Mapambano kati ya Israeli na Palestina

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Jeshi la Misri likivuka Mfereji wa Suez tarehe 7 Oktoba 1973.

Mapambano kati ya Israeli na Palestina ni ugomvi baina ya nchi ya Israeli na wakazi wa Palestina unaoathiri pia uhusiano na nchi jirani. Ugomvi huu ulianza katika karne ya 20 baina ya wakazi Wayahudi na Waarabu wa maeneo ambayo leo hii yako chini ya Israeli na Mamlaka ya Kitaifa ya Palestina. Ulisababisha tayari vita sita kati ya nchi ya Israeli tangu kuundwa kwake mwaka 1948 na jirani zake za Kiarabu. Mapambano yanaendelea, hayajapata suluhisho hadi sasa.

Mapambano yalianza wakati wa kuongezeka kwa uhamiaji wa Wayahudi katika maeneo ya Palestina yaliyokaliwa na Waarabu. Kuundwa kwa Dola la Israeli kulisababisha vita ya kwanza baina ya Israeli mypa na nchi zote za jirani. Hivyo ilikuwa pia chanzo cha mgongano kati ya Israeli na nchi za Waarabu kwa jumla.

Msingi katika itikadi

Mapambano hayo si ya kijeshi tu, bali yanaanza upande wa siasa na pia upande wa dini.

Wayahudi wa Ulaya waliokuwa wahamiaji wa kwanza kuja Palestina waliona uhamiaji wao kama kurudi kwenye nchi ya mababu wao kwenye mahali ambako taifa lao litazaliwa upya. Sehemu ya Wayahudi waliona mwendo wao si kurudi tu kwenye ardhi ya mababu kama taifa lakini pia utimiaji wa sala ya Kiyahudi yenye ombi la "kuonana katika Yerusalemu mwaka ujao". Mpaka leo wengine wanaona jambo hilo kutokana na ahadi za Mungu kwa taifa lao kadiri ya Tanakh (yaani Biblia ya Kiebrania).

Kumbe wakazi Waarabu wa Palestina waliona uhamiaji wa wageni kutoka Ulaya kama harakati ya kikoloni iliyolenga kutwaa ardhi yao. Tena Waislamu kadhaa wanaona ya kwamba, tangu itwaliwe na jeshi la Uislamu katika karne ya 7 ardhi ya Palestina - Israeli imekuwa nchi ya Kiislamu inayopaswa kutawaliwa na serikali ya Waislamu daima. Wakristo hawakuwa wengi, tena wamezidi kupungua kwa kuhama kutokana na ugumu wa hali yao wanaojisikia kubaguliwa kama kundi dogo hata kati ya Wapalestina.

Historia

Utangulizi: Pogromu, Uhamiaji na Uzayuni

Theodor Herzl, mwanzilishaji wa Uzayuni.
Wahamiaji Wayahudi kwenye Kibbutz ya Migdal wakati wa kazi shambani mwaka 1912

Katika karne ya 19 idadi kubwa ya Wayahudi waliishi katika maeneo kadhaa ya Milki ya Urusi [1] yaliyotwaliwa na milki hiyo mnamo 1800.

Uadui dhidi ya Wayahudi ulitokea dhidi ya utawala wa Kirusi [2] Kuanzia mwaka 1880 kulitokea ghasia mbalimbali ambako Wayahudi walishambuliwa katika miji ya Urusi. Wimbi la pili la ghasia hizo zilizoitwa pogromu likatokea mwaka 1905, ambapo Wayahudi zaidi ya 2000 waliuawa mjini Odessa [3]. Wakati ule Wayahudi wa Urusi walianza kuhamia nje: wengi wao walikwenda Marekani, lakini wachache walielekea Palestina.

Mapogromu yalikuwa pia chanzo cha harakati mpya ya Uzayuni (Zionism) kati ya Wayahudi wa Ulaya. Uzayuni ulilenga kuwapa Wayahudi eneo maalum ili wapate kujenga upya taifa katika dola lao wenyewe, ambako wangekuwa wenyeji, si kundi la pekee katikati ya watu waliowadharau.

Mwaka 1896 Theodor Herzl (1860-1904) aliandika kitabu "Dola la Wayahudi" alimodai kuundwa dola la pekee kwa ajili ya Wayahudi. Mkutano wa kwanza wa wafuasi wake ulichagua jina la "Zayuni" ambalo lilikuwa jina asilia la mlima wa hekalu mjini Yerusalemu; wakachagua jina hilo kwa sababu linataja mahali patakatifu zaidi pa Uyahudi. Mkutano huo uliazimia kuwa "Uzayuni unalenga kuunda makazi salama yaliyokubaliwa rasmi kwa ajili ya taifa la Kiyahudi katika nchi ya Palestina".

Wazayuni walikusanya pesa kote Ulaya wakanunua ardhi katika Palestina na kuanzisha vijiji kwa ajili ya Wayahudi waliohima huko.

Palestina katika Milki ya Osmani mwaka 1914

Tamko la Balfour na chanzo cha mapambano

Vita ya Kwanza ya Dunia ilikwamisha mipango yote kwa sababu Palestina ilikuwa sehemu ya Milki ya Osmani iliyoshiriki katika vita pamoja na Ujerumani na Austria dhidi ya Urusi, Ufaransa na Uingereza.

Mwaka 1917 wakati ambapo jeshi la Uingereza lilifaulu kusogea mbele kutoka Misri na kuingia Palestina, waziri wa mambo ya nje Arthur James Balfour alitoa tamko la Balfour yaani tamko rasmi kuwa Uingereza inataka kusaidia mipango ya kuanzisha makazi ya Kiyahudi katika Palestina. Wakati uleule Waingereza waliwaahidi Waarabu kuundwa kwa dola la Kiarabu kwenye maeneo yaliyokaliwa nao katika Milki ya Osmani. Lakini wakati huohuo walipatana na Ufaransa kuhusu ugawaji wa maeneo ya Kiarabu ya Milki ya Osmani.

Kwenye mkutano wa amani wa Paris wa mwaka 1919, ulioandaa Mkataba wa Versailles, mwakilishi wa Waarabu, Faisal bin Hussein bin Ali al-Hashimi, alipatana na mwakilishi wa Wazayuni, Chaim Weizmann, kuwa anakubali uhamisho wa Wayahudi kuja Palestina, na Palestina kuwa eneo la pekee tofauti na Dola la Waarabu ambayo Faisal alilenga kujenga Uarabuni pamoja na Syria na Irak. Haki za wakazi Waarabu zilitakiwa kulindwa na maendeleo ya pamoja kati ya wakazi Waarabu na Wayahudi kujengwa. Lakini Uingereza na Ufaransa waliendelea kugawa Mashariki ya Kati, hivyo Waarabu wengi hawakusikia ya kwamba mapatano ya Faisal yalikuwa na umuhimu tena.

Baada ya vita Uingereza ilichukua utawala wa Palestina kama eneo la kudhaminiwa kwa niaba ya Shirikisho la Mataifa. Idadi ya Wayahudi waliofika kutoka nchi za Ulaya iliongezeka, lakini bado Wayahudi wengi walihamia Marekani, si Palestina. Hata hivyo shirika za Uzayuni ziliendelea kununua ardhi, kuanzisha vijiji vya Ujamaa vilivyoitwa Kibbutz hata Tel Aviv ilikua kama mji wa Kiyahudi kandokando ya Yafo ya Kiarabu. Mnamo 1931 asilimia 17 ya wakazi wa Palestina walikuwa Wayahudi.

Katika Palestina mufti mkuu wa Yerusalemu, Mohammed Amin al-Husseini, alichukua uongozi wa Waarabu akapinga kufika kwa Wayahudi wapya. Serikali ya Kiingereza ilisitasita kuamua juu ya msimamo wake - haikuzuia kufika kwa Wayahudi, lakini haikuwasaidia kujiimarisha nchini.

Mashambulio dhidi ya Wayahudi yalianza mwaka 1921. Mwaka 1929 Wayahudi 67 waliuawa mjini Hebron.

Kati ya 1936 na 1939 kulitokea ghasia kubwa ya Waarabu dhidi ya polisi na jeshi la Kiingereza na dhidi ya makazi ya Wayahudi. Uingereza ulifaulu kukandamiza ghasia hii kwa jeshi lake. Kati ya Wayahudi vikundi vyenye silaha vilianzishwa vilivyolenga kutetea vijiji vya Kiyahudi na kulipiza kisasi kwa mashambulio. Vikundi hivyo viliendelea baadaye kuwa chanzo cha jeshi la Israeli.

Siasa ya chuki dhidi ya Wayahudi iliyoendeshwa na Chama cha Nazi chini ya dikteta Adolf Hitler katika Ujerumani na nchi nyingine za Ulaya iliongeza namba ya Wayahudi waliopaswa kuondoka kwao Ulaya. Miaka baada ya 1933 takriban wakimbizi Wayahudi 250,000 walifika Palestina - hii ilikuwa sababu moja ya ghasia ya Waarabu miaka 1936-1939. Hadi mwaka 1945 Wayahudi walikuwa asilimia 33 ya wakazi wote wa Palestina.

Baada ya vita kuu ya pili kulikuwa na laki za Wayahudi waliowekwa huru kutoka makambi ya KZ na wengi wao walielekea Palestina. Hapo Serikali ya Uingereza, iliyosita kuamua kama ilitaka kutekeleza ahadi zake kwa Waarabu au kwa Wayahudi, iliomba Umoja wa Mataifa kuamua juu ya hatua zijazo kwa ajili ya Palestina, maana ilikuwa eneo la kudhaminiwa na asili ya mamlaka hii ilikuwa imepita kutoka Shirikisho la Mataifa kwenda Umoja wa Mataifa.[4].

Kuundwa kwa Dola la Israeli

Mpango wa Umoja wa Mataifa wa mwaka 1947 ya kugawa Palestina

Mwaka 1947 Mkutano Mkuu wa Umoja wa Mataifa ulipigia kura mpango wa ugawaji wa Palestina. Mataifa 33 yalipiga kura ya ndiyo, 13 hapana, 10 hayakusimama upande wowote. Hivyo eneo la Palestina lilitakiwa kugawiwa kwa dola la Kiyahudi, dola la Kiarabu na mji wa Yerusalemu. Mamlaka ya Uingereza yalitakiwa kwisha tarehe 14 Mei 1948.

Waarabu walipinga ugawaji kwa kudokeza ya kwamba mpango wa ugawaji haukuwa adili kwa sababu zifuatazo. Mwaka 1947 Palestina ilikuwa na wakazi 1,845,000. Watu 1,237,000 au theluthi mbili walikuwa Waarabu, wakati watu 608,000 tu au theluthi moja walikuwa Wayahudi. Kumbe Dola la Kiyahudi lilitakiwa kupokea asilimia 56 cha ardhi, pamoja na maeneo yaliyofaa zaidi kwa kilimo ingawa mali ya Kiyahudi wakati ule ilikuwa asilimia 7 tu ya ardhi yote ya Palestina. Katika eneo la Dola la Kiyahudi takriban 40% ya wakazi wangekuwa Waarabu. Sehemu kubwa ya ardhi katika sehemu ya Dola la Kiarabu ilikuwa mlimani na haikufaa vema kwa ajili ya kilimo.

Wawakilishi wa Kiyahudi walisema idadi ya Wayahudi itaongezeka haraka kutokana na uhamiaji wa Wayahudi wengine - wakati ule walikuwa bado laki za Wayahudi katika makambi katika nchi za Ulaya, ni hao ambao hawakuuawa na Wajerumani katika Holocaust.

Mara baada ya azimio la UM, mapigano yalianza katika Palestina na kuwa vita ya wenyewe kwa wenyewe nchini. Vikundi vya wanamgambo wa Kiarabu vilishambulia makazi ya Kiyahudi kote nchini. Wayahudi pia walikuwa na vikundi vya wanamgambo.

Tarehe 14 Mei mkutano wa wawakilishi Wayahudi ulitangaza Dola la Israeli kama nchi mpya. Waingereza waliondoa jeshi lao.

Tarehe 15 Mei 1948 majeshi ya Misri, Yordani, Lebanoni, Syria na Irak yaliingia Palestina yakatwaa maeneo ya Kiarabu na kushambulia makazi ya Kiyahudi. Katika vita ya miezi 10 jeshi la Israeli lilifaulu kusimamisha wapinzani na kuwarudisha nyuma. Jeshi la Kiarabu pekee lenye uwezo lilikuwa Kikosi Arabu cha Yordani. Wakati wa kusimamisha mapigano Israeli ilikuwa imeongezeka maeneo yake ikatawala asilimia 78 za eneo la kukabidhiwa la awali yaani maeneo yote yaliyowahi kukusudiwa na Umoja wa Mataifa kwa ajili ya Dola la Kiyahudi pamoja na nusu ya maeneo yaliyokusudiwa kwa ajili ya Dola la Kiarabu.

Ukanda wa Gaza ulitawaliwa na Misri na Ukingo wa Magharibi wa Yordani (mto) pamoja na mji wa kale wa Yerusalemu ukawa chini ya milki ya Yordani.

Zaidi ya wakazi Waarabu 700.000 walilazimika kuondoka au walimkimbia kutoka miji na vijiji vyao, wakikaa nje ya maeneo yaliyotawaliwa sasa na Israeli. Waarabu 150,000 hivi walibaki ndani ya maeneo haya sasa kama raia Waarabu wa Israeli. Baada ya vita Israeli ilikataa kurudi kwa waliokuwa nje. Ndiyo asili ya Wakimbizi Wapalestina wanaoishi Syria, Lebanoni, Yordani na Misri, pamoja na hao wanaoendelea kukaa katika makambi katika maeneo ya Gaza na Ukingo wa Magharibi.

Madola yote ya Waarabu isipokuwa milki ya Yordani yalikataa kuwapa wakimbizi hao haki za uraia, na kwa hiyo hadi leo wajukuu wamebaki kama wakimbizi katika nchi za kigeni bila uraia; wakisafiri wanatumia vitambulisho vilivyotolewa na UM, wanakosa haki ya kutafuta kazi au kushiriki katika siasa kama raia wa kawaida, hata kama familia zimeshaishi katika nchi hizo hadi kizazi cha tatu au nne.

Wapalestina baada ya 1948

Jumuiya ya Nchi za Kiarabu ilianzisha taasisi iliyoitwa "Serikali kwa Palestina yote" (ing. All-Palestine Government, ar. حكومة عموم فلسطين hukumat 'umum Filastin) wakati wa vita (1948) iliyotambuliwa na nchi za Kiarabu isipokuwa milki ya Yordani. Ilikuwa na mamlaka fulani katika Ukanda wa Gaza pekee, ikafanya kazi chini ya usimamizi wa Misri na mwisho wa 1948 ilipelekwa Kairo ikafutwa na serikali ya Misri mwaka 1959.

Taasisi mpya ikaundwa mwaka 1964 kwa azimio la Jumuiya ya Nchi za Kiarabu ikaitwa PLO (Palestine Liberation Organization, ar.: منظمة التحرير الفلسطينية‎ [[munaẓẓamat at-taḥrīr al-filasṭīniyyah) ambayo ni maungano ya vikundi mbalimbali ya Kipalestina. Shabaha yake ilikuwa "ukombozi wa Palestina". Serikali ya Misri ilikuwa na athira kubwa katika PLO. Harakati ya Fatah mwanzoni haikushiriki. PLO iliendesha vikundi vya wanamgambo ya Fedayin Wapalestina walioshambulia mipaka ya Israel mara kwa mara.

Yordani na Israeli (kwa Wapalestina walioweza kubaki kwao) zilikuwa nchi pekee zilizowapa Wapalestina uraia, lakini katika nchi nyingine walibaki kama wakimbizi bila uraia. Makambi yao yaliangaliwa na shirika la Umoja wa Mataifa linaloitwa UNRWA.

Israel na majirani hadi 1973

Maeneo yaliyotwaliwa na Israeli baada ya vita ya siku 6 mwaka 1967 hadi mapatano ya Misri 1973

Baada ya vita ya 1948-1949 nchi jirani zilikataa kutambua dola la Israeli. Hali ya vita ikaendelea ingawa bila mapigano kati ya majeshi makubwa. Wanamgambo wa Wafedayin Wapalestina waliendelea kuvuka mpaka kutoka makambi ya wakimbizi na kushambulia vijiji vya Kiyahudi. Wanamgambo hao walipata mara nyingi silaha na mafunzo kutoka kwa majeshi ya Misri na Syria.

Vita ya 1948-1949 ilisababisha ghasia na mashambulio dhidi ya Wayahudi walioishi katika nchi za Kiarabu. Nchi kadhaa za Kiarabu ziliweka sheria za ubaguzi dhidi ya Wayahudi. Hivyo katika miaka baada ya kuundwa kwa Israeli karibu Wayahudi wote waliondoka au walifukuzwa katika nchi za Kiarabu na kufika kama wakimbizi katika Israel, Marekani au Ulaya. Jumla ya wakimbizi hao Wayahudi karibu ililingana na idadi ya Waarabu waliofukuzwa kutoka Palestina. Hivyo idadi ya wananchi Wayahudi wa Israeli iliongezeka sana.

Uhusiano mbaya kati ya Israeli na majirani Waarabu ulisababisha vita zaidi.

Mwaka 1956 Israeli ilishambulia Misri katika vita ya Suez kufuatana na mpango wa pamoja na Ufaransa na Uingereza baada ya kuona ununuzi wa silaha nyingi na Misri.

Mwaka 1967 jeshi la Misri lilikusanya vikosi vingi vya jeshi lake katika rasi ya Sinai ikafukuza walinzi wa amani wa UM na kufunga mlango wa Tiran hivyo kuzuia usafiri wa meli baina ya Israeli na Bahari Hindi. Israeli ikajibu kwa kushambulia Misri tarehe 5 Juni 1967 katika Sinai ikaharibu jeshi la Misri katika muda wa siku 6. Wakati huohuo milki za Yordani na Syria ziliamua kushikamana na Misri zikashambulia eneo la Israeli. Tokeo lake lilikuwa ya kwamba jeshi la Israeli likatwaa Ukingo wa Magharibi wa Yordani na pia milima ya Golan hadi maadui walisalimisha amri tarehe 10 Juni. Pia eneo lote la Sinai likatwaliwa na Israel na Mfereji wa Suez ulifungwa.

Vita ya Yom Kippur iliyofuata ilikuwa mashambulio ya Misri na Syria dhidi ya Israeli katika mwezi wa Oktoba 1973. Mashambulio yalianza kwenye sikukuu ya Kiyahudi ya Yom Kippur. Jeshi la Misri lilifaulu kuingia kwenye rasi ya Sinai na Syria kwenye milima ya Golan. Lakini Syria ilirudishwa nyuma haraka na Waisraeli walifikia kilomita 40 tu kutoka Dameski. Jeshi la Misri lilifeli zaidi hadi Israeli iliweza kuvuka mfereji wa Suez na kufunga kikosi kikubwa cha Wamisri nyuma ya mstari wa mapigano na kuingia katika mji wa Suez na hata kukaribia Kairo. Mnamo 23 Oktoba pande zote zilikubali kusimamisha mapigano kwa ombi la UM. Baada ya majadiliano marefu, kila upande ulirudisha wanajeshi wake kilomita kadhaa kwa kusudi la kuwa na umbali kati ya majeshi.

Misri na Israeli zikaendelea kuwa na majadiliano na kupatana kufanya amani mwaka 1978. Israeli iliondoka katika Sinai na nchi zote mbili zikafungua ubalozi katika nchi ya pili. Ukanda wa Gaza ulibaki chini ya Israeli.

Uamsho wa Wapalestina na PLO

Vita ya siku 6 ya 1967 ilileta uamsho kati ya Wapalestina katika makambi ya wakimbizi. Kundi la Fatah lililoundwa mwaka 1959 nchini Kuwait liliongeza sifa zake kutokana na kupigana na jeshi la Israeli mwaka 1968 katika kambi la Karame (Yordani). Fatah lilijiunga na PLO na mwenyekiti wake Yasser Arafat akawa mwenyekiti wa PLO. Alileta mwelekeo mpya kuwa Wapalestina wanapaswa kujikomboa badala ya kutegema nchi za Waarabu wengine. Vikundi vya PLO viliendelea na mashambulio pamoja na kutumia mbinu za kigaidi dhidi ya wananchi raia wa Israeli.

Tangu 1968 vikundi vya PLO viliteka nyara ndege au watu raia kwa shabaha ya kuwabadilisha na wafungwa Wapalestina katika Israeli. Hadi mwaka 1970 PLO ilikua kuwa na mamlaka kubwa nchini Yordani hadi jeshi la nchi hiyo iliwafukuza vikosi vya PLO kutoka milki ya Yordani.

Hapo Arafat na sehemu ya askari wake walihamia Lebanoni. Wakati wa vita ya wenyewe kwa wenyewe ya Lebanoni PLO ilichukua upande na kushiriki lakini sehemu nyingine za vikundi vya Kipalestina vilishikamana na serikali za nchi za Waarabu zilizoshiriki pia katika vita hiyo ndani ya Lebanoni. Baada ya mashambulio ya Israeli PLO ilifukuzwa kutoka Lebanoni na kuhamia Tunisia mwaka 1982.

Intifada ya kwanza

Katika miaka iliyofuata Wapalestina katika Ukanda wa Gaza na Ukingo wa Magharibi wa Yordani walisikia maisha kuwa vigumu zaidi. Wengi wao walikuwa vijana waliozaliwa chini ya utawala wa Israeli. Vijana wengi walikosa kazi. Hawakuwa na matumaini katika jitihada za PLO iliyokuwa mbali nao.

Basi, baada ya ajali ya barabarani ambako Wapalestina wanne waliuawa na gari la kijeshi la Israeli, mnamo Disemba 1987 ililipuka ghasia ya ghafla iliyoitwa intifada. Wapalestina waliandamana barabarani, watoto na vijana walitupa mawe dhidi ya askari wa Israeli. Kundi jipya la Hamas lilichokoza mwendo huu na kuongoza upinzani. Katika miezi iliyofuata Wapalestina 1,551 na Waisraeli 422 waliuawa.

Kutangazwa kwa "Dola la Palestina" na majadiliano kati ya PLO na Israeli

Mwaka moja baada ya intifada ya kwanza PLO katika mji wa Tunis ilitoa tamko la kutangaza "Dola la Palestina". Katika tamko hili PLO ilitambua kwa mara ya kwanza kuwepo kwa Israeli. Tamko hili lilikuwa msingi kwa nchi kama Marekani kutambua pia PLO kama mwakilishi wa Wapalestina na baadaye kwa majadiliano ya kwanza kati ya PLO na Israeli.

Wakati wa Vita ya Ghuba ya 1990/91 Arafat aliamua kuwa upande wa Saddam Hussein aliyeshambulia Kuwait. Hii ilisababisha kufukuzwa kwa Wapalestina wengi kutoka Kuwait baada ya vita na kushindwa kwa Iraq. Nchi za Kiarabu kama Misri na Saudia zilizowahi kusaidia PLO lakini zilichukua msimamo dhidi ya Saddam Hussein zilikata misaada yao kwa PLO. Kudhoofishwa kwa PLO kwa njia hii ilisaidia pia kuanzisha majadiliano ya moja kwa moja. Katika mkutano wa amani wa Madrid, Hispania, Wapalestina walishiriki kwa mara ya kwanza katika majadiliano na Israeli.

Mapatano ya Oslo na kuanzishwa kwa mamlaka ya kitaifa ya Palestina

Tangu Januari 1993 wawakilishi wa PLO na Israeli walikutana kwa siri mjini Oslo, Norwei. Arafat alitamka kutambua Israeli na kuachana na mbinu za kigaidi katika barua kwa kiongozi wa Israeli Yitzhak Rabin. Rabin na Arafat walikutana Washington, D.C. na kutia sahihi mapatano ya kwanza yaliyokuwa mwanzo wa mfuatano wa majadiliano marefu yaliyolenga kuleta amani kati ya Wapalestina na Israeli katika muda wa miaka 5.

Kwa jumla mapatano hayakuweza kufikia mwisho. Lakini katika hatua za kwanza Mamlaka ya Kitaifa ya Palestina yaliundwa kama mbegu ya serikali kamili. Jeshi la Israeli ilijiondoa katika Gaza na sehemu za Ukingo wa Magharibi wa Yordani zilizowekwa chini ya mamlaka mpya.

Mwaka 1995 uongozi wa PLO ulihamia Palestina na kuanzisha ofisi kuu ya Mamlaka ya Palestina huko Ramallah.

Kukwama kulisababishwa na shaka kama ifuatavyo:

  • katika jamii ya Israeli kama Arafat na upande wa Kipalestina walitaka kweli kujenga amani na kusimamisha ugaidi wakati mashambulio dhidi ya askari na wananchi raia wa Israeli yalipoendelea kutokea. Kilele cha upinzani ndani ya Israeli kilikuwa uuaji wa waziri mkuu Rabin mwaka 1995 uliofanywa na mpinzani Mwisraeli.
  • Katika jamii ya Wapalestina kama Israeli ilitaka kweli amani kwa sababu kujengwa kwa makazi kwa walowezi Waisraeli nje ya mipaka ya Israeli ya 1967 kuliendelea.
  • Sehemu ya vikundi vya kisiasa upande wa Palestina, hasa Hamas, ilikataa kukubali mapatano yaliyofikiwa.
  • Swali la pekee lilihusu hali ya Yerusalemu ya Mashariki ambayo Wapalestina wanaidai kama mji mkuu wao ambayo iko nje ya mipaka ya Israeli ya 1967. Lakini Israeli iliwahi kutangaza kuunganishwa kwa mji huu wote na kuitawala sehemu ya magharibi na ya mashariki kama mji mmoja wa Israeli usioweza kutengwa tena.
  • Tatizo ni pia suala la "haki ya kurudi" kwa ajili ya watoto na wajukuu wa wakimbizi Wapalestina wa mwaka 1948 wanaotaka kurudi kwenye makazi ya mababu yaliyo sasa ndani ya eneo la Israeli.

Katika uchaguzi wa mwaka 1996 chama cha Benyamin Netanyahu kilishinda kura ya bunge la Israeli. Netanyahu hakukubali majadiliano; alidai kuwa yaliimarisha tu wapinzani wakali wa Israeli upande wa Wapalestina na kusabisha mashambulio na ugaidi zaidi.

Mwaka 2005 jeshi la Israeli lilitoka kabisa katika Ukanda wa Gaza na kubomoa vijiji vya walowezi Wayahudi kule.

Mafarakano kati ya Wapalestina yaliendelea kuongezeka kati ya Fatah na Hamas. Mwaka 2007 Chama cha Hamas kilichukua mamlaka juu ya Gaza kikaendelea kushambulia Israeli kwa makombora. Israeli ilijibu kwa kufunga mipaka ya Gaza na kungilia ndani ya Ukanda wa Gaza kijeshi mara kadhaa.

Kutokana na mashambulio dhidi ya wananchi wa Israeli yaliyoendelea Waisraeli walianza kujenga fensi na ukuta wa kutenganisha Ufuko wa Magharibi na Israeli yenyewe. Ukuta huu wenye urefu hadi mita nane umesaidia kupunguza sana mashambulio dhidi ya raia, lakini umejengwa zaidi kwenye ardhi ya Kipalestina na kuongeza matatizo kwa wananchi.

Israeli inaendelea kujenga makazi na vijiji kwa walowezi wa Kiyahudi ndani ya eneo la Kipalestina. Jeshi lake linashika vituo vingi katika ufuko wa magharibi na kutawala mwendo wa watu huko na kuzuia usafiri mara kwa mara kwa kulinda usalama wake.

Farakano kati ya Hamas upande wa Gaza na Mamlaka ya Kipalestina mkononi mwa PLO-Fatah upande wa Ramallah haijapata suluhisho.

Tazama pia

Tanbihi

  1. katika nchi za kisasa za Poland, Belarus na Ukraine zilizokuwa chini ya Tsar wa Urusi wakati ule
  2. Maeneo penye Wayahudi wengi yalikuwa chini ya milki ya Poland hadi kugawanyika kwa Polandi kati ya majirani yake. Wayahudi waliowahi kuwa na uhuru fulani katika Poland walijikuta chini ya utawala wa Kirusi. Warusi ambao hawakuzoea Wayahudi wengi waliwabana wananchi wapya hao kwa sheria za ubaguzi.
  3. Ukraine ya leo
  4. Umoja wa Mataifa uliundwa wakati wa Vita Kuu ya Pili kama maungano ya mataifa yote yaliyopiga vita dhidi ya Ujerumani na Japani. Shirikisho la Mataifa lilijifuta yenyewe mwaka 1946 na kukabidhi shughuli zake zote kwa UM

Marejeo

Viungo vya nje

Vyanzo rasmi

Vyanzo vya kieneo

Israeli
Arab

Uchunguzi wa kitaalamu

Mapendekezo ya amani

Ramani

Vyanzo vya jumla