utakaso wa kikabila uliondelea na ghasia za kikabila pia zilisababisha watu zaidi kuyapoteza makazi yao. Ingawa wachache wamerudishwa makwao, mpango uliofadhiliwa na Umoja wa Mataifa kutoka Iran hadi Pakistan, sensa ya mwaka 2007 ya Ubalozi wa Umoja wa Mataifa wa Wakimbizi ilitambua zaidi ya wakimbizi milioni mbili ambao bado walikuwa wakiishi nchini Pakistan pekee.

Tangu mwezi Februari mwaka wa 2007, Iran ilikuwa nchi nyumbani kwa wakimbizi 915,000 wa Kiafghani na wakimbizi 54,000 wa Kiiraki.[97] Mnamo mwaka wa 2002, Ubalozi wa Umoja wa Mataifa wa Wakimbizi ulianza mpango wa hiari wa kuwarudisha Waafghanistani nyumbani.[97] Tangu mwishoni mwa Aprili mwaka wa 2007, serikali ya Iran imewarudisha wakimbizi ambao hawajasajiliwa (na wachache waliosajiliwa) waliokuwa wakiishi na kufanya kazi nchini Iran kwa lazima hadi Afghanistan. Kuwarudisha wakimbizi hao nyumbani kwa nguvu, huku wengi wao wakiwa wameishi nchini Iran na Pakistan kwa muda wa karibu miongo mitatu, ni sehemu ya mipango kubwa ya nchi hizi mbili za kuwarudisha wakimbizi wote wa Kiafghanistan makwao. Wataalam wanasema mpango huu utakuwa 'janga' kwa nchi ya Afghanistan.[98][99] Waafghanistan 362,000 walifukuzwa kutoka nchini humo mnamo mwaka wa 2008 .[100]

Ugawaji wa 1947[hariri | hariri chanzo]

Ugawaji wa Bara ndogo la Uhindi ili kuunda nchi za India na Pakistan mnamo mwaka wa 1947 ulisababisha kuhama kukubwa zaidi kwa binadamu kihistoria: ubadilishanaji wa Wahindu na Wakalasinga 18,000,000 (65% kutoka Bangladesh na 35% kutoka Pakistan) na Waislamu (kutoka India). Wakati wa kipindi cha Vita ya Ukombozi vya Bangladesh vya mwaka wa 1971, kutokana na vita vya wenyewe kwa wenyewe nchini Bangladesh (iliyofahamika apo awali kama Pakistan ya Mashariki) na Oparesheni tafuta-taa, zaidi ya Wabangladeshi milioni kumi waliokuwa wazungumzaji wa lugha ya Kibengali walikimbilia nchi jirani ya Uhindi .

Wakimbizi wa Kibangladeshi nchini Uhindi mnamo mwaka wa 1971[hariri | hariri chanzo]

Kama matokeo ya Vita vya Ukombozi vya Bangladesh, mnamo tarehe 27 Machi mwaka wa 1971, Waziri Mkuu wa India, Indira Gandhi, alionyesha kuunga mkono kamili kwa serikali yake kwa mapambano ya Kibangladeshi ya uhuru. Mpaka wa Bangladesh na Uhindi ulifunguliwa ili kuwapa Wabangladeshi walioadhirika kivita makao salama nchini Uhindi. Serikali za Bengal Magharibi, Bihar, Assam, Meghalaya na Tripura zilianzisha makambi ya wakimbizi mpakani. Maafisa wa jeshi la Kibangladeshi waliokuwa uhamishoni na jeshi la Uhindi mara moja walianza kutumia makambi haya kwa ajili ya kuwaajiri na kuwafunza wanachama wa Mukti Bahini. Wakati wa Vita vya Uhuru vya Bangladesh takriban Wabangladeshi milioni 10 walikimbia nchi kuepuka mauaji na mateso ya kinyama waliyotendewa na Jeshi la Pakistan. Wakimbizi wa Kibangladeshi wanajulikana kama "Chakmas"' nchini India.

Maeneo ya Himalaya[hariri | hariri chanzo]

Baada ya msafara wa kutoka wa Watibeti wa mwaka 1959, kuna zaidi ya Watibeti 150,000 wanaoishi nchini Uhindi, wengi katika makazi katika Dharamsala, Mysore, na Nepal. Hawa ni pamoja na watu ambao wamekimbia kwa kuikwea milima ya Himalaya wakitoroka eneo la Tibet, wakiwa na watoto wao na wajukuu wao. Nchini Uhindi idadi kuu ya Watibeti wanaozaliwa nchini humo bado hawana uraia na wao hubeba hati iitwayo Kadi ya Utambulisho inayotolewa na serikali ya Uhindi badala ya pasipoti. Waraka huo unasema kuwa uraia wa mtu mwenye kuubeba waraka ni wa Kitibeti. Ni waraka huo ambao mara nyingi hukataliwa kama hati halali ya kusafiri katika idara nyingi za forodha na uhamisho. Wakimbizi wa Kitibeti pia humiliki Kitabu cha Kijani Kibichi kinachotolewa na Serikali ya Tibet Uhamishoni kwa haki na wajibu kuelekea utawala huu.

Kati ya mwaka 1991 na mwaka wa 1992, Bhutan iliwafukuza takriban watu 100,000 wa kabila la Kinepali wenye asili ya nchi ya Nepal, wengi ambao wamekuwa wakiishi katika makambi saba ya wakimbizi katika Nepal mashariki tangu wafukuzwe. Mnamo mwezi Machi mwaka wa 2008, idadi hii ilianza kupewa makazi ya kudumu miaka mingi katika nchi tatu zikiwemo Marekani, New Zealand, Udenimaki na Australia. Kwa sasa, Marekani inajibidiisha kuwapa makao mapya zaidi ya wakimbizi 60,000 kati yao nchini Marekani kama harakati ya kuwapa makazi katika nchi ya tatu.[101]

Wakati uo huo, ipatao Wanepali 200,000 walipoteza makao wakati wa ukereketwa wa Kimao na Vita vya Wenyewe kwa Wenyewe vya Nepali vilivyomalizika mnamo mwaka wa 2006.

Zaidi ya raia wa Kipakistani milioni 3 wameyakimbia makazi yao baada ya Vita katika eneo la Kaskazini-Magharibi la Pakistan (tangu mwaka 2004-hadi wa leo) kati ya serikali ya Kipakistan na wanamigambo wa Kitaliban.[102]

Watamil wa Sri Lanka[hariri | hariri chanzo]

Vita vya wenyewe kwa wenyewe nchini Sri Lanka (tangu mwaka wa 1983 hadi mwaka wa 2009) vimefanya mamilioni kukimbia makazi na wengine kufanywa kuwa wakimbizi. Watamil wa Kisiri Lanka wametoroka hadi Uhindi, Ulaya (hasa Ufaransa, Udenmaki, Uingereza, na Ujerumani), na Kanada (zaidi ya watu 103,625).

Kashmir[hariri | hariri chanzo]

Wakashmiri takriban milioni moja wa Kiislamu wanaoishi katika sehemu ya Kashmir inayosimamiwa na Uhindi walikimbilia Kashmir inayosimamiwa na Pakistan kwa hofu ya kutendewa mauaji ya kimbari mikononi mwa jeshi la Uhindi lililotumwa pale kukabiliana na harakati ya utengano ya tangu mwaka 1988. Wahindu Wakashmiri wa Kipandit takriban 300,000 (makisio ya upeo wa chini) wamehamishwa makazi yao kutoka Kashmir na mashirika ya utengano ya Kipakistan. Kulingana na Tume ya Taifa ya Haki za Binadamu, Wakashmiri wa Kipandit takriban 300,000 wamelazimika kuondoka Kashmir. Lakini makundi ya Kikashmiri yanadadisi kuwa idadi ya wahamiaji inakaribia 500,000.[103]

Vita vya Wenyewe kwa Wenyewe vya Tajikistan[hariri | hariri chanzo]

Tangu mwaka wa 1991, kiasi kikubwa cha idadi ya watu nchini humo ambao si Waislamu, ikiwemo Warusi wa Wayahudi wamekimbia Tajikstan kwa sababu ya umaskini mwingi, ukosefu wa usalama, na Vita vya Wenyewe kwa Wenyewe vya Tajikistan (1992-1997).[104] Mnamo mwaka wa 1992, kiasi kikubwa cha watu wa Kiyahudi nchini humo walihamishwa hadi Israeli.[105] Na vita vya wenyewe kwa wenyewe vilipokwisha, Tajikistan ilikuwa katika hali ya kusambaratika. Takriban watu milioni 1.2 walikuwa wakimbizi ndani na nje ya nchi.[106]

Uzbekistan[hariri | hariri chanzo]

Mnamo mwaka wa 1989, baada ya mashambulizi makali dhidi ya Waturuki wa Kimeskhetian katika Bonde la Ferghana la Asia ya Kati, karibu Waturuki 90,000 wa Kimeskhetian walikimbia nchi ya Uzbekistan.[107][108]

Asia ya Kusini-mashariki (Vita vya Vietnam)[hariri | hariri chanzo]

Kufuatia wakomunisti kuyachukua mamlaka katika nchi za Vietnam, Cambodia, na Laos mnamo mwaka wa 1975, takriban watu milioni tatu walijaribu kutoroka katika miongo iliyofuata. Kadiri wakimbizi wengi walivyofurika kila siku, ndivyo rasilimali za nchi zilizowapokea zilivyozidi kuwa chache. Taabu za watu wa meli ikawa shida kuu ya kimataifa ya kibinadamu. Ubalozi wa Umoja wa Mataifa wa Wakimbizi (UNHCR kwa lugha ya Kiingereza) ulijenga makambi ya wakimbizi katika nchi jirani ili kufanya mchakato wa watu wa meli. Bajeti ya Ubalozi wa Umoja wa Mataifa wa Wakimbizi iliongezeka kutoka dola milioni 80 mnamo mwaka wa 1975 hadi dola milioni 500 mnamo mwaka wa 1980. Kwa kazi yake katika eneo la Indochina, Ubalozi wa Umoja wa Mataifa wa Wakimbizi ulipatiwa tuzo ya Amani la Nobel mnamo mwaka wa 1981.

  • Idadi kubwa ya wakimbizi wa Kivietinamu ilitokea baada ya 1975 wakati ambapo Vietnam ya Kusini ilinyakuliwa na vikosi vya kikomunisti. Wengi walijaribu kutoroka, baadhi yao wakitumia meli, hivyo kuanzisha utumizi wa maneno "watu wa meli." Wakimbizi wa Kivietinamu walihama hadi Hong Kong, Ufaransa, Marekani, Kanada, Australia, na nchi nyinginezo, ambapo waliunda jamii kubwa za wataalam kutoka nchi geni, hasa nchini Marekani.
  • Waathirika wa utawala wa Khmer Rouge nchini Cambodia walikimbia na kuvuka mpaka ambapo waliingia nchi ya Thailand baada ya uvamizi wa Kivietinamu wa 1978-79. Takriban watu 300,000 kati ya hawa hatimaye walipewa makao mapya nchini Marekani, Ufaransa, Kanada, na Australia kati ya mwaka wa 1979 na mwaka 1992, wakati makambi yalifungwa na watu waliobaki kurudishwa makwao.
  • Takriban Walao 400,000 walikimbilia Thailand baada ya Vita vya Vietnam na Wakomunisti kuyachukua mamlaka mnamo mwaka wa 1975. Baadhi yao walitoroka kwa sababu ya mateso yenye misingi ya kidini au kikabila waliyotendewa na serikali. Wengi wao walikimbia kati ya mwaka wa 1976 na mwaka wa 1985 na kuishi katika makambi ya wakimbizi mpakani mwa Thailand na Laos. Wengi wao walipata makao nchini Marekani, Kanada, Ufaransa, na Australia. Nchini Marekani wengi wao waliishi katika maeneo ya Jimbo la Washington, California, Washington DC, Texas, Virginia, na Minnesota.
  • Wamien au Wayao hivi karibuni waliishi katika eneo la Vietnam kaskazini, Laos kaskazini na kaskazini mwa Thailand. Mnamo mwaka wa 1975, vikosi vya Lao vya Kipathet vilianza kulipiza kisasi kuhusika kwa Wamien wengi kama askari katika Vita vya Kisiri nchini Laos vilivyodhaminiwa na Shirika la Ujasusi la Marekani (CIA katika lugha ya Kiingereza). Kama ishara ya shukrani kwa watu wa Kihmong na Kimien waliokuwa wanachama wa jeshi la kisiri la Shirika la Ujasusi la Marekani. Marekani iliwakubali wengi wao kama wakimbizi na kuwafanya kuwa raia wa Kimarekani (Wamien wa Kimarekani). Wahmong wengi zaidi wanaendelea kutafuta hifadhi katika nchi jirani ya Thailand [10] Archived 25 Agosti 2009 at the Wayback Machine..
  • Kutokana na mateso ya kikabila dhidi ya Wakaren, Wakarenni na wakazi wengine wenye idadi chache ya watu nchini Burma (Myanmar) idadi kubwa ya wakimbizi wanaishi mpakani mwa Thailand katika makambi yenye takriban watu 100,000.
  • Makabila ya Kiislamu kutoka Burma, Warohingya na Waarakanisi wamekuwa wakiishi katika makambi nchini Bangladesh tangu miaka ya 1990 [11] [12].

Kuhama kwa wakimbizi barani Afrika[hariri | hariri chanzo]

Tangu miaka ya 1950, mataifa mengi barani Afrika yamekumbwa na vita vya wenyewe kwa wenyewe na vita vya kikabila, hivyo kuzalisha idadi kubwa ya wakimbizi wa mataifa na makabila mbalimbali. Mgawanyiko wa Afrika kuwa nchi mbalimbali za kikoloni za Ulaya mnamo mwaka wa 1885, ambao ulitumiwa kuunda mipaka ya mataifa yaliyopata uhuru wao upya miaka ya 1950 na 1960, imedokezwa kama sababu kuu iliyosababisha Afrika kukumbwa na mapambano mengi ya wenyewe kwa wenyewe. Idadi ya wakimbizi barani Afrika iliongezeka kutoka 860,000 mnamo mwaka wa 1968 hadi 6,775,000 kufikia mwaka wa 1992 (Kamusi elezo ya Britannica, 2004). Kufikia mwisho mwa mwaka wa 2004, idadi hiyo ilikuwa imeshuka hadi wakimbizi 2,748,400, kulingana na Ubalozi wa Umoja wa Mataifa wa Wakimbizi [13]. (takwimu hiyo haijumuishi idadi ya watu waliokimbia makazi yao, ambao hawavuki mipaka ya kimataifa na kwa hivyo hawaambatani na ufafanuzi rasmi wa mtu ambaye anafaa kuitwa mkimbizi.)

Wakimbizi wengi barani Afrika huvuka na kuingia nchi jirani ili kutafuta usalama; mara nyingi, nchi za Kiafrika ni nchi za asili za wakimbizi na nchi za hifadhi za wakimbizi wengine kwa wakati mmoja. Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, kwa mfano, ilikuwa nchi ya asili ya wakimbizi 462,203 mwishoni mwa mwaka 2004, lakini nchi ya hifadhi kwa wakimbizi wengine 199,323.

Nchi za Afrika ambapo wakimbizi 5,000 au zaidi walitoka kufikia mwisho wa mwaka 2004, zimeorodheshwa hapa kwa mpangilio wa kupungua wa idadi ya wakimbizi. (Ubalozi wa Umoja wa Mataifa wa Wakimbizi,, Jedwali ya 3.) Idadi kuu ya wakimbizi ni kutoka nchi ya Sudan na wamekimbia Vita vya Wenyewe kwa Wenyewe vya Sudan vilivyoendelea kwa kipindi kirefu kabla ya kuisha hivi majuzi na hivi karibuni mgogoro wa Darfur na wengi wao wanapatikana nchini Chad, Uganda, Ethiopia, na Kenya.

Angola[hariri | hariri chanzo]

Upinzani dhidi ya ukoloni katika kipindi cha miaka ya 1960 na 1970 mara nyingi kulisababisha misafara mikubwa ya Walowezi wenye asili ya Kiulaya kuhama bara la Afrika - hasa kutoka Afrika Kaskazini (Watu wenye asili ya Ulaya yaani "pied noirs" milioni 1.6 ),[109] kutoka nchi za Kongo, Msumbiji na Angola.[110] Kufikia miaka ya kati ya 1970, maeneo yaliyotawaliwa na Ureno barani Afrika yalikuwa yamepotea kutoka mikononi mwao, na Wareno takriban milioni moja au watu wa asili ya Kireno walihama kutoka maeneo hayo (hasa Angola ya Kireno na Msumbiji) kama wakimbizi hohehahe- yaani "retornados".[111]

Vita vya Wenyewe kwa Wenyewe vya Angola (1975-2002), mojawapo ya migogoro mikubwa zaidi na yenye kusababisha vifo vingi iliyotokana na Vita Baridi, ilitokea muda mfupi baadaye na kuenea katika nchi iliyokuwa imeanza kujitegemea upya. Takriban watu milioni moja waliuawa, milioni nne wakawachwa bila makao na wengine nusu milioni wakatoroka kama wakimbizi.[112]

Uganda[hariri | hariri chanzo]

Katika miaka ya 1970 Uganda na mataifa mengine ya Afrika Mashariki yalitekeleza sera za ubaguzi wa rangi zilizolenga wakazi wa Kiasia katika kanda hiyo. Uganda chini ya uongozi wa Idi Amin ilikuwa maarufu sana katika sera zake dhidi ya Waasia, ambazo hatimaye zilisababisha kufukuzwa na utakaso wa kikabila wa idadi chache ya watu wa Uganda waliokuwa Waasia.[113] Idadi kubwa ya Waasia 80,000 wa Uganda walikuwa Wahindi waliokuwa wamezaliwa nchini humo. Uhindi ilikuwa imekataa kuwakubali.[114] Idadi kubwa ya Wahindi waliofukuzwa hatimaye walipata makazi Uingereza, Kanada na Marekani.[115]

Mgogoro wa wakimbizi wa eneo la Maziwa Makuu[hariri | hariri chanzo]

Kambi ya wakimbizi nchini Zaire, mnamo mwaka wa 1994

Kufuatia Mauaji ya Kimbari ya Rwanda ya mnamo mwaka wa 1994, zaidi ya watu milioni mbili walikimbilia nchi jirani, hususan Zaire. Makambi ya wakimbizi baada ya hapo yalidhibitiwa na serikali ya awali na Wanamigambo wa Kihutu ambao walitumia makambi kama maeneo misingi ya kufanya mashambulizi dhidi ya serikali mpya nchini Rwanda. Hatua chache zilichukuliwa kuitatua shida hiyo na mgogoro haukuisha hadi wakati ambapo waasi walioungwa mkono na Rwanda walipowalazimisha wakimbizi kuvuka mpaka na kurudi Rwanda ndipo Vita vya Kwanza vya Kongo vilipoanza.

Darfur[hariri | hariri chanzo]

Takriban watu 2.5 milioni ambao ni karibu theluthi moja ya wakazi wa eneo la Darfur, wamelazimishwa kukimbia makazi yao baada ya mashambulizi ya wanamgambo wa Kiarabu wa Janjaweed wanaoungwa mkono na majeshi ya Sudan kutokana na mgogoro unaoendelea wa Darfur magharibi mwa Sudan.[116][117]

Kuhama kwa wakimbizi barani Ulaya[hariri | hariri chanzo]

Umoja wa Ulaya[hariri | hariri chanzo]

Umoja wa Ulaya unajaribu kuunda mfumo sawa wa uhamiaji na hifadhi kwa wakimbizi na mkakati mmoja wa kudhibiti mipaka ya nje. Hili linahusisha kuwaainisha wakimbizi wawe tofauti na wahamiaji wa kiuchumi - yaani kama wahamiaji wa kisiasa na kujumuisha aina mbalimbali kama vile wahamiaji haramu, wanaotafuta hifadhi, na wakimbizi.

Kulingana na Baraza ya Ulaya la Wakimbizi na watu walio Uhamishoni, mtandao wa mashirika yasiyokuwa ya kiserikali ya Ulaya ya kuwasaidia wakimbizi, kuna tofauti kubwa kati ya mifumo mbalimbali ya kitaifa ya hifadhi kwa wakimbizi Barani Ulaya, hivyo basi kufanya mfumo wa hifadhi wa wakimbizi kuwa kama 'bahati na nasibu' kwa wakimbizi. Kwa mfano, Wairaki ambao hukimbia nchi yao hadi Ujerumani wana uwezekano wa 85% wa kutambuliwa kama wakimbizi na wale wanaoomba hifadhi ya ukimbizi nchini Slovenia hawapati hadhi yoyote ya ulinzi.[118] Tabia inayojulikana kama 'kuhama kwa pili' inaelezea kusafiri kwa watafuta hifadhi kutoka nchi moja ya Ulaya hadi nyingine.

Nchini Ufaransa, kumsaidia mhamiaji haramu (kutoa malazi, kwa mfano) ni marufuku kwa mujibu wa sheria iliyopitishwa mnamo tarehe 27 Desemba mwaka wa 1994 [14]. Sheria hiyo ililaumiwa vikali na mashirika yasiyo ya kiserikali kama vile CIMADE na GISTI, vyama vya upinzani vya mrengo wa kushoto vyama kama vile Chama cha Kijani Kibichi na Wakomunisti, na mashirika ya kibiashara kama vile "Syndicat de la magistrature" la mahakimu .

Gazeti ya Kituruki la "Hürriyet" lilichapisha makala mnamo Julai mwaka 2004 na Mei mwaka 2006 kuhusu meli za Kigiriki za Kulinda Pwani zilizorekodiwa kupitia filamu zikiwa majini mita mia chache kutoka pwani ya Kituruki ambapo ziliwaacha wahamiaji baharini. Zoezi hili linadaiwa kusababisha kufa maji kwa watu sita kati ya Chios na Rasi ya Karaburun mnamo tarehe 26 Septemba, mwaka wa 2006 ilhali wengine watatu walipotea na 31 kuokolewa na majeshi ya wanamaji wa Kituruki na wavuvi.[119]

Sheria mpya kali ya uhamiaji ya Umoja ya Ulaya inayowaweka kizuizini wahamiaji haramu kwa hata miezi 18 kabla ya kuwarudisha nyumbani imesababisha hasira katika eneo la Marekani ya Kilatini, huku Rais wa Venezuela, Hugo Chavez akitishia kukomesha kuyauza mafuta kutoka nchi yake barani Ulaya.[120][121]

Hungaria[hariri | hariri chanzo]

Kati ya mwaka wa 1956 na mwaka wa 1957 kufuatia Mapinduzi ya Hungaria ya mwaka wa 1956 takriban watu 200,000, karibu asilimia mbili ya wakazi wa Hungaria, walikimbia kama wakimbizi nchi za Austria na Ujerumani ya Magharibi.[122]

Chekoslovakia[hariri | hariri chanzo]

Mkataba wa Warsaw wa uvamizi wa Chekoslovakia mnamo mwaka wa 1968 ulifuatiwa na wimbi la uhamiaji, ghaibu hapo awali na ambao lilikomeshwa muda mfupi baadaye (makisio: 70,000 mara moja, jumla ya 300,000),[123] kwa kawaida yalihusisha watu waliohitimu na waliohamia Austria au Ujerumani ya Magharibi.

Cyprus[hariri | hariri chanzo]

Inakadiriwa kuwa 40% ya wakazi wa Kigiriki wa nchi ya Kupro, na vilevile zaidi ya nusu ya idadi ya watu wa Uturuki wa Kisaiprasi, walipoteza makazi yao kufuatia uvamizi wa Cyprus na Waturuki mnamo mwaka wa 1974. Takwimu za Wasaiproti waliokimbia makazi ndani ya nchi zinatofautiana, Umoja wa Kikosi cha Kulinda Amani nchini Cyprus (UNFICYP) unakadiria idadi hiyo kuwa Wagiriki wa Kisaiprasi 165,000 na Waturuki wa Kisaiprasi 45,000. Ubalozi wa Umoja wa Mataifa wa Wakimbizi una takwimu za juu zaidi za 200,000 na 65,000 mtawalia, zinazotokana na takwimu rasmi za Kisaiprasi ambazo husajili watoto wa familia zisizokuwa na makazi kama wakimbizi.[124] Mgawanyiko wa jamii hizo mbili kupitia Mstari ya Kijani Kibichi unaochungwa na Umoja wa Mataifa ulipiga marufuku kurudi kwa watu wote waliokimbia makazi yao.

Eneo la Balkans[hariri | hariri chanzo]

Kufuatia Vita vya Wenyewe kwa Wenyewe vya Kigiriki (1946-1949) mamia ya maelfu ya Wagiriki na watu wa kabila la Kimasedonia walikimbia nchi. Idadi ya wakimbizi ilikuwa kati ya 35,000 kufikia zaidi ya 213,000. Zaidi ya watoto 28,000 waliokolewa kwenda nchi za Kanada ya Mashariki na Jamhuri ya Kisoshalisti ya Masedonia. Jambo hili liliwaacha maelfu ya Wagiriki na Wamesedonia wa Kiegia kuenea duniani kote.

Kampeni ya kuwafanya watu kutangamana kwa lazima ya miaka ya 1980 iliyowalenga watu wa kabila la Kituruki ilisababisha uhamiaji wa takriban Waturuki wa Kibulgaria 300,000 kuelekea nchi ya Uturuki.

Kuanzia mwaka wa 1991, mapinduzi ya kisiasa katika eneo la Balkans kama vile kuvunjika kwa Yugoslavia, kuliwaacha watu 2,700,000 bila makazi kufikia kipindi cha katikati cha mwaka wa 1992, ambapo zaidi ya 700,000 kati yao walitafuta hifadhi ya ukimbizi Barani Ulaya.[125][126] Mnamo mwaka wa 1999, takriban Waalbania milioni moja walitoroka kutoka mateso yaliyotendwa dhidi yao na Wasabia.

Hadi wa leo bado kuna maelfu ya wakimbizi na watu waliokimbia makazi yao katika eneo la Balkans ambao hawawezi kurudi makwao. Wengi wao ni Waserbia ambao hawawezi kurudi Kosovo, na ambao bado huishi katika makambi ya wakimbizi katika Serbia hadi wa leo. Zaidi ya Waserbia 200,000 na makundi mengine madogo ambayo siyo ya Kialbeni yalikimbia au yalifukuzwa kutoka Kosovo baada ya Vita vya Kosovo vya mwaka 1999.[127][128]

Wakimbizi na watu waliofurushwa kutoka makwao nchini Serbia ni kati ya 7% na 7.5% ya wakazi wake - karibu nusu milioni ya wakimbizi walikimbia nchini humo kufuatia mfululizo wa Vita vya Yugoslavia (hasa kutoka Kroatia, na wachache kutoka Bosnia na Herzegovina pia na watu waliofurushwa kutoka Kosovo, ambao ndio wengi zaidi idadi yao ikizidi 200,000).[129] Serbia ina idadi kuu ya wakimbizi barai Ulaya.[130]

Chechnya[hariri | hariri chanzo]

Tangu mwaka wa 1992 kumekuwa na mgogoro katika eneo la Caucasus la Chechnya kutokana na uhuru uliotangazwa na jamhuri hii mnamo mwaka wa 1991 ambayo haikubaliki na Shirikisho la Kirusi au taifa lingine lolote duniani. Kama matokeo, takriban watu milioni 2 wameyakimbia makazi yao na bado hawawezi kurejea makwao. Miaka ya Kisovyeti ilipoisha, watu wa kabila la Kirusi walikuwa takriban 23% ya idadi ya watu (269,000 mnamo mwaka wa 1989). Kutokana na kuenea kwa uasi na utakaso wa kikabila chini ya serikali ya Dzhokhar Dudayev watu wengi ambao hawakuwa Wachechenia (na Wachechenia wengi vilevile) walikimbia nchi hiyo katika miaka ya 1990 au kuuawa.[131][132]

Georgia[hariri | hariri chanzo]

Kuhamishwa kutoka makazi yao kwa lazima na utakaso wa kikabila wa zaidi ya watu 250,000, wengi wao Wajojia lakini baadhi yao wa makabila mengine pia, kutoka eneo la Abkhazia wakati wa vita na baadaye katika miaka ya 1993 na 1998.[133]

Kama matokeo ya Vita vya Ossetia Kusini vya 1991-1992, takriban watu 100,000 wa kabila la Kiossetia walikimbia kutoka eneo la Ossetia Kusini na Georgia yenyewe, wengi wakivuka mpaka na kuingia Ossetia ya Kaskazini. Watu wengine wa kabila la Kijojia 23,000 walikimbia Ossetia ya Kusini na kufanya makazi katika maeneo mengine ya Georgia.[134]

Umoja wa Mataifa umekadiria kuwa Wajojia 100,000 wamelazimishwa kuhama kama matokeo ya Vita vya Ossetia Kusini vya mwaka 2008; Takriban wakazi 30,000 wa Ossetia Kusini walikimbilia jimbo jirani la Kirusi la Ossetia Kaskazini.[135]

Kuhama kwa wakimbizi katika maeneo ya Amerika[hariri | hariri chanzo]

Zaidi ya Wasalvadori milioni moja walifukuzwa kutoka makazi yao wakati wa Vita vya Wenyewe kwa Wenyewe vya Kisalvadori kati ya mwaka 1975 na mwaka 1982. Karibu nusu yao walikwenda Marekani, wengi wakifanya makao katika eneo la Los Angeles. Pia kulikuwa na msafara mkubwa wa Waguatemala uliotoroka Vita vya Wenyewe kwa Wenyewe na pia mauaji ya kimbari katika miaka ya 1980. Watu hawa walikwenda Kusini mwa Meksiko na Marekani

Kati ya mwaka 1991 hadi mwaka 1994, kufuatia mapinduzi ya kijeshi dhidi ya Rais Jean-Bertrand Aristide, maelfu ya Wahaiti walikimbia vurugu na ukandamizaji kupitia meli. Ingawa wengi walirudishwa nchini Haiti na serikali ya Marekani, wengine waliingia Marekani kama wakimbizi. Wahaiti walionekana haswa kama wahamiaji wa kiuchumi kutoka umaskini uliokidhiri nchini Haiti, ambalo ndilo taifa lenye umaskini mwingi zaidi katika ulimwengu wa Magharibi.

Ushindi wa vikosi vilivyoongozwa na Fidel Castro katika Mapinduzi ya Cuba ulisababisha msafara mkubwa wa Wakiuba kutoka nchini humo kati ya mwaka wa 1959 na 1980. Wakiuba wengi kila mwaka huendelea kuyahatarisha maisha yao kuvuka hadi eneo la pwani ya Florida wakitafuta maisha bora ya kiuchumi na kisiasa nchini Marekani. Mnamo mwaka wa 1999 kesi iliyoangaziwa sana habarini ya mvulana wenye umri wa miaka sita, Elián González, iliupa uhamiaji wa kisiri kipaumbele kimataifa. Hatua za serikali zote mbili zimejaribu kushughulikia suala hilo; Marekani ilianzisha sera ya miguu yenye maji na, miguu mikavu kuruhusu kimbilio kwa wale wasafiri ambao wanafaulu kukamilisha safari yao, na serikali ya Cuba imeruhusu mara kwa mara uhamiaji uliopangwa. Maarufu zaidi kati ya uhamiaji wa aina hii ni ule wa safari ya meli ya Mariel ya 1980.

Kolombia ina mojawapo ya idadi kubwa dunia ya watu waliokimbia makazi yao, na makadirio ni kati ya watu milioni 2.6 na 4.3, kutokana na mgogoro unaoendelea wa Kisilaha wa Kolombia. Takwimu ya upeo wa juu ni ya kuongeza idadi ya wakimbizi tangu mwaka wa 1985.[136][137] Hivi sasa inakadiriwa na [Kamati ya Wakimbizi na Wahamiaji ya Marekani] kwamba kuna Wakolombia 150,000 katika "hali kama za ukimbizi" nchini Marekani, wasiotambulika kama wakimbizi au wasiopewa ulinzi wowote rasmi.

Wakati wa Vita vya Vietnam, raia wengi wa Marekani waliokataa vita na waliotaka kukwepa rasimu walitafuta hifadhi ya kisiasa nchini Kanada. Rais Jimmy Carter alitoa msamaha. Tangu mwaka wa 1975, Marekani imewapa makao mapya takriban wakimbizi milioni 2.6, huku takriban 77% wakiwa Wahindi wa Kichina au raia wa zamani wa Umoja wa Kisovyeti. Tangu kukubalika kwa Sheria ya Wakimbizi ya mwaka wa 1980, takwimu za kila mwaka za kusajiliwa zimeyumbayumba kati ya idadi juu ya 207,116 mnamo mwaka wa 1980 na idadi ndogo ya 27,100 mnamo mwaka wa 2002.

Hivi sasa, mashirika kumi ya kujitolea yanawapa wakimbizi makazi mapya kitaifa kwa niaba ya serikali ya Marekani: Huduma ya Kanisa ya Dunia, Baraza la Maendeleo ya Kijamii la Ethiopia, Wizara za Maaskofu za Uhamiaji Archived 10 Aprili 2011 at the Wayback Machine., Shirika la Kiyahudi la Usaidizi, Shirika la Kimataifa la Wokovu Archived 13 Juni 2009 at the Wayback Machine., Kamati ya Marekani ya Wakimbizi na Wahamiaji, , Huduma ya Uhamiaji na Wakimbizi ya Kilutherani, Mkutano Marekani wa Maaskofu wa Kikatoliki Archived 10 Januari 2010 at the Wayback Machine., Shirika la Kimataifa la Usaidizi na Jimbo la Iowa, Ofisi ya Huduma za Wakimbizi Archived 9 Oktoba 2009 at the Wayback Machine..

Kwa mfano, Ofisi ya Marekani ya kuwapa Wakimbizi Makazi Mapya (ORR kwa Kiingereza) inazipa fedha mashirika yanayotoa misaada ya kiufundi kwa mashirika ya kujitolea na mashirika ya kitaifa ya kuwatafutia wakimbizi makazi mapya. Kazi za Kikimbizi Archived 6 Januari 2010 at the Wayback Machine., lenye makao yake mjini Baltimore, MD., ndilo tawi la ORR linalopeana mafunzo na misaada ya kiufundi kwa ajili ya ajira na shughuli za kujitosheleza. Shirika hili lisilokuwa la kutafuta faida huwasaidia watoa huduma wa wakimbizi katika juhudi zao za kuwasaidia wakimbizi kuweza kujitosheleza. Shirika la Kazi za Wakimbizi linachapisha majarida meupe, majarida ya kawaida na ripoti kuhusu mada za ajira kwa wakimbizi.[138]

Kufifia kwa tofauti kati ya "wakimbizi" na "wahamiaji wa kiuchumi"[hariri | hariri chanzo]

Sio wahamiaji wote wanaotafuta hifadhi katika nchi nyingine hulingana na ufafanuzi wa "mkimbizi" katika makala ya 1a ya Mkataba wa Geneva. Mnamo mwaka wa 1951, wakati Nakala ya Mkataba ilipojadiliwa, vyama vya mkataba huo vilikuwa na wazo kuwa utumwa ulikuwa ni kitu cha zamani: kwa hivyo watumwa waliokuwa wakikimbia na kutoroka walikuwa kundi ambalo halikutajwa katika ufafanuzi huo, na pia aina nyingine iliyojitokeza: k.m. mkimbizi wa hali ya anga (tazama hapa chini).

Mnamo mwaka wa 2008 na 2009, hali ya kibinadamu ya kuhama kwa idadi kubwa ya Wazimbabwe, wakiingia nchi jirani ya Afrika Kusini, kulifanya tofauti kati ya "wakimbizi" na wa "wahamiaji wa kiuchumi" kufifia. Watu kama hao hawaambatani na jamii yoyote kikamilifu na wana mahitaji ya kijumla, haki na majukumu, yanayopatikana nje ya majukumu ya Ubalozi wa Umoja wa Mataifa wa Wakimbizi. Wao huanguka kati ya nyufa, kulingana na ripoti iitwayo Uhamiaji wa Kizimbabwe Kuingia Afrika Kusini: Mielekeo Mipya na Majibu, iliyozinduliwa mnamo Novemba 2009 na Mpango wa Masomo ya Uhamiaji wa Lazima (FMSP kwa Kiingereza) katika Chuo Kikuu cha Witwatersrand, Afrika Kusini. Kulingana na watafiti, ukosefu wa ulinzi wa wahamiaji katika kanda kulisababishwa na "tofauti isiyo ya kweli" kati ya kuwa mhamiaji wa kulazimishwa na mhamiaji wa kiuchumi. Ripoti hiyo ilipendekeza kuwa maneno bora zaidi yangekuwa "wahamiaji wa kulazimishwa wa kibinadamu", ambao wanahama kwa kusudi la kuishi kwao na kuishi kwa wanaowategemea.

Kusisitiza umuhimu wa mtazamio kawaida wa kibinadamu kuhusu kuhama kwa Wazimbabwe kuingia ofisi ya kanda hiyo, Ofisi ya Kanda ya Afrika Kusini ya Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Kuratibu Masuala ya Kibinadamu ilianzisha maneno "wahamiaji wanaofaa kushughulikiwa kidharura wa kibinadamu" mnamo mwaka wa 2008.

Majibu rasmi kuhusu uhamiaji wa Wazimbabwe nchini Botswana, Malawi, Zambia na Msumbiji bado yanaambatana na ufafanuzi wa awali kutoka Mkataba wa mwaka wa 1951, na hivyo basi nchi hizi zinasemekana kushindwa kuwalinda Wazimbabwe na wananchi wao wenyewe. Waliokuwa wakivuka mpaka hawakuwa wakimbizi - wengi hata hawakuomba hadhi ya ukimbizi - na, kutokana na kiwango cha kuzoroteka wa kiuchumi nyumbani, hawangeweza hata kuchukuliwa kama wahamiaji wa kiuchumi wa "hiari". Kwa hivyo wengi wao hawalindwi kisheria, wala hawapokei msaada wa kibinadamu, kwani hawashughulikiwi na jukumu la miundo ya msaada inayotolewa na serikali na taasisi zisizo za kiserikali. Nchini Botswana, Zambia na Malawi, ukimbizi unapatikana kwa Wazimbabwe; nchini Msumbiji, waombaji wachache wa hadhi ya ukimbizi wamekataliwa kutokana na uamuzi wa serikali wa kuwatazama Wazimbabwe kama wahamiaji wa 'kiuchumi' na wala si wahamiaji wa kibinadamu wa kulazimishwa.

Isipokuwa Afrika ya Kusini, ulinzi na upatikanaji wa huduma katika nchi nyingi katika kanda inategemea kupokea hadhi ya ukimbizi, na zinahitaji wanaotafuta hifadhi kukaa katika makambi, hawawezi kufanya kazi au kusafiri, na hivyo kutuma pesa kwa jamaa waliobaki nyuma nchini Zimbabwe. Afrika ya Kusini ilitaka kuanzisha kibali maalum kwa ajili ya Wazimbabwe, lakini sera hiyo bado inaendelea kuangaliwa.

Wakimbizi wa hali ya hewa[hariri | hariri chanzo]

Ingawa hawaambatani na ufafanuzi wa wakimbizi uliowekwa katika Mkataba wa Umoja wa Mataifa, watu wanaokimbia makazi yao kutokana na madhara ya mabadiliko ya hali ya hewa mara nyingi wameitwa "wakimbizi".[139] or "climate change refugees".[140]

Kupanda kwa uwiano wa maji baharini na kuongezeka kwa joto duniani kunatishia usalama wa chakula na uhuru wa nchi nyingi na kuwaathiri wengi duniani kote. Vipimo vya juu zaidi vya joto vinatarajiwa kuinua maji ya bahari, kuyeyusha barafu na kuacha theluji ndogo juu ya milima, na kusababisha sehemu za barafu za Greenland na ya eneo la Antaktiki kuyeyuka. Jopo la Kimataifa la Mabadiliko ya Hali ya Hewa (IPCC kwa lugha ya Kiingereza) linakadiria kwamba eneo la bahari lenye maji la wastani la kimataifa litapanda kwa kiasi cha kati ya mita 0.18-0.59 (futi 0.6 na 2) katika karne ijayo.[141], huku vyanzo vingine vikidokeza kwamba hitimisho hili ni la upeo wa chini. Majarida ya Sayansi na Sayansi Jiolojia ya Maumbile yalitumia data ya kupima kutoka karne iliyopita ili kutabiri kuwa kiwango cha maji cha bahari kinaweza kupanda hata futi 5 zaidi (mita 0.5-1.4) kufikia mwaka 2100 na kuongezeka kwa inchi 6 kila mwongo.[142][143] Mifano hii inatoa ushahidi kwamba watu wa maatoli, visiwa, na eneo la Kiaktiki watakuwa wakimbizi.

Katika maeneo ya kitropiki na maeneo yanayoelekea kuwa ya kitrokipi na hata katika maeneo yanayopatikana nje ya tropiki ambapo uzalishaji wa mazao na mifugo unachukua nafasi muhimu katika uchumi wa maeneo hayo, kuna uwezekano mkubwa sana wa kuathiriwa na kupanda kwa joto duniani na baada ya hapo shida za uhaba wa chakula.[144] Ukame uliokithiri na vifo vinavyotokana na njaa vitazidi, na kusababisha "viwango visivyotarajiwa vya uhamiaji kutoka kaskazini kwenda kusini, na kutoka vijijini kwenda mijini, na kutoka nchi zisizo na njia za kwenda baharini hadi nchi zinazopakana na bahari" kama ilivyoonekana kati ya miaka ya mwishoni mwa 1960 na miaka ya mapema ya 1990 na Sahel.[144]

Wakimbizi kama vitisho vya usalama[hariri | hariri chanzo]

Mara chache sana, wakimbizi wametumika na kuajiriwa kama wakimbizi wapiganaji,[145] na misaada ya kibinadamu inayoelekezwa kwa kuwasaidia wakimbizi imetumika mara chache sana kwa ununuzi wa silaha.[146] Msaada kutoka nchi inayopokea wakimbizi imetumika nadra sana kuwawezesha wakimbizi kuhamasishwa kijeshi, na kuwezesha vita kuenea nje ya mipaka.[147]

Matatizo ya kawaida matibabu ya wakimbizi[hariri | hariri chanzo]

Wakimbizi wa Kikorea katika meli ya Majeshi wanamaji wa Marekani

Mbali na majeraha ya kimwili au njaa, asilimia kubwa ya wakimbizi huonyesha dalili za ugonjwa unaotokana na kukabiliana na shida nyingi (PTSD kwa Kiingreza) au unyogovu. Matatizo haya ya muda mrefu ya kiakili yanaweza kuzuia kutenda kazi kwa mtu katika hali za kila siku; yanafanya mambo kuwa hata mabaya zaidi kwa watu waliotimuliwa ambao wanakabiliwa na mazingira mapya na changamoto mpya. Wao pia wamo katika hatari kubwa ya kujiua.[148]

Miongoni mwa dalili nyingine, ugonjwa unaotokana na kukabiliana na shida nyingi unahusisha wasiwasi, kuwa chonjo sana, kutolala, dalili za uchovu mwingi, matatizo ya kusongesha sehemu za mwili, kudhoofika kwa kumbukumbu ya muda mfupi, kusahau, mazingaombwe na kupooza-usingizi. Kukumbuka visa vibaya vya awali kila mara ni dalili ya ugonjwa huo: mgonjwa anawaza tukio la mateso, au vipande yake, tena na tena. Unyogovu pia ni dalili ya wagonjwa wa PTSD na pia huweza kutokea bila kuambatana na PTSD.

Ugonjwa wa PTSD ulipatikana katika watoto 34.1% wa Kipalestina, wengi ambao walikuwa wakimbizi, wa kiume, na wenye kufanya kazi. Washiriki walikuwa watoto 1,000 kati ya umri wa miaka 12 hadi 16 kutoka mashirika ya kiserikali, ya kibinafsi, na shirika la Umoja wa Mataifa la kuwasaidia wakimbizi, shule za UNRWA katika eneo la Yerusalemu ya Mashariki na maeneo mbalimbali katika Ufuo wa Magharibi.[149]

Utafiti mwingine ulionyesha kuwa 28.3% ya wakimbizi wanawake wa Kibosnia walikuwa na dalili za PTSD miaka mitatu au minne baada ya kuwasili nchini Uswidi. Wanawake hawa pia walikuwa na hatari zaidi ya kuwa na dalili za unyogovu, wasiwasi, na dhiki ya kisaikolojia kuliko wanawake waliozaliwa nchini Uswidi. Kwa unyogovu, uwezekano wa uwiano ulikuwa 9.50 miongoni mwa wanawake wa Kibosnia.[150]

Utafiti wa Idara ya Afya ya Watoto na Matibabu ya Dharura katika Chuo Kikuu cha Boston cha Matibabu ulionyesha kuwa asilimia ishirini ya wakimbizi - watoto kutoka Sudan wanaoishi nchini Marekani walikuwa na utambuzi wa ugonjwa unaotokana na kukabiliana na shida nyingi. Pia walikuwa na uwezekano wa kuwa na matokeo mabaya zaidi katika Maswali ya Kupima Afya ya Watoto.[151]

Utafiti mwingi wa aina hii unaashiria matatizo sawa. Utafiti mmoja wa kimeta ulifanywa na idara ya Elimunafsia ya magonjwa ya akili yasiyokuwa ya kawaida ya Chuo Kikuu cha Oxford katika Hospitali ya Warneford nchini Uingereza. Utafiti ishirini tofauti ulichunguzwa, na kutoa matokeo ya wakimbizi wazima 6,743 kutoka nchi saba. Katika utafiti mkubwa zaidi, 9% walipatikana kuwa na ugonjwa unaotokana na kukabiliana na shida nyingi na 5% na unyogovu mkuu, pamoja na ushahidi wa kinafsia wa kuwa na maradhi zaidi ya moja. Utafiti tano mbalimbali wa watoto wakimbizi 260 kutoka nchi tatu kulionyesha kuwepo kwa ugonjwa unaotokana na kukabiliana na shida nyingi kwa kiwango cha 11%.

Kulingana na utafiti huu, wakimbizi wanaopata makao mapya katika nchi za Magharibi wanaweza kuwa na uwezekano mara kumi zaidi wa kuwa na PTSD wakilinganishwa na watu wa umri sawa wa jumla ambao ni wakazi wa kiasili wa nchi hizo. Duniani kote, makumi ya maelfu ya wakimbizi na wakimbizi wa zamani ambao walipata makao mapya katika nchi za Magharibi wana ugonjwa unaotokana na kukabiliana na shida nyingi.[152]

Unyonyaji[hariri | hariri chanzo]

Wakimbizi huwa watu wenye woga na wanaoishi mbali na mazingira waliyoyazoea. Kuna uwezekano wa kuwa na matukio ya unyonyaji mikononi mwa maafisa wa kutekeleza sheria, raia wa nchi waliyohamia, na hata walinda amani wa Umoja wa Mataifa. Matukio ya ukiukaji wa haki za binadamu, watoto kulazimishwa kufanya kazi, mateso/majeraha ya kiakili na kimwili, majeraha yanayotokana na unyanyasaji, na unyonyaji kingono, hasa wa watoto, hutokea mara kwa mara.

Katika makambi mengi ya wakimbizi katika nchi tatu za Afrika ya Magharibi zilizoadhirika kivita: Sierra Leone, Guinea, na Liberia, wasichana wachanga walipatikana wakifanya ngono kwa ajili ya pesa, kiganja cha matunda, au hata kipande cha sabuni. Wasichana wengi miongoni mwa hawa walikuwa kati ya umri wa miaka 13 na 18. Katika visa vingi, ikiwa wasichana walikuwa wamelazimika kubaki, wangelazimishwa kuolewa. Walipata mimba walipokuwa na umri wa wastani wa miaka karibu 15. Hili lilitokea hivi karibuni tu, mnamo mwaka wa 2001. Wazazi walipuuza mambo haya kwani unyonyaji kingono ulikuwa "mfumo wa maisha katika makambi haya.[153]

Siku ya Wakimbizi Duniani[hariri | hariri chanzo]

Msichana kutoka Syria akiwa mkimbizi jijini Istanbul, Uturuki.

Siku ya Wakimbizi Duniani huadhimishwa tarehe 20 mwezi Juni. Siku hiyo iliundwa mnamo mwaka wa 2000 na azimio maalum la mkutano Mkuu wa Umoja wa Mataifa. Tarehe 20 mwezi Juni hapo awali ilikuwa ikiadhimishwa kama Siku ya Wakimbizi wa Afrika katika nchi kadhaa za Kiafrika.[154]

Nchini Uingereza Siku ya Wakimbizi Duniani huadhimishwa kama sehemu ya Wiki ya Wakimbizi. Wiki ya Wakimbizi ni tamasha la kitaifa lilioundwa ili kukuza uelewano na kusherehekea mchango wa kitamaduni wa wakimbizi, na huhusisha matukio mengi kama vile muziki, ngoma na maigizo[155].

Katika Kanisa Katoliki, Siku ya Wahamiaji na Wakimbizi Duniani huadhimishwa kila mwezi Januari kuanzia mwaka 1914, ilipoanzishwa na Papa Pius X[156].

Vitabu[hariri | hariri chanzo]

  • David Weissbrodt The human rights of non-citizens, Oxford: Oxford UP, 2008
  • Richard Perruchoud & Katarína Tömölová (ed.) Compendium of international migration law instruments, The Hague: T.M.C. Asser Press, 2007
  • Guy S. Goodwin-Gill The refugee in international law, Oxford: Clarendon Press, 2007 (1983, 1996)
  • Richard Plender (ed.) Basic documents on international migration law, Leiden: Nijhoff, 2007 (orig. 1988)
  • Peter W. Van Arsdale Forced to flee - human rights and human wrongs in refugee homelands, Lanham, MD: Lexington Books, 2006
  • Stephen H. Legomsky Immigration and refugee law and policy, Westbury, NY: Foundation Press, 2005 (1992, 1997)
  • James C. Hathaway The rights of refugees under international law, Cambridge: Cambridge UP, 2005
  • Christina Boswell The ethics of refugee policy, Aldershot: Ashgate, 2005
  • Susan F. Martin The uprooted - improving humanitarian responses to forced migration, Lanham, MD: Lexington Books, 2005
  • Prakash Shah (ed.) The challenge of asylum to legal systems, London: Cavendish, 2005
  • Stephen John Stedman & Fred Tanner (ed.) Refugee manipulation - war, politics, and the abuse of human suffering, Washington, D.C.: Brookings Institution Press, 2003
  • Omprakash Mishra & Anindyo J. Majumdar (ed/) The elsewhere people - cross-border migration, refugee protection and state response, New Delhi: Lancer, 2003
  • Niraj Nathwani Rethinking refugee law, The Hague: Nijhoff, 2003
  • Arthur C. Helton The price of indifference - refugees and humanitarian action in the new century. Oxford: Oxford UP, 2002
  • James C. Hathaway The law of refugee status, Toronto: Butterworths Canada, 2001 (orig. 1991)
  • Manik Chakrabarty Human rights and refugees - problems, laws and practices, New Delhi: Deep & Deep Note, 2001
  • Manoj Kumar Sinha Basic documents on international human rights and refugee laws, Delhi: Manak, 2000
  • Ivor C. Jackson The refugee concept in group situations, The Hague: Nijhoff, 1999
  • Elizabeth Adjin-Tettey A feminist analysis of the convention refugee definition, Ann Arbor, MI: UMI, 1999
  • Frances Nicholson & Patrick Twomey (ed/) Refugee rights and realities - evolving international concepts and regimes, Cambridge: Cambridge University Press, 1999
  • Pirkko Kourula Broadening the edges - refugee definition and international protection revisited, The Hague: Nijhoff, 1997
  • James C. Hathaway (ed.) Reconceiving international refugee law, The Hague: Nijhoff, 1997
  • Jean-Yves Carlier (ed.) Who is a refugee? a comparative case law study, The Hague: Kluwer Law International, 1997
  • Jean Aitchison International thesaurus of refugee terminology, Dordrecht: Nijhoff, 1996 (orig. 1989)
  • Patricia Tuitt False images - law's construction of the refugee, London: Pluto Press, 1996
  • Paul Weis The Refugee Convention, 1951 - the travaux préparatoires analysed, Cambridge: Cambridge UP, 1995
  • Gil Loescher Beyond charity - international cooperation and the Global Refugee Crisis, New York: Oxford UP, 1993
  • Office of the United Nations High Commissioner for Refugees Handbook on procedures and criteria for determining refugee status - under the 1951 convention and the 1967 protocol relating to the status of refugees, Geneva: Office of the United Nations High Commissioner for Refugees, 1992 (orig. 1988)
  • Louis B. Sohn & Thomas Buergenthal (ed.) The movement of persons across borders, Washington, D.C : American Society of International Law, 1992
  • Göran Rystad (ed.) The uprooted - forced migration as an international problem in the post-war era, Lund : Lund University Press, 1990
  • Alex Takkenberg & Christopher C. Tahbaz The collected Travaux préparatoires of the 1951 Geneva Convention relating to the Status of Refugees, Amsterdam : Dutch Refugee Council, 1989/1990
  • David Matas & Ilana Simon Closing the doors - the failure of refugee protection, Toronto: Summerhill Press Downsview, 1989
  • Aristide R. Zolberg, Astri Suhrke & Sergio Aguayo Escape from violence - conflict and the refugee crisis in the developing world, New York: Oxford UP, 1989
  • Göran Melander The two refugee definitions - Protection of refugees in Europe as seen in 1987, Lund: Raoul Wallenberg Institute, University of Lund, 1987
  • Guy S. Goodwin-Gill International law and the movement of persons between states, Oxford: Clarendon Press, 1978
  • Atle Grahl-Madsen The status of refugees in international law, part I Refugee character, part II Asylum, entry and sojourn, Leiden: Sijthoff, 1966 and 1972
  • Robert Kee Refugee world, London: Oxford UP, 1961
  • John George Stoessinger The refugee and the world community, Minneapolis: The University of Minnesota press, 1956
  • Jacques Vernant The refugee in the post-war world, London: Allen & Unwin, 1953
  • Norman Angell & Dorothy Frances Buxton You and the refugee - the morals and economics of the problem, Harmondsworth, Middlesex : Penguin Books, 1939
  • John Hope Simpson The refugee problem - report of a survey, London: Oxford UP, 1939
  • Harold Fields The refugee in the United States, New York: Oxford UP, 1938

Vidokezo[hariri | hariri chanzo]

  1. Nakala iliyohifadhiwa. Jalada kutoka ya awali juu ya 2010-01-13. Iliwekwa mnamo 2010-01-10.
  2. Refugees by Numbers 2006 edition, UNHCR
  3. Who is a Palestine refugee?. United Nations Relief and Works Agency for Palestine Refugees in the Near East. Jalada kutoka ya awali juu ya 2010-12-02. Iliwekwa mnamo 2009-09-21.
  4. Framework for Durable Solutions for Refugees and Other Persons of Concern, UNHCR Core Group on Durable Solutions, Mei 2003, p. 5
  5. Education in Azerbaijan. UNICEF.
  6. Global forced displacement trends. 2018 (Annexes). United Nations Convention Relating to the Status of Refugees (2018).
  7. Global forced displacement trends. 2017 (Annexes). United Nations Convention Relating to the Status of Refugees (2017).
  8. Global forced displacement trends. (Annexes) UNHCR Statistical Yearbook. United Nations Convention Relating to the Status of Refugees (2016).
  9. Global forced displacement trends. (Annexes) UNHCR Statistical Yearbook. United Nations Convention Relating to the Status of Refugees (2014).
  10. Global forced displacement trends. (Annexes) UNHCR Statistical Yearbook. United Nations Convention Relating to the Status of Refugees (2013).
  11. Global forced displacement trends. (Annexes) UNHCR Statistical Yearbook. United Nations Convention Relating to the Status of Refugees (2012).
  12. Global forced displacement trends. (Annexes) UNHCR Statistical Yearbook. United Nations Convention Relating to the Status of Refugees (2011).
  13. Global forced displacement trends. (Annexes) UNHCR Statistical Yearbook. United Nations Convention Relating to the Status of Refugees (2010).
  14. Global forced displacement trends. (Annexes) UNHCR Statistical Yearbook. United Nations Convention Relating to the Status of Refugees (2009).
  15. Global forced displacement trends. (Annexes) UNHCR Statistical Yearbook. United Nations Convention Relating to the Status of Refugees (2008).
  16. By the early 19th century, as many as 45% of the islanders may have been Muslim.
  17. Justin McCarthy, Death and Exile: The Ethnic Cleansing of Ottoman Muslims, 1821-1922, (Princeton, N.J: Darwin Press, c1995
  18. Greek and Turkish refugees and deportees 1912-1924 Archived 16 Julai 2007 at the Wayback Machine.. Universiteit Leiden.
  19. 19.0 19.1 [http://nobelprize.org/nobel_prizes/peace/laureates/1938/nansen-history.html Nansen International Office for Refugee: The Nobel Peace Prize 1938], nobelprize.org
  20. Old fears over new faces, The Seattle Times, 21 Septemba 2006
  21. U S Constitution - The Immigration Act of 1924. Jalada kutoka ya awali juu ya 2012-05-26. Iliwekwa mnamo 2010-01-10.
  22. Forced displacement of Czech population under Nazis in 1938 and 1943, Radio Prague
  23. Spanish Civil War fighters look back
  24. Statistisches Bundesamt, Die Deutschen Vertreibungsverluste, Wiesbaden, 1958; Alfred de Zayas, "Forced Resettlement", "Population, Expulsion and Transfer", "Repatriation" in Encyclopaedia of Public International Law, North Holland Publishers, Vols. 1–5, Amsterdam 1993–2003; Norman Naimark, The Russians in Germany, Harvard University Press, 1995; Alfred de Zayas, Nemesis at Potsdam, Routledge, London and Boston, 1977; Alfred de Zayas, "A Terrible Revenge" Palgrave/Macmillan 2006
  25. The United States and Forced Repatriation of Soviet Citizens, 1944-47 by Mark Elliott Political Science Quarterly, Vol. 88, No. 2 (Jun., 1973), pp. 253–275
  26. Repatriation -- The Dark Side of World War II. Jalada kutoka ya awali juu ya 2012-01-17. Iliwekwa mnamo 2010-01-10.
  27. Forced Repatriation to the Soviet Union: The Secret Betrayal
  28. Final Compensation Pending for Former Nazi Forced Laborers
  29. Forced Labor at Ford Werke AG during the Second World War. Jalada kutoka ya awali juu ya 2007-10-14. Iliwekwa mnamo 2010-01-10.
  30. The Nazi Ostarbeiter (Eastern Worker) Program
  31. Soviet Prisoners of War: Forgotten Nazi Victims of World War II. Jalada kutoka ya awali juu ya 2008-03-30. Iliwekwa mnamo 2010-01-10.
  32. Soviet Prisoners-of-War
  33. The warlords: Joseph Stalin
  34. Remembrance (Zeithain Memorial Grove). Jalada kutoka ya awali juu ya 2008-02-27. Iliwekwa mnamo 2010-01-10.
  35. Patriots ignore greatest brutality
  36. Joseph Stalin killer file. Jalada kutoka ya awali juu ya 2013-08-03. Iliwekwa mnamo 2010-01-10.
  37. Forced migration in the 20th century. Jalada kutoka ya awali juu ya 2015-10-21. Iliwekwa mnamo 2010-01-10.
  38. "United Nations Relief and Rehabilitation Administration," The Columbia Electronic Encyclopedia, © 1994, 2000-2005, on Infoplease, © 2000–2006 Pearson Education, publishing as Infoplease. (accessed 13 October 2006)
  39. "International Refugee Organization %u2014 Infoplease.com." The Columbia Electronic Encyclopedia, The Columbia Electronic Encyclopedia, © 1994, 2000–2005, on Infoplease, © 2000–2006 Pearson Education, publishing as Infoplease. (accessed 13 Oktoba 2006)
  40. What is resettlement? A new challenge. UNHCR. Iliwekwa mnamo 2009-07-19.
  41. 41.0 41.1 41.2 41.3 Resettlement: A new beginning in a third country. UNHCR. Iliwekwa mnamo 2009-07-19.
  42. 42.0 42.1 42.2 42.3 Understanding Resettlement to the UK: A Guide to the Gateway Protection Programme. Refugee Council on behalf of the Resettlement Inter-Agency Partnership (Juni 2004). Iliwekwa mnamo 2009-07-19.
  43. Evans, Olga; Murray, Rosemary (Februari 2009). "The Gateway Protection Programme: An evaluation". Home Office Research Report 12. Archived from the original on 2009-04-14. Retrieved 2010-01-10.  Check date values in: |date= (help)
  44. "EU plans to admit more refugees", BBC News, 2009-09-02. Retrieved on 2009-09-02. 
  45. Japan's refugee policy. Jalada kutoka ya awali juu ya 2015-02-16. Iliwekwa mnamo 2010-01-10.
  46. Sweeping changes to mandatory detention announced: ABC News 29/7/2008
  47. Australia abandons asylum policy: BBC News 29/7/2008
  48. 48.0 48.1 All I wanted was justice https://web.archive.org/web/20080110192141/http://www.haaretz.com/hasen/spages/941518.html
  49. Schwartz, Adi. "All I wanted was justice" Haaretz. 10 Januari 2008.
  50. 50.0 50.1 1,000 Africans estimated to have infiltrated Israel in 2 weeks, Tani Goldstein, Published: 02.18.08, Ynet news
  51. Nakala iliyohifadhiwa. Jalada kutoka ya awali juu ya 2009-12-04. Iliwekwa mnamo 2010-01-10.
  52. Luck of the Draw: Rohingya Refugees in Bangladesh. Jalada kutoka ya awali juu ya 2009-12-19. Iliwekwa mnamo 2010-01-10.
  53. Human Rights Watch : Rohingya Refugees from Burma Mistreated in Bangladesh
  54. Web site of Arakan Rohingya National Organisation
  55. On French immigrants, the words left unsaid. Jalada kutoka ya awali juu ya 2007-10-25. Iliwekwa mnamo 2007-10-25.
  56. For Pieds-Noirs, the Anger Endures
  57. Lebanon: Haven for foreign militants
  58. Lebanon Higher Relief Council (2007). "Lebanon Under Siege" Archived 27 Septemba 2006 at the Wayback Machine.. Retrieved 5 Machi 2007.
  59. Middle East crisis: Facts and Figures. BBC News Online (2006-08-31). Iliwekwa mnamo 2008-07-13.
  60. Michael Hirst. "Rise in radical Islam last straw for Lebanon's Christians", Daily Telegraph, 2007-04-03. Retrieved on 2021-07-13. Archived from the original on 2008-04-23. 
  61. EU donates €10 million to Western Sahara refugees
  62. Refugees and internally displaced persons. Jalada kutoka ya awali juu ya 2009-12-06. Iliwekwa mnamo 2010-01-10.
  63. Western Sahara: Lack of donor funds threatens humanitarian projects
  64. De Waal, Black Garden, p. 285
  65. Refugees and displaced persons in Azerbaijan. Jalada kutoka ya awali juu ya 2008-07-25. Iliwekwa mnamo 2010-01-10.
  66. Europe's Forgotten Refugees. Jalada kutoka ya awali juu ya 2011-10-08. Iliwekwa mnamo 2010-01-10.
  67. Radu, Michael. (2001). "The Rise and Fall of the PKK", Orbis. 45(1):47–64.
  68. Turkey: "Still Critical" - Introduction
  69. DISPLACED AND DISREGARDED: Turkey's Failing Village Return Program
  70. Prospects in 2005 for Internally Displaced Kurds in Turkey
  71. HRW Turkey Reports Archived 5 Juni 2011 at the Wayback Machine.
    See also: Report D612, Oktoba 1994, "Forced Displacement of Ethnic Kurds" (A Human Rights Watch Publication).
  72. [http://www.unhcr.org/iraq.html UNHCR | Iraq]
  73. Iraq refugees chased from home, struggle to cope
  74. U.N.: 100,000 Iraq refugees flee monthly. Alexander G. Higgins, Boston Globe, 3 Novemba 2006
  75. Anthony Arnove: Billboarding the Iraq disaster Archived 16 Juni 2010 at the Wayback Machine., Asia Times 20 Machi 2007
  76. Iraqi refugees facing desperate situation Archived 25 Januari 2010 at the Wayback Machine., Amnesty International
  77. 40% of middle class believed to have fled crumbling nation
  78. Iraq's middle class escapes, only to find poverty in Jordan. Jalada kutoka ya awali juu ya 2008-05-01. Iliwekwa mnamo 2008-05-01.
  79. '50,000 Iraqi refugees' forced into prostitution. Jalada kutoka ya awali juu ya 2008-07-08. Iliwekwa mnamo 2010-01-10.
  80. Iraqi refugees forced into prostitution. Jalada kutoka ya awali juu ya 2008-11-01. Iliwekwa mnamo 2010-01-10.
  81. US in Iraq for 'another 50 years' Archived 1 Oktoba 2009 at the Wayback Machine., The Australian, 2 Juni 2007
  82. Five years on Europe is still ignoring its responsibilities towards Iraqi refugees (PDF). ECRE. Jalada kutoka ya awali juu ya 2008-05-17. Iliwekwa mnamo 2008-09-03.
  83. Syria moves to restrain Iraqi refugee influx
  84. Syria to restricts Iraqi refugee influx
  85. Christians, targeted and suffering, flee Iraq
  86. Terror campaign targets Chaldean church in Iraq
  87. UNHCR |Iraq
  88. Christians live in fear of death squads
  89. 'We're staying and we will resist'
  90. Crawford, Angus. "Iraq's Mandaeans 'face extinction'", BBC News, 2007-03-04. 
  91. Damon, Arwa; Mohammed Tawfeeq and Raja Razek. "Iraqi officials: Truck bombings killed at least 500", CNN, 2007-08-15. 
  92. Iraq is disintegrating as ethnic cleansing takes hold. Jalada kutoka ya awali juu ya 2008-08-20. Iliwekwa mnamo 2008-08-20.
  93. "There is ethnic cleansing". Jalada kutoka ya awali juu ya 2010-10-12. Iliwekwa mnamo 2010-01-10.
  94. Satellite images show ethnic cleanout in Iraq, Reuters, 19 Septemba 2008
  95. [1] Archived 26 Septemba 2009 at the Wayback Machine.
  96. [2] Archived 3 Juni 2010 at the Wayback Machine.
  97. 97.0 97.1 "Afghan refugees given repatriation extension", IRIN, UN Office for the Coordination of Humanitarian Affairs, 2007-02-28. Retrieved on 2009-10-10. 
  98. Iranian Deportations Raise Fears of Humanitarian Crisis in Afghanistan. Jalada kutoka ya awali juu ya 2008-03-05. Iliwekwa mnamo 2010-01-10.
  99. To root out Taliban, Pakistan to expel 2.4 million Afghans
  100. "Afghanistan denies laxity in visa rules", Fars News Agency, 2009-10-06. Retrieved on 2009-10-10. Archived from the original on 2012-03-14. 
  101. Bhaumik, Subir. "Bhutan refugees are 'intimidated'", BBC News, 7 Novemba 2007. Retrieved on 2008-04-25. 
  102. 3.4 million displaced by Pakistan fighting. United Press International. 30 Mei 2009.
  103. India Archived 11 Juni 2008 at the Wayback Machine., The World Factbook. Retrieved 20 Mei 2006.
  104. Russians left behind in Central Asia, by Robert Greenall, BBC News, 23 Novemba 2005.
  105. For Jews in Tajikistan, the end of history is looming
  106. Tajikistan: rising from the ashes of civil war United Nations
  107. Focus on Mesketian Turks
  108. Meskhetian Turk Communities around the World. Jalada kutoka ya awali juu ya 2007-07-14. Iliwekwa mnamo 2007-07-14.
  109. For Pieds-Noirs, the Anger Endures, The New York Times, 6 Aprili 1988
  110. Flight from Angola, The Economist , 16 Agosti 1975
  111. Portugal - Emigration, Eric Solsten, ed. Portugal: A Country Study. Washington: GPO for the Library of Congress, 1993.
  112. Refugees Magazine Issue 131: (Africa) – Africa At A Glance, UNHCR
  113. Ugandan refugees recount black deeds of 'butcher of Kampala'
  114. UK Indians taking care of business
  115. Uganda's loss, Britain's gain
  116. African Union Force Ineffective, Complain Refugees in Darfur
  117. Arabs pile into Darfur to take land 'cleansed' by janjaweed. Jalada kutoka ya awali juu ya 2007-07-16. Iliwekwa mnamo 2010-01-10.
  118. European Council on Refugees and Exiles (ECRE) - Asylum in the EU. Jalada kutoka ya awali juu ya 2010-01-08. Iliwekwa mnamo 2010-01-10.
  119. Delete the Border Archived 3 Mei 2008 at the Wayback Machine. quoting Khaleej Times; ADN Kronos Archived 13 Machi 2007 at the Wayback Machine. Survivors of the immigrant boat tragedy accuse Greeks (in English) – [3] [4] [5]. The newspaper Hürriyet (in Turkish). Three of the drowned were Tunisians, one was Algerian, one Palestinian and the other Iraqi. The three disappeared were also Tunisians.
  120. Chavez: Europe risks oil over immigrant law
  121. Venezuela's Chavez Threatens to Deny Oil, Investments to EU Over Immigration Laws
  122. The Lives of the Hungarian Refugees, UNHCR
  123. "Day when tanks destroyed Czech dreams of Prague Spring" (Den, kdy tanky zlikvidovaly české sny Pražského jara) at Britské Listy (British Letters)
  124. internal-displacement.org. Jalada kutoka ya awali juu ya 2007-08-12. Iliwekwa mnamo 2010-01-10.
  125. Bosnia: Dayton Accords
  126. Resettling Refugees: U.N. Facing New Burden
  127. Serbia threatens to resist Kosovo independence plan
  128. Kosovo/Serbia: Protect Minorities from Ethnic Violence (Human Rights Watch)
  129. The World Factbook. Serbia. Central Intelligence Agency. Jalada kutoka ya awali juu ya 2009-04-02.
  130. Tanjug (22 Oktoba 2007). Serbia's refugee population largest in Europe. B92. Jalada kutoka ya awali juu ya 2007-11-12.
  131. Chechnya Advocacy Network. Refugees and Diaspora. Jalada kutoka ya awali juu ya 2014-06-15. Iliwekwa mnamo 2010-01-10.
  132. Ethnic Russians in the North of Caucasus - Eurasia Daily Monitor
  133. Bookman, Milica Zarkovic, "The Demographic Struggle for Power", (p. 131), Frank Cass and Co. Ltd. (UK), (1997) ISBN 0-7146-4732-2
  134. Human Rights Watch/Helsinki, RUSSIA. THE INGUSH-OSSETIAN CONFLICT IN THE PRIGORODNYI REGION, Mei 1996.
  135. 100,000 refugees flee Georgia conflict
  136. Internal Displacement. Global Overview of Trends and Developments in 2008. (PDF). IDMC. Iliwekwa mnamo 2009-06-28.
  137. Number of internally displaced people remains stable at 26 million Archived 21 Mei 2010 at the Wayback Machine.. Source: United Nations High Commissioner for Refugees (UNHCR). 4 Mei 2009.
  138. RefugeeWorks Mission Statement Archived 5 Julai 2010 at the Wayback Machine.
  139. Kirby, Alex. "West warned on climate refugees", BBC News, 2000-01-24. Retrieved on 2009-07-17. 
  140. Strange, Hannah. "UN warns of growth in climate change refugees", The Times, 2008-06-17. Retrieved on 2009-07-17. 
  141. (http://www.epa.gov/climatechange/effects/coastal/index.html)Accessed Feb. 10 2009.
  142. Rahmstorf, Stephan. "A Semi-Empirical Approach to Projecting Sea Level Rise." Science. vol 315: Jan 19, 2007.
  143. Rohling, E.J and Grant, K. et al., "High rates of sea-level raise during the last interglaical period". Nature GeoScience. vol 1, pg 38–42. Published Online Dec. 16, 2007.
  144. 144.0 144.1 (Battisti, David and Naylor, Rosamond. "Historical Warnings of Future Food Insecurity with Unprecedented Seasonal Heat". Science.vol 323, pg 240–244. Jan. 9 2009)
  145. United Nations High Commissioner for Refugees (UNHCR) 1999 “The Security and Civilian and Humanitarian Character of Refugee Camps and Settlements.” UNHCR EXCOM Report
  146. Crisp, J. 1999 “A State of Insecurity: The Political Economy of Violence in Refugee-Populated Areas of Kenya.” Working Paper No. 16, “New Issues in Refugee Research.”
  147. Weiss, Thomas G. (1999). "Principles, politics, and humanitarian action". Ethics & International Affairs 13 (1): 1–22. doi:10.1111/j.1747-7093.1999.tb00322.x. 
  148. CNN.com - Detainee children 'in suicide pact' - January 28, 2002. Jalada kutoka ya awali juu ya 2008-12-19. Iliwekwa mnamo 2010-01-10.
  149. Khamis, V. Post-traumatic stress disorder among school age Palestinian children. Child Abuse Negl. 2005 Jan;29(1):81–95.
  150. Sundquist K, Johansson LM, DeMarinis V, Johansson SE, Sundquist J. Posttraumatic stress disorder and psychiatric co-morbidity: symptoms in a random sample of female Bosnian refugees. Eur Psychiatry. 2005 Mar;20(2):158–64.
  151. Geltman PL, Grant-Knight W, Mehta SD, Lloyd-Travaglini C, Lustig S, Landgraf JM, Wise PH. The "lost boys of Sudan": functional and behavioral health of unaccompanied refugee minors re-settled in the United States. Arch Pediatr Adolesc Med. 2005 Jun;159(6):585–91.
  152. Fazel M, Wheeler J, Danesh J. Prevalence of serious mental disorder in 7000 refugees resettled in western countries: a systematic review. Lancet. 2005 Apr 9–15;365(9467):1309–14.
  153. Aggrawal A. (2005) "Refugee Medicine" in : Payne-James JJ, Byard RW, Corey TS, Henderson C (Eds.) Encyclopedia of Forensic and Legal Medicine, Elsevier Academic Press: London, Vol. 3, Pp. 514–525.
  154. Kigezo:UN document
  155. Refugee Week (UK) About Us. Refugee Week. Jalada kutoka ya awali juu ya 2020-08-26. Iliwekwa mnamo 2021-11-27.
  156. "Day 10, Year of #Mygration: Pope Francis World Day of Migrants and Refugees, 14 January 2018", Research at The Open University, 2018-01-12. (en) 

Marejeo[hariri | hariri chanzo]

  • Mark Bixler, "The Lost Boys of Sudan: An American Story of the Refugee Experience," University of Georgia Press 2005
  • Refugee number statistics taken from 'Refugee', Encyclopaedia Britannica CD Edition 2004.
  • Peter Fell and Debra Hayes, "What are they doing here? A critical guide to asylum and immigration." Venture Press 2007.
  • Matthew J. Gibney, "The Ethics and Politics of Asylum: Liberal Democracy and the Response to Refugees," Cambridge University Press 2004
  • Michael Robert Marrus, The Unwanted: European refugees in the 20th century, Oxford University Press 1985
  • Dietmar Schultke, refugees in former East-Germany 1945-1990, in: "Keiner kommt durch - Die *Geschichte der innerdeutschen Grenze und Berliner Mauer, Aufbau-Verlag, Berlin 2008
  • Tony Waters, Bureaucatizing the Good Samaritan, Westview Press, 2001.
  • Aristide R. Zolberg et al.,"Escape from Violence," Oxford University Press, 1989.

Viungo vya nje[hariri | hariri chanzo]

Wikimedia Commons ina media kuhusu:
Simple English Wiktionary
Simple English Wiktionary
Wikamusi ya Kiswahili ina maelezo na tafsiri ya maana ya neno:

[15] Refugees United an internet search engine designed for refugees looking for lost family and friends worldwide