Waarusha

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Wachezaji Waarusha katika arusi wakati wa ukoloni mnamo 1936.

Waarusha ni kabila la watu linalopatikana kaskazini mwa Tanzania katika eneo la mlima Meru, Mkoa wa Arusha. Lugha yao ni Kiarusha inayohesabiwa kama lahaja ya Kimaasai[1]. Wakati wa kuja kwa wakoloni hao walikuwa wakazi wa eneo la mji wa Arusha wa leo.

Asili ya Waarusha

Kuna mawazo mawili juu ya asili ya Waarusha.

Wengine wanasema asili yao ni kundi la Wamaasai walioshindwa katika vita kati ya Wamaasai na hivyo kutafuta kimbilio kati ya wakulima; walianza kulima wenyewe na hivyo kutofautiana na Wamaasai wengine.[2] [3]

Wengine wanasema asili yao ni Wapare waliohamia mlima Meru kufuatana na mapatano na Wamaasai. Hapo walianza kutumia lugha ya Wamaasai na kupokea desturi nyingine. Wakati wa sotoka kubwa ya 1892 Wamaasai ambao mifugo yao walikufa wote walijiunga na Waarusha na hivyo kuimarisha athira ya utamaduni wa Kimaasai kati yao.[4]waarusha walitokea meru.

Kwa namna yoyote katika eneo la mlima Meru Waarusha walikuwa majirani wa karibu na Wameru wanaosema kwa lugha karibu na ya Wachagga. Wameru waliwahi kufika Meru mapema wakakalia sehemu za juu zaidi mlimani wakati Waarusha walianza chini zaidi. [5]. Mwanzoni walipigana kati yao lakini baadaye walianza kushirikiana kwa karibu hadi mwaka 1881 Wameru walikaribishwa kuunga vijana wao katika rika mpya ya Waarusha iliyoitwa "talala".

Zamani ya ukoloni

Katika miaka ya 1880 wakoloni Wajerumani walianza kufika katika eneo la Kilimanjaro kati ya Wachagga. Wakati ule Waarusha walikuwa wakishirikiana na machifu wa Wachagga katika vita vyao. [6]

Waarusha waliathiriwa sana na uenezi wa ugonjwa wa sotoka wa 1892 ulioua asilimia kubwa ya ng'ombe nchini. Wakidhoofishwa vile hata wakoloni Wajerumani walianza kufika wakajaribu kutawala maeneo.

Wajerumani waliingia polepole katika eneo la mlima Meru. Mara ya kwanza Waarusha walikutana nao mwaka 1881 wakati ambako kundi dogo la Wajerumani chini ya Hermann von Wissmann pamoja na Wachagga wa Moshi na kundi la Waarusha walishambulia Kibosho; mwaka 1885 walishambuliwa na Wajerumani kutoka Moshi chini ya Kurt Johannes kama kisasi kwa mashambulio yao dhidi ya makabila yaliyoshirikiana na Wajerumani.

Mwaka 1896 Ovir na Segebrock, wamisionari Wajerumani Walutheri waliuawa na vijana Waarusha; hapo kapteni Johannes alirudi na askari zake na kundi kubwa la Wachagga na kuharibu nchi ya Waarusha na Wameru mara mbili katika miaka 1896 na 1897.

Tanbihi

  1. http://multitree.org/codes/mas-aru Kiarusha katika multitree
  2. "Arusha were agro-pastoral Maasai who first settled on the southwestern slopes of the mountain in the 1830s during a period when struggles among pastoralists to control the plains were taking place" (Spear, uk. 2)
  3. Nakala iliyohifadhiwa. Jalada kutoka ya awali juu ya 2013-02-05. Iliwekwa mnamo 2013-02-26.
  4. http://www.ntz.info/gen/n01826.html#id01171
  5. Spear uk. 34
  6. Thomas Spear, Mountain Farmers: Moral Economies of Land & Agricultural Development in Arusha & Meru, University of California Press, 1997 , uk.30

Marejeo

Makala hii kuhusu utamaduni wa Tanzania bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Waarusha kama historia yake au mahusiano yake na mada nyingine?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.