Tabibu

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Tabibu akichungulia masikio ya mtoto

Tabibu (kutoka neno la Kiarabu; kwa Kiingereza: physician) ni mtu aliyesoma elimu ya tiba hadi kufikia kiwango kinachompa uwezo wa kutambua na kutibu magonjwa mbalimbali.

Tabibu anashirikiana na watu wengine waliojifunza sehemu za elimu ya afya na tiba kama vile wauguzi, wataalamu wa tibamaungo, tibaredio au uchunguzi wa maabara, wafamasia na wengineo. Kutokana na elimu yake ya juu tabibu ni yule anayefanya maamuzi kuhusu mwelekeo na matibabu na chaguo la dawa.

Kwa kawaida tabibu anatakiwa kutimiza masomo ya tiba kwenye chuo kikuu kwa miaka kadhaa. Masomo hayo ni pamoja na au yanafuatwa na vipindi vya kupata maarifa ya kazi akimsaidia tabibu mzoefu katika hospitali. Matabibu wengi wanaendelea kusoma elimu kwenye fani za pekee kama vile upasuaji, jinakolojia, tiba ya watoto, magonjwa ya akili na mengine.

Tabibu, mganga, daktari[hariri | hariri chanzo]

Tabibu akichukua sampuri ya damu kwa mtoto

Mara nyingi tabibu huitwa "daktari" ingawa hii si jina la elimu maalumu, bali ni cheo cha mtu aliyeonyesha kiwango cha juu katika mojawapo ya sayansi mbalimbali. Ni sahihi kwa tabibu aliyemaliza masomo yake hadi shahada ya uzamivu.

Jina la kimila kwa tabibu ni "mganga". Tamaduni zote za dunia zilikuwa na waganga waliopata elimu ya tiba ya jadi kwa viwango tofautitofauti. Lakini kwa kawaida hawana elimu ya kichuo na kutegemeana na mazingira mbinu zao zinaweza kuchanganywa na ushirikina, uchawi na imani potovu.

Kote duniani vifo vilipungua na watu kufikia umri mkubwa zaidi baada ya kupatikana kwa matabibu waliosoma tiba ya kisayansi.

Makala hii kuhusu mambo ya tiba bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Tabibu kama sababu yake au mahusiano yake na mada nyingine?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.