Mawese

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Tunda la mchikichi

Mawese ni mafuta ya kula yanayotolewa katika matunda ya mti wa mchikichi (Elaeis guineensis). Ni mafuta ya kupikia ya Afrika, hasa penye asili ya mchikichi kutokana na kupatikana kwa wingi katika nchi za kanda ya Guinea.

Mawese kutokana na nyama ya tunda[hariri | hariri chanzo]

Kuna aina mbili za mawese; mawese hasa hutolewa na nyama ya tunda, ina rangi nyekundu na vitamini nyingi. Inatumika kama mafuta ya kupikia ama moja kwa moja ikitolewa na wakulima wenyewe na kuonyesha rangi nyekundu. Kama mawese inatengenezwa kibiashara kiwandani rangi inaondolewa kwa njia ya kusafisha mafuta kwenye vichujio. Baada ya kusafishwa huwekwa kwenye makopo au chupa na kuuzwa madukani au kupelekwa nje. Mafuta haya yanatumika pia viwandani kwa kutengeneza majarini, sabuni, mishumaa, mafuta ya kupakaa mwilini na aina mbalimbali ya madawa na urembaji.

Dizeli ya mawese[hariri | hariri chanzo]

Mawese hutumika pia kiteknolojia tangu miaka ya nyuma kwa kutengeneza dizeli. Hasa nchini Malaysia teknolojia hii imesonga mbele. Malaysia inajaribu kupunguza gharama za kununua petroli na dizeli kwa kutengeneza kiwanda kikubwa cha kusafisha mawese kuwa dizeli. Sheria ya Malaysia inadai kuanzia mwaka 2007 ya kwamba dizeli yote inayouzwa nchini iwe na 5% dizeli ya mawese.

Mawese kutokana na kiini cha tunda[hariri | hariri chanzo]

Aina ya pili ni mafuta yanapatikana katika kiini cha tunda. Haya baadhi ya wenyeji huyaita mafuta ya mise. Mafuta haya yana halijoto ya kuyeyuka kwenye 26 – 28 . Hivyo kwa kawaida ni imara, si majimaji. Inatumika katika viwanda vya vyakula lakini pia kwa majarini. Yanatumika pia sana katika madawa ya urembaji na madawa ya kusafishia. Hata viwanda vya kutengeneza alumini hutumia aina hii ya mawese. Kuna biashara kubwa ya viini vya mchikichi (mise) kwa sababu husafirishwa bila kuharibu mafuta ndani yake.

Matatizo kutokana na matumizi makubwa[hariri | hariri chanzo]

Nchi zinazopanda michikichi hasa ni Malaysia na Indonesia zenye mavuno ya 80% ya mawese yotr duniani. Brazil na Kolumbia ziemanza vilevile kupanda michikichi kwa wingi. Uthai, Papua–Guinea Mpya na nchi za Afrika ya Magharibi zinachangia asilimia ndogo kwenye soko la dunia ya mawese.

Kwa jumla mawese ina nafasi ya pili duniani kati ya mafuta kutokana na mimea inayotumika zaidi baada ya mafuta ya soya.

Mawese katika historia ya Afrika ya Magharibi[hariri | hariri chanzo]

Mawese ilikuwa muhimu sana katika uchumi na historia ya Afrika ya Magharibi wakati wa karne ya 19 BK. Ulaya iliingia katika mapinduzi ya viwandani ikahitaji mafuta ya kutia grisi kwa ajili ya mashine za viwanda vyake. Mafuta haya yalipatikana katika nchi za Guinea hasa eneo la delta ya Niger.

Kiuchumi kwa nchi za Afrika ya Magharibi biashara ya mawese ilichukua nafasi ya biashara ya watumwa; hadi mwanzo wa karne ya 19 falme za pwani zilitajirika kwa kuwauzia wafanyabiashara Wazungu watumwa kwa ajili ya masoko ya Amerika.

Biashara hii ya watumwa ilipigwa marufuku polepole. Mabadiliko ya sheria katika Uingereza yalitangulia. Mapatano ya kimataifa kwenye Mkutano wa Vienna mwaka 1815 yalipakana biashara hii ikapungua hadi kwisha.

Umuhimu mpya wa Afrika ya Magharibi kwa ajili ya Ulaya ulikuwa mafuta ya mawese. Hasa viini vilipelekwa Ulaya kwa sababu mawese asilia huharibika haraka. Kabla ya kuwepo kwa viwanda Afrika kwenyewe viini viliweza kusafirishwa mbali bila kuharibu mafuta ndani yake. Mawese ya tunda lenyewe linaharibika kama haitengenezwi kwa kufuata mbinu mbalimbali zinazopatikana kiwandani lakini si rahisi kuzitumia katika uzalishaji wa kienyeji.

Marejeo[hariri | hariri chanzo]

Athari za kijamii na za kiikolojia za matengenezo ya mawese[hariri | hariri chanzo]

Habari nyingine za mawese[hariri | hariri chanzo]